Mshambuliaji
nyota wa Simba, hiyo, Amissi Tambwe, ameamua kufunguka na kuweka wazi sababu
zitakazomuondoa klabuni hapo.
Tambwe amesema
yupo tayari kuondoka Simba licha ya kuwa bado anaipenda klabu hiyo lakini
sababu kubwa ni maneno anayosingiziwa na manyanyaso anayopata klabuni hapo.
“Kabla ligi haijaanza,
nilipatwa na hofu baada ya kuambiwa kuwa uongozi unataka kuachana na mimi ili
nafasi yangu ichukuliwe na (Emmanuel) Okwi, hali hiyo ilinifanya nipoteze mudi
ya mazoezi kutokana na kutumia muda mwingi kufikiria hali hiyo.
“Baada ya siku
chache, viongozi hao waliibua jambo jingine tena, hilo lilikuwa ni lile la
kuniondoa katika orodha ya wachezaji watakaosafiri kwa ndege kwenda Mtwara
katika mechi dhidi ya Ndanda FC, si unakumbuka?
“Nilisafiri kwa
basi kwenda na kurudi huku wenzangu wakipanda ndege, hakika niliumia sana.
“Lakini kitendo
cha hivi karibuni cha kunisingizia kuwa ninaihujumu timu pia kinanifanya niwe
na wakati mgumu na kujikuta nikitumia muda mwingi kufikiria mambo hayo, ndiyo
maana kiwango changu kimeshuka ukilinganisha na msimu uliopita ambao nilikuwa
na amani,” alisema Tambwe ambaye ni mfungaji bora wa Ligi Kuu Bara msimu
uliopita.
Kuhusiana na
mpango wa kujiunga na Yanga, Tambwe alisema: “Habari hizo za kujiunga na Yanga
hazina ukweli wowote na zinalenga kutaka kunichonganisha na viongozi wangu,
mimi ni mali ya Simba.
“Ndiyo, Yanga
waliwahi kunihitaji lakini hiyo ni zamani, siyo sasa, walinifuata msimu
uliopita nikawaambia wafuate taratibu zinazotakiwa kwa kuwa nilikuwa bado nina
mkataba mrefu na Simba. Kama bado wana nia na mimi wafuate tu mchakato
unaotakiwa.”
Akizungumzia
juu ya Tambwe kuondoka klabuni hapo, Ofisa Habari wa Simba, Humphrey Nyasio,
mapema wiki hii alinukuliwa akisema:
“Tambwe bado ni
mchezaji wetu na ataendelea kuwa klabuni hapa kwa kipindi chote cha mkataba
wake na bado tunamhitaji.”
0 COMMENTS:
Post a Comment