October 24, 2014


KILA Ligi Kuu Bara inapoanza kupamba moto, mashabiki wengi sana wa soka huelekeza masikio na macho yao upande huo, pia inakuwa vigumu sana kuyabandua upande huo.


Siku zote Ligi Kuu Bara inakuwa na presha kubwa kwa kuwa kila timu inataka ushindi na waliopoteza wanataka kuendeleza mambo lakini kwa wale walioshinda wanataka kuendelea bila ya kufungwa.

Presha inakuwa kubwa zaidi kwa Yanga na Simba kwa kuwa zina mashabiki wengi wanaoziunga mkono, mashabiki walalamishi na wasiokuwa na subira. Hali hii inawafanya viongozi kuwa na presha kubwa.


Unapofikia wakati wa ligi hiyo, hakuna ubishi kwamba uongozi unaelekeza nguvu zake nyingi upande huo ukitaka kupata mafanikio na kuepukana na kelele hasi za mashabiki ambao wanataka kuona chanya kila kukicha.

Si vibaya kuwa na uongozi unaotupia nguvu zake katika moja ya mambo ya msingi na kuwafanya mashabiki kuona wako sahihi katika uteuzi wao wakati wa uchaguzi. Pia si vibaya uongozi kukumbuka mashindano lakini kutosahau umuhimu vitu vya maendeleo muhimu kwa klabu zao.

Si vibaya kuwasaidia makocha Marcio Maximo na Patrick Phiri, lakini vitu muhimu kama uwanja, ni sahihi na muhimu zadi kuhakikisha vinamilikiwa na klabu hizo kwa ajili ya maendeleo.

Utakumbuka klabu zote mbili za Yanga na Simba zilianzisha mchakato wa viwanja vyao. Kila upande unamiliki uwanja, Yanga ukiwa ni ule wa Kaunda ambao uko katikati ya jiji na Simba katika eneo la Boko, nje kidogo ya Dar es Salaam.

Maandalizi ya kuhakikisha unafanyika ukarabati au ujenzi tayari yalianza, lakini yamepotea ghafla na hakuna anayezungumzia wala kulifanyia tena kazi jambo hilo ambalo ni muhimu sana kwa klabu hizo.

Simba na Yanga zinahitaji sana viwanja kwa kuwa ndiyo pango la kazi zao. Kuuza bidhaa bila kuwa na sehemu ya kufanyia biashara haiwezi kuwa sahihi na klabu hizo kongwe hazipaswi kwenda na mfumo wa biashara za ‘kutembeza’.

Wenyeviti wanaoziongoza Yanga na Simba ni vijana au kaka zetu wa enzi hizi. Yusuf Manji na Evans Aveva. Wote wametembea, wafahamu wa mambo na hauwezi kusema kutakuwa na ugumu kwa wao kuleta mabadiliko.

Kama Aveva na Manji itafikia siku wameondoka Simba na Yanga, halafu wakaziacha klabu hizo kutokuwa hata na uwanja wa mazoezi unaotambulika kwa ajili ya timu zao. Hakika litakuwa ni jambo la kushangaza na linapaswa kuzungumzwa au kukemewa kwa miaka mingi.

Manji na Aveva lazima watupie nguvu zao kwenye kuhakikisha hata kabla ya kuisha kwa msimu huu, basi Yanga na Simba zinakuwa na viwanja vyao, angalau vya mazoezi tu.

Kuwa na viwanja ni kujikomboa, timu zote hizo mbili zinauhitaji uwanja. Lakini timu zao za vijana pia zinahitaji viwanja. Si kazi rahisi kukuza vijana bila ya kuwa na uwanja kwa ajili ya mazoezi.

Kama ni aibu ya kukosa uwanja imekuwa ni ya muda mrefu sana. Kwa Simba ya Aveva na Yanga ya Manji, kuna kila sababu ya klabu hizo kupata uwanja. Tayari zilianza mikakati na hakuna sababu ya kuisimamisha na kubaki nguvu kwenye ligi.

Hata kuwa na kikosi bora, kupata uwanja ni sehemu ya mikakati bora ya kuwa na kikosi imara kwenye ligi. Manji na Aveva msiliweke kando suala la viwanja kwa kuwa umuhimu wake ni sawa na uti wa mgongo wa klabu zenu.

Kitu kizuri zaidi ni suala linalowezekana na klabu hizo zinazoongozwa na wenyeviti vijana zaidi ukilinganisha na wakati mwingine uliopita, zina kila sababu ya kuwa Yanga na Simba mfano ukilinganisha na zile zilizopita lakini changamoto kwa Yanga na Simba zinazokuja.



1 COMMENTS:

  1. unajua nyinyi waandishi mnaboa sana, hivi kwenye uchaguzi wa Simba Aveva kama mgombea sela yake si mliipigia debe? Point tatu goli tatu, sasa huo uwanja unaouzungumzia ni upi alio ahidi Aveva? hapa kweli naamini njaa zinawasumbua waandishi wengi hapa Tanzania, hebu toa na lihabari lako linaboa

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic