July 23, 2014



Na Saleh Ally
BADO nitakuwa naendelea kukumbushia kuhusiana na namna ambavyo nimekuwa nikihadithiwa na wazee mbalimbali wa Yanga na Simba ambao niliomba kukaa nao kwa lengo la kujifunza.


Nimekuwa nikitaka kujua mengi kuhusiana na historia ya Yanga na Simba, sijali sana kama wakati mwingine inachanganya, kitu kizuri ni kwamba, nimekuwa nikijifunza mengi.

Moja ya mambo ambayo yamekuwa yakinivutia na kunifanya nitake kujua mengi zaidi ni namna walivyoishi kwa kushirikiana na upinzani wao ukawa ni uwanjani iwe Simba dhidi ya timu nyingine au siku wanapokutana wenyewe watani.

Kwamba kama kuna msiba, aliyefariki ni mwanachama au shabiki wa Yanga, basi Simba walikwenda msibani na kuwataka wafiwa kukaa kando na wenyewe wangefanya taratibu zote za mazishi hadi mwisho.


Huo ndiyo ulikuwa mfumo wa klabu hizo, ndiyo maana kuna mzee mmoja shabiki na mwanachama wa Simba, siku zote amekuwa akikaa kwenye jukwaa la Yanga huku akiendelea kutaniana na mashabiki na wanachama wa Yanga.

Kawaida, wanachama wa Yanga wamekuwa wakimuwekea kiti kuhakikisha hakosi nafasi, ili anapofika pale aendeleze utani wao na ukikaa karibu yake ni burudani ya kutosha.

Huo ndiyo mpira, soka ni mchezo wa raha tupu, kweli ni biashara lakini burudani yake ndiyo imefanya uwe unaingiza fedha nyingi hadi kujipatia umaarufu.

Nchi kama Rwanda ambazo zilivurugwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe, mfano wa mauaji ya kimbari mwaka 1994, zinautumia mchezo huo kurudisha umoja, lakini ajabu hapa nyumbani wako watu, tena ni vijana wanakwenda tofauti, haijulikani ni wapi!


Siku chache zilizopita, mashabiki wa Simba wamechoma jezi ya Yanga yenye namba 7 ikiwa na jina la Coutinho, yule Mbrazil ambaye Yanga imemsajili kwa ajili ya msimu ujao.

Mashabiki bao walimvua jezi hiyo shabiki mmoja wa Yanga aliyekuwa ameivaa na kujitokeza kwenye mazoezi Simba yaliyokuwa yanafanyika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Kisa ni kwa nini amejitokeza kwenye mazoezi hayo? Waliamini haikuwa sahihi yeye kwenda pale na mwisho wakamvua jezi na kuichoma. Si jambo zuri, si jambo la kimichezo na si sahihi kwa uongozi wa Simba kukaa kimya bila ya kusema lolote.

Waliofanya hivyo ni watu wachache sana, wanaweza wakawa wanachafua sifa ya Simba wengi ambao wana sifa ya ustaarabu na urafiki. Simba ina sifa ya kuwa na mashabiki na wanachama wavumilivu na waelewa zaidi kwenye soka, kwamba timu yao imecheza vipi na si walalamishi kupita kiasi.

Hawa wengine wametokea wapi? Tena wanafikia hatua ya kuchoma jezi ya timu pinzani, hali inayoashiria uhasama, uadui ambao unawashawishi wengine pia kujibu mapigo na mwisho itakuwa ni kuumizana. Nani amezungumza na kukemea hilo?

Jambo ambalo limefanywa na watu wasiojua michezo na hasa wa soka maana yake nini, watu ambao hawajui historia au chimbuko la Simba na Yanga na namna walivyoishi huko nyuma hadi wao wakazikuta timu hizo sasa.

Wamechoma jezi, eti shabiki wa Yanga ameenda mazoezi ya Simba kwenye Uwanja wa Chuo Kikuu Dar es Salaam. Hawaoni matumizi ya viwanja vya chuo hicho, watu wangapi wanafanya pale? Kuna tenisi, judo, kikapu, netiboli na mingine. Je, ni kiwanja cha Simba? Hata kingekuwa, vipi iwe hivyo, hawa watu vipi?

Kawaida nafanya mazoezi kwenye viwanja vya Chuo Kikuu Dar es Salaam tangu nikiwa ‘kula kulala’ hadi leo najitegemea. Hakuna suala la rangi na si uwanja wa klabu, hivyo mashabiki waliofanya hivyo watakuwa ni wageni katika jiji hili au eneo hilo. Ndiyo maana nataka wajifunze ili siku nyingine wasichafue sifa nzuri ya Simba, undugu wa Yanga na Simba na amani ya soka nchini.

Angalia sura na maumbo yao, hakuna ubishi ni vijana na sura zao ni za kisasa. Lakini wana mawazo duni kuhusiana na mchezo wa soka ambao umekuwa ukitumika kumaliza uadui na uhasama na mwisho kurudisha umoja, lakini wao wanautumia kujenga uadui tena, watu wa aina gani hawa wasio na haya wala kutaka kujifunza?

Inawezekana wengi wanalichukulia tukio hilo kama utani, lakini ni baya na linaweza kuwa tatizo kubwa, pengine ingekuwa vizuri kusikia hata Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) likifumbua mdomo na kusema jambo kuhusiana na suala hilo.

Kwangu nitakuwa nina maombi mawili, naanza na upande wa vijana kwa kuwa bado nipo kwenye kundi hilo. Kuwa ni vizuri kuachana na ushabiki wa fuata mkumbo au kutaka sifa. Wapo mashabiki wanaokuwa wendawazimu wanapokuwa mbele ya wenzao na wanataka kuonyesha wanazijua au kuzipenda sana timu na klabu zao.

Ukiwauliza, hawajalipa ada au si wanachama kabisa. Ikiwezekana hawajawahi kuiunga mkono Simba au Yanga kwa lolote lile. Badala yake vitendo vya kipuuzi au maneno mengi tu, lengo kuonyesha wanajua sana, kumbe hakuna lolote!

Nawaomba vijana, wanaoshabikia soka na hasa Yanga na Simba, kuachana na tabia za sifa zisizokuwa na mpaka, tabia za kutaka kuonekana sana kwenye makundi ya watu, mwisho wake zina madhara na faida zake ni chache sana.

Pili, kwa mashabiki na wanachama wa Yanga, wanapaswa kulichukulia suala hilo la mashabiki wa Simba kuchoma jezi ni la kipuuzi, lililofanywa na watu wasioelewa lolote.

Uwanja wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ni sehemu ya watu wote, hivyo waamini Simba wengi hawatakuwa wamefurahishwa na hilo na wao Yanga hawana sababu ya kulichukulia kwa uzito na mwisho kulipa kisasi.

Wajue wakilipa kisasi, watamuumiza Simba ambaye hakushiriki kwenye tukio hilo. Wanaweza kulaani kilichotokea kwa lengo la kuonyesha njia na mwisho kurekebisha, lakini si kulipa kisasi.





1 COMMENTS:

  1. HAWA KAKA NI WATANI WAJADI WALA HAKUNA MBORA HAPA NI KWAHI TU NA UTANI HAUNA KISASA WALA KIZAMANI, LAKINI SHABIKI UNAUMIA,MWANACHAMA UTANI

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic