December 19, 2014


NAAMINI utakuwa unakumbuka nilipoandika makala iliyokuwa inahusiana na suala la nani anapata nini kuhusiana na mapato ya mechi ya kirafiki ya Nani Mtani Jembe.


Mechi hiyo inayowakutanisha watani, Yanga na Simba inajulikana kwa kuingiza fedha nyingi na pale ukubwa wa mechi si jina Nani Mtani Jembe, badala yake timu hizo mbili.

Nikahoji timu hizo zinafaidika na nini hasa baada ya mechi hiyo huku nikipiga hesabu ya fedha zinazotolewa na wadhamini Kampuni ya Bia ya Kilimanjaro ambazo mimi niliamini ni kidogo na si sahihi.

Wadhamini hawawezi kuchukua mapato ya mlangoni, wadhamini wanaopoingia kwenye klabu kwa ajili ya kuidhamini, lengo lao linakuwa ni kujitangaza.

Hakuna ubishi, Kilimanjaro kama ni kujitangaza, ukianzia mbele ya watu zaidi ya 65,000 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar, kweli walijitangaza na wamefaidika.

Sasa nikawa ninahoji, vipi tena wachote na mapato ya mlangoni, kwani Kilimanjaro ambayo iko chini ya Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) inafanya kazi ya kuuza bia au kuandaa mechi?

Hili ni swali ambalo sijajibiwa hadi sasa pia nisisitize, hata kama katika fedha hizo TBL itakuwa imechukua Sh milioni moja, bado ninahoji kwamba ni sahihi mdhamini kuingia kuchukua mapato?

Leo nina hoja tofauti kabisa, nayo ni kuhusiana na suala la mapato yaliyopatikana katika mechi hiyo iliyojaza watu pomoni.

Kuna watu kadhaa walinipigia simu na kunifafanulia kuhusiana na mgawo. Najua wana nia njema na ninawaamini lakini sijadhibitisha hadi hapo itakapotolewa ‘official’ kuhusiana na mapato na mgawo wenyewe.

Kama Yanga na Simba zikicheza kwenye Ligi Kuu Bara, kupitia Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) inatangaza suala la mapato na mgawo ulivyokuwa mara baada ya mchezo.

Sasa kama huo ndiyo utaratibu sahihi, vipi mechi hiyo ambayo inaandaliwa na wadhamini mapato hayatangazwi. Tunajua Simba na Yanga ni klabu za wananchi, vizuri wajue kilichopatikana ni kiasi gani.

Sitaki kujua walioingia uwanjani ni wangapi wanakunywa kinywaji cha Kilimanjaro, lakini najua wengi walioingia ni waliotoa kiingilio. Je, kiasi gani kimepatikana, Simba na Yanga kila upande wameingiza kiasi gani?

Vizuri pia jamii ingejua kama wadhamini hao kuna kiasi wanachochukua, basi wamechukua kiasi gani na kwa sababu zipi? Pia kama hawajachukua, vizuri tukaelezwa halafu tuendelee kuhoji kama ni hivyo, fedha hizo zimekwenda wapi na kwa nini?

Huu ndiyo wakati wa uwazi zaidi, ukimya au uficho wa mambo unaashiria kuna tatizo au kuna mambo ya konakona. Kama hakuna tatizo, lazima kunakuwa hakuna sababu ya kuficha mambo.

Nitaendelea kuhoji, kama wadhamini watakuwa wanachukua fedha. Je, wanazipeleka kwenye biashara yao au wanazirudisha kwenye mpira? Haya ndiyo mambo ambayo ninataka yafanyiwe ufafanuzi.

Leo ninauliza maswali mengi kwa kuwa tu hakukuwa na taarifa ya kiasi kilichopatikana kwenye mechi hiyo ya watani lakini mgawo pia ulikwenda kwa nani na yupi na kwa nini pia.

Lazima fedha za mpira zirudi kwenye mpira na kusaidia. Hata kama serikali itakuwa imechukua nyingi kupitia kodi, bado nako nitahoji kwa kuwa ninaamini lazima zisaidie mpira.

Yeyote anaweza kutofautiana nami, lakini fedha za viingilio uwanjani zinatolewa na wapenda mpira, hivyo wana haki ya kuona zinaleta maendeleo kwenye sekta wanayoifurahia.

Je, wadhamini wakichukua ni sahihi, huu ni utaratibu wa hapa Tanzania pekee au duniani kote?


Hakika hamjachelewa, hata keshokutwa inawezekana. Ndiyo maana nasisitiza ili kuepusha maswali mengi ninayouliza, tuelezwe mapato yalikuwa kiasi gani? Nani na yupi alichukua, kwa nini? Nitarudi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic