*Asisitiza,
soka ya Tanzania ni sawa na kibarua cha Mhindi…
Na Saleh Ally
SAKATA la kiungo nyota wa Simba, Amri Kiemba kutaka kujiunga na
Yanga na baadaye kubaki katika klabu yake hiyo limekuwa ni gumzo la chinichini
kwa kipindi kirefu sasa.
Taarifa za Kiemba kuwa katika hatua za mwisho kusaini Yanga
zilienea kila sehemu na hata baadhi ya wadau wa Yanga kutangaza amesajili
tayari, hali ambayo ilizua utata.
Pamoja na kwamba takribani mwezi sasa, bado kumekuwa na hamu kubwa
kwa mashabiki wengi wa soka kutaka kujua kama kweli kulikuwa na tukio kama hilo
au la.
Championi Ijumaa liliamua kukata mzizi wa fitna na kumtafuta
Kiemba ili aelezee kuhusiana na hali hiyo ya yeye kutakiwa na Yanga au zilikuwa
ni taarifa zisizo rasmi.
Awali baadhi ya viongozi wa Yanga walilizungumzia suala hilo na
kusema hawakuwahi kabisa kutaka kumsajili Kiemba kama ambavyo ilikuwa
imeripotiwa!
Kiemba ni kati ya viungo nyota nchini, amewahi kuchezea timu
mbalimbali na kufanya vizuri. Yanga, Moro United na Miembeni ni kati ya timu
alizosukuma gozi akiwa katika kiungo.
Ingawa umri unamtupa mkono taratibu, lakini ni kati ya wachezaji
gumzo kutokana na uwezo wake. Tayari timu za Israel na Morocco zimeonyesha nia
ya kutaka kumsajili kutokana na uwezo wake.
Katika mahojiano na gazeti hili, Kiemba ambaye anasifika kwa
kuzungumza moja kwa moja bila ya kupindisha maneno, anasema alikuwa tayari
kwenda Yanga kwa kuwa katika soka anachoangalia zaidi ni maslahi yake.
Kiemba anathibitisha kweli alifanya mazungumzo na Yanga baada ya
kumfuata na walikuwa wamefikia katika hatua ya mwisho kabisa baada ya yeye
kukubali kusaini kuichezea timu hiyo kwa mara nyingine.
Championi: Labda ilikuwaje kuhusiana na Yanga?
Kiemba: Walionyesha nia ya
kutaka kunisajili, nami niliwasikiliza na kutaka kujua walichonacho, basi
tutakaa ana kuzungumza.
SALEHJEMBE: Mazungumzo yenu yaliishia wapi?
Kiemba: Baada ya mazungumzo na kuwaeleza nilikuwa ninahitaji kiasi
gani, basi wao walikwenda kujipanga halafu wakarudi na kuniambia walikuwa
tayari kunipa dau ambalo nilikuwa nimetaka.
SALEHJEMBE: Sasa kipi kilikuzuia kusaini na kutua Jangwani tena?
Kiemba: Walipokuja nikiwa tayari kusaini kukajitokeza kitu kimoja
ambacho kikasababisha mambo yote kukwama katika hatua za mwisho.
SALEHJEMBE: Kitu kipi?
Kiemba: Yanga walikuwa na fedha zao ambazo ningechukua na kusaini,
tatizo likawa ni moja, mshahara. Walitaka kunipa mshahara ambao nilikuwa
naupata Simba, kitu ambacho sikukubaliana nacho.
SALEHJEMBE: Kiasi gani labda?
Kiemba: Kweli siwezi kutaja, ila Yanga walisema wana kiwango chao
cha wachezaji wa nyumbani wanacholipwa ambacho ni cha juu. Sasa mshahara wangu
ulikuwa umefikia zaidi ya hapo na mimi waliotaka kunipa nilikuwa nalipwa Simba.
Kama kweli ni suala la maslahi kusingekuwa na tofauti.
SALEHJEMBE: Sasa nini kikaendelea?
Kiemba: Nakumbuka ilikuwa Jumapili, nikaendelea kushikilia msimamo
na kuwaambia mshahara niliokuwa nataka, wao wakakwama hapo na mimi nikaona
basi.
SALEHJEMBE:Maana yake mngeelewana mshahara, basi ungesaini?
Kiemba: Hakika ingekuwa hivyo, kikubwa kwa sasa naangalia maslahi
maana soka ya Tanzania haina tofauti na kibarua cha Mhindi.
Championi: Una maanisha nini?
SALEHJEMBE: Kama unafanya kazi kwa ‘Mhindi’, siku moja anaweza kuamka
na kusema, “wewe, leo hakuna kazi, kwenda jumbani”. Siku hiyohiyo kibarua
kikawa kimeisha.
SALEHJEMBE:Sasa vipi ukaamua kusaini Simba na awali ulikuwa
umeamua kusaini Yanga?
Kiemba: Nilikuwa nimemaliza Simba mkataba miezi miwili iliyopita
na hawakuwa wamenifuata na walionekana hawako siriazi. Katika hali ya kawaida
nilianza kujua wanaweza wasinitake tena au vinginevyo, kama nilivyokuambia soka
ni sawa na kibarua cha Mhindi.
SALEHJEMBE: Sasa baada ya hapo Simba ikawaje?
Kiemba: Sijui walipata taarifa za Yanga, maana siku hiyohiyo usiku
walianza kunipigia simu na Jumatatu wakanifuata na kunipa mkataba ambao
niliwaomba waniachie ili niupitie na watu wangu wausome halafu watauijia,
nikabaki nao.
SALEHJEMBE:Yanga walikuwa mmeishashindwana?
Kiemba: Hapana, huenda wangerudi, niliona hizo dalili, lakini baada
ya kuusoma mkataba wa Simba na kuwapa watu wangu siku hiyo ya Jumatatu,
nikawarudishia lakini wao ili kuonyesha wamepania na huenda hofu ya Yanga,
wakaacha fedha kabisa zikalala mapokezi.
SALEHJEMBE:Mwisho ukaamua nini?
Kiemba: Jumanne ndiyo siku niliyosajili Simba, maana walirudi na
mkataba wakiwa wamefanya marekebisho ambayo kwangu niliona si sahihi. Basi,
tukafikia mwafaka na kusaini.
SALEHJEMBE: Yanga hawakurudi tena?
Kiemba: Nafikiri walisikia nimeishasaini Simba tena, hivyo hakuna
aliyerudi tena.
SALEHJEMBE: Kwa hiyo tofauti ya mshahara waliotaka kukupa Yanga na
wanaokulipa Simba ni kiasi gani?
Kiemba: Sitataja, ila mshahara wa Simba ni mzuri zaidi.
SALEHJEMBE:Sawa, ninashukuru sana kwa uwazi na ushirikiano, ninakutakia
maandalizi mema katika mechi ya michuano ya Chan dhidi ya Uganda.
Kiemba: Nashukuru sana.
0 COMMENTS:
Post a Comment