January 23, 2015


Na Saleh Ally
MSHAMBULIAJI nyota wa TP Mazembe, Mbwana Samatta ameanza majaribio na Klabu ya CSKA Moscow ya Urusi akiwania kupata nafasi ya kuitumikia.


CSKA Moscow ni moja ya klabu kubwa kabisa barani Ulaya na duniani kote, si vibaya kusema ni klabu ya kiwango cha akina Chelsea, Manchester United, Arsenal na wengine.

Siku chache kabla Samatta kwenda Urusi kwa ajili ya majaribio na baadaye kusafiri na timu hiyo hadi Hispania kwa ajili ya kambi, meneja wake, Jamal Kisongo aliliambia Championi kwamba juhudi kubwa zilifanyika kumshawishi mmiliki wa TP Mazembe, Moise Katumbi akubali.

Bilionea Katumbi alitaka Samatta aendelee kubaki TP Mazembe kwa kuwa ndiye mchezaji tegemeo na kipenzi chake. Hakuona kama kuna sababu ya kumuachia huku akiwa tayari kumuongezea dau zaidi ya dola 10,000 ambayo hulipwa sasa.

Kumuondoa Samatta ndani ya Mazembe ndiyo ushindi namba moja na huenda hapo ndiyo pongezi ndiyo zilikuwa zinahitajika. Si sasa.

Sitaki kuingilia uhuru wa wale wanaompongeza Samatta sasa, lakini huu ni wakati mwafaka wa kumpa moyo na ikiwezekana kumuombea dua afanikiwe kwa kuwa hatuna sababu ya kuuliza juhudi kwa Samatta hadi alipofikia.

Tunampongeza kwa kupata majaribio? Naona ni sawa na kumpongeza wakati akiwa vitani kwamba hongera kwa kupigana. Tuwe naye, tumpe moyo, tumueleze Watanzania wanavyomtegemea na akishinda tumpongeze. Akishindwa tumuambie kateleza, ainuke asonge na tumuunge mkono hadi atakaposhinda na hapo ndiyo wakati wa pongezi.

Unakumbuka alikuja baada ya Mussa Hassan Mgosi, Mrisho Ngassa, Shabani Nditi na wengine wengi unaowajua. Juhudi na maarifa, uthubutu wa kukubali kwamba kufanya vema nje ya Tanzania inawezekana.

Uthubutu pia wa kukubali kubadilisha kwamba Simba na Yanga si mwisho wa mafanikio yote. Samatta anajiamini na mfano mzuri wa utofauti wake na wachezaji wengine ulianza kuonekana pale alipogoma kucheza Simba.

Aligoma kwa kuwa waliahidi kumpa gari, lakini hawakufanya hivyo na badala yake wakaanza kuuza maneno. Akakaa nyumbani hadi walipompa walichoahidi. Kama unakumbuka, siku chache TP Mazembe wakamchukua.

Wachezaji wangapi wa Tanzania wamekwenda nje ya nchi yetu wakafanya madudu. Wako waliolipwa vizuri, walipewa nyumba za kuishi halafu siku chache wakarudi nyumbani kisa wamekumbuka kuja kuungana na wenzao kucheza mechi za mchangani au kuvuta pamoja sigara kubwa?

Wangapi unawajua hawaamini kucheza nchi za jirani kama Kenya, Uganda, DR Congo, Rwanda na kwingine ni njia ya kusonga kulikoendelea zaidi kisoka kama Uganda?

Unawajua wangapi ambao wanaona kucheza Yanga au Simba ndiyo mwisho kabisa wa ndoto zao na wala hawahitaji tena kwenda kwingine?

Samatta ni ‘figa’ ya mabadiliko ya Tanzania, hivyo tumuombee na huenda akasaidia kujenga kizazi kipya kinachojiamini, kilicholenga kwenda mbele zaidi ya Yanga na Simba.

Ndani ya CSKA Moscow kuna nyota kadhaa kutoka Afrika lakini hawa wawili, Ahmed Musa kutoka Nigeria na Seydou Doumbia wa Ivory Coast ndiyo wanaofanya vizuri zaidi.

Kwa msimu huu kila mmoja ana mabao saba. Ninaamini kama Samatta atapata nafasi, basi hata wao watakuwa na hofu kubwa kwa kuwa uwezo wake uko juu zaidi.

Kama atashindwa, timu nyingine tatu zinamsubiri ili zimpe nafasi ya kufanya majaribio, moja wapo St Etienne ya Ufaransa ambayo si klabu ndogo.

Ndiyo maana nikasema, huu si wakati wa pongezi kwa Samatta. Badala yake dua na kuwa naye pamoja, wakati wa ushindi, pongezi zitafuatia na akifanikiwa basi safari moja au hatua muhimu itakuwa imepigwa katika maendeleo ya soka nchini.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic