August 30, 2014



Suala la Emmanuel Okwi kutangaza kuwa Yanga imevunja mkataba wake na sasa ataitumikia Simba, limezua sekeseke na sasa ni mtafutano kila kona, kama ni vita sasa hii ndiyo inaanza kukolea.


Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji, amefunguka kuwa wametoa siku saba kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutoa majibu sahihi juu ya Simba kumtangaza Okwi kuwa mchezaji wao wakati bado kuna kesi inayoendelea baina ya Yanga na Okwi.

Kuonyesha kuwa wapo ‘serious’ na hicho wanachokifanya, Manji amesema kuwa ikiwa TFF haitatoa majibu ya kueleweka kwao ndani ya siku saba, basi moja kwa moja watatua katika Shirikisho la Soka la Afrika (Caf), ikiwa pia hapo hakutaeleweka ndani ya siku saba, basi wataelekea Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) kwa ajili ya suala hilo.

Manji alionekana kutokuwa na utani kwenye kauli zake, alionekana kukerwa na kitendo cha Okwi kutua Simba na kusema kuwa Yanga imevunja mkataba wake, ndiyo maana ameamua kwenda kuichezea Simba.

Waipa siku saba TFF
“Tumepeleka barua TFF, leo (Ijumaa) asubuhi kutoa malalamiko kuhusiana na Simba kumsainisha Okwi wakijua wazi kuwa ana mkataba na sisi wa miaka miwili.

“Hii ni barua yetu ya tatu baada ya mbili tulizopeleka mwezi wa tano na wa saba juu ya malalamiko kwa Okwi kutoitumikia Yanga kutofanyiwa kazi.

Kutinga Fifa
“Tumetoa siku saba kwa TFF kulitolea ufafanuzi suala hili na kutoa maamuzi juu ya kilichofanyika na iwapo maamuzi hayatatolewa ndani ya muda huo, tunatarajia kuwasilisha malalamiko yetu Fifa na ikishindikana tutaliwasilisha katika Mahakama ya Michezo nchini Uswisi (CAS).

Simba hawajui sheria za soka
“Viongozi wa Simba wameshindwa kufanya suala la uungwana kwa kufuata sheria za mpira kama zinavyoeleweka, wangekuja kuwauliza kwani hatukatai kuuza wachezaji ila sheria ifuatwe.

“Mfano mzuri kina Frank Domayo na Didier Kavumbagu wamesajiliwa, hatujalalamika kwa kuwa walifuata utaratibu unaotakiwa.

“Upande wangu naona ni jambo la kawaida kushirikiana, hata mimi nilimpongeza (Evans) Aveva alipochaguliwa kuwa rais kwani ndiyo mambo ya mpira yalivyo.

Waongeza dau la fidia
“Dau la awali kabla ya kusaini Simba tulitaka alipe fidia ya dola 200,000 (Sh milioni 320) lakini baada ya kuamka leo tumeongeza dola 500,000 (Sh milioni 800), kwa hiyo jumla ni dola 700,000 (Sh bilioni 1.12). Hii tutawadai Simba na Okwi mwenyewe.

Wataka Okwi afungiwe maisha
“Tumepeleka malalamiko TFF ikiwezekana mchezaji huyo afungiwe maisha, pamoja na wakala wake kutoshiriki masuala ya soka hapa Tanzania kutokana na ukiukwaji wa sheria alioufanya ikiwa ni wazi kuwa bado ana mkataba na klabu yake ya awali.

Apendekeza Simba ishushwe daraja
“Kutokana na kitendo walichokifanya Simba wasinione mbaya iwapo timu itashushwa daraja kutokana na kumsajili mchezaji aliyekuwa na mkataba kwa kutofuata sheria, iwapo walikuwa wanahitaji kumnunua wangekuja na kuzungumza nasi.

“Kwani sisi huwa tunaachana vizuri na wachezaji wetu, mfano mzuri Fred Mbuna na Shadrack Nsajigwa ambaye kwa sasa amerudi kuja kufundisha Yanga, hii ni kutokana na kuachana vizuri.

Atishia kuinunua Simba
“Mimi nina uwezo wa kununua wachezaji wote wa Simba na nikawalipa mshahara na jambo hilo naliweza, ila tunachoangalia ni kufuata kanuni na sheria za soka.

“Kwani hata sisi tungeweza kumchukua (Amissi) Tambwe kutokana na kumuona ni mchezaji mzuri na kumsajili Yanga lakini hatuwezi kufanya hivyo kwa kuwa tunatambua sheria na mchezaji huyo ana mkataba ambao tunauheshimu.

“Hata hivyo Klabu ya Yanga ina mfuko mrefu kuliko Simba.

Jina lake limo katika usajili TFF
“Tumewasilisha majina sita ya wachezaji wa kimataifa akiwemo Okwi kwa kuwa hatukupata majibu yetu mapema kutoka TFF.

“Iwapo wangetupatia taarifa mapema tungeamua kumuacha mchezaji mmoja, hata Jaja na kumwambia akakae kwa miezi sita kisha angerudi tena kucheza.

“Siyo kwamba tunalalamika kuwa tunamhitaji mchezaji huyo kwani kuna wachezaji wengi na tunaweza kwenda kusajili sehemu mbalimbali duniani ila tunataka sheria ifuatwe.

Okwi ataka kukutana na Manji 
“Okwi alikuja ofisi kwangu na kutaka kuonana na mimi lakini nikawa bize akaambiwa na katibu muhtasi wangu kuwa atapangiwa siku, kweli akapangiwa siku, hakutokea, akapigiwa simu hakupokea lakini alitumiwa meseji hakuweza kujibu wala kutokea tena.

Akana kuvunja mkataba
“Hatujawahi kuvunja mikataba na wachezaji wa Simba, kwani hata Juma Kaseja tulisubiri mkataba uishe ndiyo tukaingia naye mkataba…

“…Ndiyo maana tulimsajili pia Kelvin Yondani baada ya mkataba wake kumalizika, hatukuvunja sheria.

Waunda kamati ya sheria
“Kesho (leo) tunatarajia kutangaza kamati yetu mpya ya sheria ambapo ilikuwa ni mpango wa muda mrefu, kwani tumeona ni muhimu kuwa na kamati hii na isifikiriwe kuwa imetokana na suala la Okwi,” alisema Manji.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic