October 24, 2014




Na Saleh Ally
UKITAJA moja ya makocha bora kwenye ukanda wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini, kamwe hauwezi kumuacha Patrick Phiri, raia wa Zambia.


Ana rekodi nzuri kwa upande wa klabu lakini timu ya taifa pia, amewahi kuivusha Zambia kwenye Kombe la Mataifa Afrika ingawa hakufika mbali.

Kila timu anayoifundisha hucheza soka la kuvutia na tayari hali hiyo imeanza kujionyesha kwa Simba ingawa muda unatakiwa ili aweze kufanya mabadiliko anayoyataka.

Wakati ameanza mabadiliko, kuna jambo amekuwa akilifanya ambalo inawezekana ni hisia za kibinadamu, kuamini au ushawishi lakini msingi wa hakuna binadamu aliyekamilika unaweza kuwa mwongozo kwamba hata yeye anakosea pia.

Phiri ameonekana kutomuamini kabisa mshambuliaji Amissi Tambwe raia wa Burundi na kuamua kumuweka benchi. Mwenyewe amekuwa akisema atampa nafasi lakini anajaribu kutengeneza mfumo tofauti.

Watu wa karibu na Phiri wamekuwa wakisema Tambwe hawezi kuendana na kasi ya Phiri katika kikosi chake, ndiyo maana sasa ameamua kumuweka benchi na kutumia vijana wengine kama Elius Maguli.

Inawezekana kabisa kuwa Phiri hamjui Tambwe na huenda amekuwa na haraka katika suala la kuamua kuhusiana naye kwani Tambwe ana vigezo vyote vya kupata nafasi ya kwanza kwenye timu yoyote ya Tanzania Bara.


Tambwe ndiye mfungaji bora msimu uliopita akiwa amepachika mabao 19 katika mechi 24 za ligi alizocheza, hali inayoonyesha ni mshambuliaji hatari anapokuwa mbele ya lango la wapinzani.

Kusema hawezi kuendana na mfumo, bado linakuwa ni jambo linalokosa uthibitisho kwa kuwa katika mechi tatu za kirafiki alizoichezea Simba ikiwa kambini Zanzibar, Tambwe alifunga bao moja.

Aliporejea kwenye ligi, mechi tatu za mwanzo ambazo zote Simba ilitoka sare, Tambwe alifunga bao moja akipiga kichwa krosi nzuri ya Okwi. Wastani wa bao moja kwa mechi tatu, bado si mbaya.

Sasa hapo ndiyo unaweza kujiuliza ni mfumo upi ambao unamshinda Tambwe kama amecheza mechi sita za ligi na kirafiki na kufunga mabao mawili? Nani anauweza huo mfumo na amefunga mabao mengi zaidi yake?

Kama ni kweli Phiri ameona Tambwe hauwezi mfumo wake basi hakutulia na kumfuatilia vizuri kwa kuwa Simba haichezi kasi ya kutisha kiasi kwamba Tambwe hataweza kucheza.

Angalia msimu uliopita, Tambwe alikuwa katika kikosi cha Simba kilichochoka, wachezaji walikuwa wakidai mishahara na fedha zao za usajili, hali za kambi zao hazikuwa nzuri na hakukuwa na watupia krosi safi kama Okwi, halafu akafunga mabao 19.

Jiulize sasa ana watu kama Haruna Chanongo na Ramadhani Singano ‘Messi’ aliokuwa nao msimu uliopita, ameongezewa Okwi na pia Paul Kiongera ingawa sasa ni majeruhi. Kwa wachezaji hao wenye kasi na furuku, unafikiri Tambwe atashindwa kufunga zaidi?

Ukisema Tambwe ni mviziaji, kazi yake ni kufunga tu, eti hawezi kwenda na mabeki wawili akaingia na kufunga, hilo ni tatizo la kutokuwa mchunguzi. Picha lukuki zinaonyesha akikabwa na mabeki wawili au akikimbia nao ndani ya 18 kabla ya kufunga.

Suala la Tambwe lisiamuliwe kishabiki, inawezejana ni matakwa ya kocha au baadhi ya viongozi wanaona Mrundi huyo si mzuri au hawafurahishi kwa aina yake ya uchezaji kwa kuwa haina chenga na mbio nyingi. Wanachopaswa kujua kazi ya Tambwe ni kufunga na wampe nafasi aifanye kazi yake.

Maguli ni mchezaji mzuri, anaweza kuja kuwa bora zaidi ya alivyo sasa. Lakini kuwa naye, isiwe sababu ya kumuona Tambwe hafai kabisa au hana lolote. Wote tunajua Mrundi huyo ana kipaji cha upachikaji mabao, analijua vema lango kuliko Watanzania lukuki.

Bado Tambwe hastahili kukaa benchi kutokana na takwimu za msimu uliopita na hata baada ya Phiri kutua Simba. Usisahau ni mwenye juhudi, anajitolea kwa ajili ya Simba na nidhamu yake iko juu.

Maana yake, kama mchezaji amekamilika. Phiri anapaswa kumpa nafasi zaidi na huenda anaweza kubadili uamuzi na kuona alichokifanya kilikuwa na haraka au walioamini hivyo pia waliharakisha mambo.

Kweli Tambwe hana kasi kama ya Chanongo, Messi, Msuva au Ngassa. Lakini ukweli linapofikia suala la kumalizia mpira ukaguse nyavu, Mrundi huyo anajua zaidi ya wote hao. Hivyo Phiri ampe nafasi tena ili akishindwa, basi kusiwe na mwanya wa kuamini alifanya haraka.



 



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic