September 1, 2014



KILA mtu anaweza kuwa na hisia zake, mawazo yake na hata uamuzi wake wa mambo. Lakini mwisho, ukweli wa mambo ndiyo jawabu la mwisho.
Kuweka hisia zako hadharani ni jambo jema na vizuri kama ukasimamia unachokiamini kuliko kuwa mwoga kwamba kuna watu fulani wanaweza wasifurahie.
Ukweli ni kwamba mshambuliaji Mganda, Emmanuel Okwi ambaye amekuwa akigombewa kila baada ya miezi miwili, mitatu, anaonyesha kiasi gani hapa nyumbani hatuthamini wachezaji wa nyumbani.
Si vibaya kusema viongozi wa Simba, watani wao Yanga ni wale wasiotaka kutumia nguvu nyingi pia kuinua vipaji vya hapa nyumbani.
Inawezekana wako wanaoamini kuwa wanapita, hivyo hawana sababu kubwa ya kufanya juhudi kuinua vipaji, badala yake wanaweza wakawa wananunua tu na kulahisiha mambo.
Wakati mwingine ni aibu, wakati mwingine inakera na hasa suala la mzozo wa usajili ambalo linahusisha mchezaji mmoja tu tena si raia wa Tanzania.
Ukiuliza anatokea wapi, jibu ni Uganda. Tofauti yake na wachezaji wa Tanzania ni ipi, lazima majibu yatakuwa yanayumba. Labda basi tuulize, Okwi ameipeleka wapi Uganda, yaani The Cranes, hakuna tofauti na Tanzania!
Sasa ubora wa Okwi ni nini? Wakati mwingine utaona Yanga walifanya kila linalowezekana kumpata lakini zaidi ilikuwa ni siasa tu kwa kuwa walilenga kuwakomoa Simba.
Uliza Yanga, kwamba Okwi aliwasaidia nini. Hakuna kwa kuwa hakucheza hata mechi saba za ligi, pia akafunga bao moja tu. Yeye na Mrisho Ngassa au Hussein Javu, nani alikuwa na msaada utapata jibu.
Wakati Okwi hakuwa na msaada Yanga, vipi leo Simba wanamchukua kwa mbwembwe na wanaonekana kufurahia sana. Jibu ni lilelile kama la Yanga, kwamba wanataka kuwaudhi Yanga lakini ukweli hakuwa kwenye mipango yao na sasa ni patapotea kama kweli atakuwa kwenye kiwango chake au la.
Yote yanawezekana, huenda akacheza vizuri na kuwa msaada kwa Simba, lakini kuna haja ya kujiuliza atakuwa msaada kwa kipindi gani na ataisaidiaje Simba kufanya vizuri kwa kuwa amekuwa ana matatizo yasiyobadilika kama kuomba ruhusa, kwenda kwao, baadaye akachelewa kurejea.
Tunajua utovu wa nidhamu kama kupata kadi zisizokuwa na ulazima kama vile msimu mmoja kabla ya kuondoka kwenda Etoile du Sahel ya Tunisia ambayo hadi leo inadai ni mchezaji wake na inadaiwa na Simba.
Okwi, Okwi, Okwi. Hivi ni nani hasa? Uwezo wake ni kweli una tofauti kupindukia na wachezaji wa hapa nyumbani?
Vipi anawaendesha hivi viongozi wa klabu kongwe za Tanzania ambazo zina umaarufu na uwezo mkubwa hata kuliko za kwao Uganda. Au kwa kuwa viongozi hao wanataka sifa tu, wanataka kufurahisha mashabiki wao bila ya kujali uzalendo au kufanya mambo kwa kuangalia maisha marefu ya baadaye ya klabu zao?
Hawafanyi hivyo kwa kuwa wanajua baada ya muda wataondoka? Je, Okwi ataendelea ‘kunyanyasa’ anavyotaka hadi lini au kwa kuwa anajua hapa Tanzania ndiyo sehemu unaweza ‘kutesa’ unavyotaka!
Hii si sawa, kwa yoyote anayesoma makala haya, akiondoa ushabiki na kutafakari atagundua Tanzania kupitia viongozi wa Yanga na Simba wakiwa wamefungua macho wanaweza kubadili njia na kuepuka kupita kwenye barabara ya kuwagombea akina Okwi kwa kuwa si lazima.
Tupeni fedha zenu nyingi kwenye timu za vijana na kwa asilimia kubwa itawasaidia kuachana na mizozo na ‘vizogo’ vya akina Okwi ambao hawana tofauti hata kidogo na wachezaji wa hapa nyumbani ambao hamuwapi vipaumbele!

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic