July 25, 2014



 
MAXIMO AKIWA NA TEGETE
UMESIKIA gumzo kuhusiana na wachezaji wapya wa Yanga, hasa wale raia wa Brazil, Geilson Santana maarufu kama Jaja na Andrey Coutinho?


Jamaa hawa ndiyo wamekuwa gumzo zaidi huku mashabiki wa Yanga wakiwa na hamu kubwa kuwaona wakiwa wanapambana uwanjani kuisaidia Yanga kufanya vizuri kwenye Ligi Kuu Bara na michuano ya kimataifa.

Hakuna hata mmoja kwa Watanzania ambaye amewahi kuwaona Jaja na Coutinho wakicheza mechi ya kirafiki au ya mashindano.

Lakini katika mazoezi ya Yanga yanayoendelea kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari ya Loyola, Mabibo jijini Dar es Salaam, hakuna ubishi inaonyesha kuwa ni wachezaji ambao kama watajituma, basi watatoa upinzani kwa wengine watakaokutana na Yanga na wanaweza kuwa msaada kwa kikosi hicho kinachoongozwa na Mbrazili mwenzao, Marcio Maximo.

Awali walionekana kama vile wazembe, lakini mazoezi yanavyoendelea, wanaonekana kubadilika na kufanya vizuri zaidi. Hata hivyo wakati watakapoanza kucheza mechi, bado pia watalazimika kuzoea mambo kadhaa kwa kuwa kuna mambo mengi kwao ya kujifunza kupitia Ligi Kuu Bara.

Wakati yote hayo yanasubiriwa, kuna mambo kadhaa ya kuangaliwa mapema ambayo nitagusa pande mbili, kuanzia kwa kocha na wachezaji wenyewe na hasa wale wazalendo.

Tanzania ina vipaji vingi sana katika kila mchezo na soka ni mmojawapo. Hakuna anayeweza kukataa kuhusiana na uwezo wa wachezaji kama vile Jerry Tegete ambaye amekuwa msaada mkubwa kwa Yanga kabla ya kuanza kuyumba taratibu msimu uliopita.

Umri bado unamruhusu Tegete, kwa kuwa hajafikisha miaka 27 ambayo ungeweza kuhesabu kwamba anaanza kuinama kwenda ukingoni, maana yake ana nafasi kubwa ya kurekebisha alichokosea na kufanya vizuri msimu ujao.

Tegete, Said Bahanuzi na Hussein Javu bado ni sehemu ya wachezaji wazalendo ambao Tanzania inaweza kuwategemea katika vikosi vya timu ya taifa au kuwa changamoto katika kuendelea kwa soka nchini.

Hivyo, wakati wenyewe wanatakiwa kujiamini na kujituma, basi hata upande wa benchi la ufundi linaloongozwa na Marcio Maximo linapaswa kuwaamini na kuwapa nafasi.

Sitaki kuingilia anachokifanya Maximo, safari hii yuko kwenye klabu na si timu ya taifa lakini bado suala la wazalendo kupata nafasi ya kucheza litakuwa ni jambo zuri kwa kuwa ujio wa Jaja na Coutinho au wageni wengine ni kuongeza changamoto na kukua kwa soka ya hapa nyumbani.

Hivyo haiwezi kuwa sahihi kama watakua wageni tu na wenyeji wakabaki palepale, maana yake soka ya nyumbani haitakuwa imepiga hatua maana baadaye wageni wataondoka na soka ya nyumbani itaendelea kubaki hapo ilipo, haitakuwa sahihi.

Kuendelea kuwakuza au kuwafanya kina Tegete na wenzao kuwa imara zaidi ni kuwapa nafasi kulingana na nafasi iliyopo. Lakini bado nasisitiza suala hili linategemeana katika pande zote mbili.

Kwamba mwalimu atoe nafasi na atafanya hivyo akiona juhudi za upande wa pili, yaani kwa wachezaji. Moja mazoezini, lakini pili kwenye mechi, kama watapata nafasi basi wamuonyeshe kocha hakukosea, maana yake hivi; wafunge au kuisaidia timu kama alivyotaka kocha au zaidi.

Pia kwa kocha, awe ‘flexible’. Kama wageni hawafanyi vizuri, basi wasiendelee kupata nafasi kwa lazima, badala yake nao wakutane na changamoto kwamba anayefanya vizuri ndiye atakayepewa nafasi ya kwanza, hii itawasaidia kujituma zaidi na kuwa msaada kwa kikosi chake.

Nyongeza ni kuhusiana na ushirikiano, linaweza kuwa jambo zuri zaidi, kwamba kama kutakuwa na kutopendana basi hakuna maana ya timu, hakuna sababu ya wachezaji wa kigeni na wenyeji watafeli na mwisho kutakuwa ni kufeli kwa Yanga.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic