August 27, 2014





Na Saleh Ally
SIKU zinavyosonga mbele na mambo yamekuwa yakibadilika kwa kila namna, hivyo kila jambo linafanyika katika mfumo unaolenga ushindani zaidi.
Ushindani umekuwa mkubwa karibu kwenye kila jambo kwa kuwa kinacholengwa ni mafanikio na mambo mengi zaidi yanakwenda kibiashara.
Katika mechi ya kirafiki kati ya wakongwe wa Real Madrid dhidi ya wenyeji wao Tanzania Eleven iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Jumamosi iliyopita, kulikuwa na mambo mengi ya kujifunza.
Hata kabla ya mechi hiyo nilieleza namna ambavyo tunaweza kujifunza badala ya kwenda kuangalia tu muonekano wa sura za akina Luis Figo, Cristian Karembeu na wenzao.

Wakati nakwenda uwanjani nilitamani kujifunza mengi na nikiwa pale kweli hilo lilitokea ingawa kuna jambo niliona lilikuwa ni sahihi kulijadili kwa pamoja na wadau wa soka kwa ajili ya maendeleo ya mpira wetu.
Mashabiki walijitokeza kwa wingi sana siku hiyo, inawezekana iliwashangaza wengi sana kuona mechi tu ya wakongwe inahudhuriwa na watu wengi namna ile.

Karibu kila aliyefika uwanjani pale alionyesha kushangazwa na idadi ile kubwa ya mashabiki ingawa wako waliokuwa wakiwazia mengine, eti “waandaaji wamepiga mkwanja aisee”.

Kwa kuwa waandaaji walipambana hadi kufikia kuwaleta Madrid kitu ambacho kilionekana hakiwezekani, basi wana haki ya “kupiga” hizo fedha kama kweli itakuwa hivyo.
Hilo si la msingi sana ingawa tunaweza kujifunza pia. Ila suala la mashabiki kujitokeza kwa wingi na wengi wakiwa ni wageni wa Uwanja wa Taifa, hilo ndilo linaweza kuwa moja ya mafunzo makubwa.

Nimekuwa kati ya wadau wanaojitokeza Uwanja wa Taifa mara kwa mara kwenda kuangalia mechi mbalimbali. Siku hiyo niliona sura nyingi mpya ambazo ninaweza kushindwa kufafanua vizuri lakini nitajitahidi.
Idadi kubwa ya mashabiki hao iliyojitokeza ilikuwa ni ya raia wa kigeni kutoka katika nchi za Ulaya ambao mara chache wamekuwa wakijitokeza kuangalia mechi za ligi za hapa nyumbani hasa Ligi Kuu Bara.

Wengine walikuwa ni Watanzania wenye asili ya Bara la Asia ambao pia walijitokeza kwa wingi sana pale uwanjani na kufanya muonekano wa baadhi ya majukwaa uwe tofauti na siku nyingine zilizopita.
Pamoja na hivyo, wengi waliofika uwanjani hapo, walifika wakiwa na familia zao kama wake na watoto zao na wakaishuhudia mechi hiyo kwa furaha kubwa mwanzo hadi mwisho.
Hapa ndiyo tunaweza kujifunza haraka na huenda Yanga, Simba, Azam FC na wengine wanaweza kuwa na kazi ya kuanza kufanya ubunifu kuhakikisha wanawapata watu hao katika mechi za ligi na zile za kimataifa.

Usiseme haiwezekani kwa kuwa wale walikwenda kumuona Figo, bado Simba, Yanga na Azam FC zinapaswa kufikiria mambo kibiashara zaidi na sasa ziamini kuwa kuna mashabiki hupenda kwenda uwanjani lakini wanashindwa na vikwazo ni vipi?
Hakuna ubishi klabu za Tanzania zinahitaji mapato zaidi kujiendeleza, lakini zimekuwa hazifanikiwi kupata watu hadi zinapocheza Yanga na Simba tu na zenyewe si kila mechi. Mapato ni sehemu ya mhimili wa kujiendeleza kwa maana ya malipo mazuri kwa wachezaji, makocha na pia maendeleo kwa ujumla.
Hivyo ni lazima kubuni kupata mashabiki wengi na mambo muhimu ni soka bora na la kuvutia kupitia vikosi vyao na lazima liwe na nidhamu ya juu.
Pili kuangalia suala la bei, kwamba Watanzania watakuwa wanaweza kujitokeza lakini kuwe na utaratibu wa kuamini hiyo ni biashara, basi zijitangaze na kuelezea ujio wa mechi fulani au jambo linalokuja.
Lakini kwa mashabiki wa Yanga au Simba, au wengine ambao wamekuwa wakija uwanjani kwa wingi wanapaswa kujua kuwa wao pia ni tatizo kwa kuwa wako wanaoamini kutukana matusi ndiyo ujanja.
Si lazima kila mmoja kutoa lugha chafu ili kujionyesha ni ‘mwenyeji’ wa Uwanja wa Taifa au unazijua sana Yanga na Simba. Hali hii imekuwa ikiwakwanza wengi na kushindwa kupeleka watoto wao uwanjani.
Taifa kumekuwa na vurugu hata zisizokuwa na sababu za msingi, ili mradi kuna watu wengi wapenda sifa hupenda kuonekana hasa wanapoona kundi kubwa la watu. Kupigana au kuvuana nguo, jambo ambalo si rahisi kusikia linatokea kwingine kwa kuwa ni la kijinga!
Hivyo ni lazima kuwe na mabadiliko, watu wanakwenda kuangalia soka na si kusikiliza matusi ya wapenda sifa. Wako watu wengi wanapenda kwenda uwanjani na viingilio vyao vingekuwa faida kwa klabu zetu lakini mambo niliyoyataja ni sehemu ya vikwazo.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic