April 16, 2014


Na Saleh Ally
KUNA watu ambao hupaswa kupewa heshima yao, lakini inawezekana kabisa wakawa hawaipati kwa kuwa wanaotakiwa kufanya hivyo wanakuwa hawafikirii mambo mengi kuhusu wao.

Mshambuliaji wa Azam FC, Gaudence Mwaikimba ni kati ya wachezaji wanaopaswa kupewa heshima ya kuwa mmoja wa wachezaji wanaoendelea kung’ara katika Ligi Kuu Bara pamoja na kuhama timu moja kwenda nyingine.
Mwaikimba, msimu huu amefikisha zaidi ya misimu saba akiwa kwenye ligi hiyo, lakini bado ameendelea kuwa nyota na mchezaji muhimu kwa kila njia.
Azam FC imetwaa ubingwa wake wa kwanza wa Ligi Kuu Bara baada ya kuifunga Mbeya City siku chache tu zilizopita, lakini Mwaikimba ambaye amekuwa chachu na mhimili wa mechi za mwisho za timu hiyo, yeye amefikisha kombe la nne.
Mwaikimba ametwaa makombe matatu ya Ligi Kuu Bara akiwa na Yanga, sasa ameongeza moja akiwa na Azam FC, maana yake ni kati ya wachezaji wachache wanaocheza ligi kuu wakiwa na mataji kama yake.
Hiyo ni sehemu ya kuonyesha mshambuliaji huyo ambaye hana makeke na aliyekuwa kipenzi cha mashabiki wa Yanga wakati anaichezea timu hiyo, anastahili heshima yake kutokana na kazi yake nzuri kwa kipindi kirefu sasa.
Kocha Joseph Marius Omog raia wa Cameroon alisema Mwaikimba atapewa nafasi katika mechi za mwisho kwa kuwa ana kazi maalum ya kufanya. Kweli mechi mbili za mwisho ambazo Azam ilijihakikishia kutwaa ubingwa baada ya kuwa inahitaji pointi sita tu, Mwaikimba akafanya kazi yake.
Mechi dhidi ya Ruvu Shooting ambayo siku ya kwanza iliahirishwa kutokana na mvua kubwa, ilipopigwa siku iliyofuata, Azam FC ikashinda kwa mabao 3-0 na Mwaikimba alikuwa wa kwanza kufungua mlango wa wanajeshi hao ambao walikuwa hawajafungwa kwenye uwanja wao wa nyumbani wa Mabatini, Mlandizi.
Azam FC ikawa imebakiza pointi tatu tu kuwa bingwa na kazi ilikuwa ngumu maana ni dhidi ya Mbeya City, Mwaikimba akaanza tena, safari hii akiwa na John Bocco na bila ajizi, Mwaikimba akafunga bao la kwanza wakati timu yake ikishinda mabao 2-1 na kutwaa ubingwa Bara.
Mwaikimba amecheza Ligi Kuu Bara tangu akiwa na Tukuyu Stars ya Mbeya, baadaye Ashanti United, Yanga, Kagera Sugar na Moro United kabla ya kutua Azam FC.
Hakuna anayeweza kukataa suala la Mwaikimba kupewa heshima yake kwa mengi, kuwa mmoja wa wachezaji wachache wenye mafanikio. Amecheza timu kubwa, ndogo lakini ameendelea kukusanya mafanikio.

Mwaikimba ameliambia Championi Jumatano kwamba, mara kadhaa watu wamekuwa wakisema amekwisha, lakini hawafanyi tathmini vizuri.

Kuisha:
Watu hawafanyi tathmini, hauwezi kusema mtu ameisha wakati hachezi. Inawezekana mfumo tu wa kocha, ndiyo maana unaona nikicheza ninafanya vizuri. Watu wapime mtu anayecheza na asiyecheza.

Kukata tamaa:
Usipokuwa makini unaweza kukata tamaa, lakini kwangu ni tofauti kwa kuwa ninajiamini lakini nina moyo wa subira, pia ninaamini kwenye nafasi kwamba siku ikifika nitapata na mimi nitacheza. Lakini kawaida, ninamuunga mkono anayecheza namba moja na mimi.
Mfano John (Bocco), anapocheza ninamuunga mkono kwa kuwa pointi tatu kwa timu ni kwa wote. Siku na mimi nikipata nafasi, najitahidi kufanya vizuri. Angalia mechi dhidi ya Ashanti United, Bocco na Kipre (Tchetche) hawakucheza, tulishinda bao nne na nikafunga mawili.

Mechi:
Sijacheza mechi nyingi, nyingi niliingia lakini nimeanza mechi sita na nimefunga mabao matano. Ninauamini uwezo wangu, ninalalia kwenye subira ndiyo maana utaona ninaendelea kufanya vizuri.
Azam FC sasa timu kubwa, hilo watu lazima wakubali. Kama ningekuwa sina uwezo, wasingenibakiza hapa, wanajua nina uwezo upi na mimi nasisitiza najiamini.

Kocha:
Kweli alisema kuna mechi ningecheza, kanipa nafasi sikumuangusha kocha (Omog). Kwangu hata kama sikucheza mechi nyingi namuona ni kocha bora na alibadili sana uchezaji wetu.
Utaona uchezaji wa Azam FC ugenini na nyumbani ulikuwa tofauti, kulikuwa na maelekezo yake. Hivyo ni kocha anayejua nini anachofanya hadi sasa.


 SOURCE: CHAMPIONI JUMATATU



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic