April 1, 2015


Na Saleh Ally
RAIS wa Baraza la Vyama vya Soka Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati (Cecafa), Leodegar Tenga na Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, wameweka msimamo wao wazi kuhusiana na uchaguzi wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).


Kwa pamoja, Tenga na Malinzi wamesema Tanzania yenyewe iko wazi mapema na hakuna sababu ya kupoteza muda kwamba katika uchaguzi ufuatao, itampigia kura Josep Blatter.

Blatter ndiye rais wa Fifa sasa, amekaa madarakani tangu mwaka 1998, maana yake ana miaka 17 akiliongoza shirikisho hilo kubwa, maarufu na tajiri kwelikweli.

Uamuzi wa Tenga na Malinzi kutangaza hadharani umekuja huku viongozi hao wakisisitiza ni kutokana na namna ambavyo Blatter amekuwa akisimamia maslahi ya Bara la Afrika katika mchezo wa soka.

Alichokisema Malinzi, hakina tofauti kabisa na Tenga. Maana yake wawili hawa wanaungana pamoja katika njia moja, kuzungumza vitu vinavyofanana na wanavyoviamini.

Sina tatizo na uamuzi wa Tenga na Malinzi kuhusiana na Blatter. Lakini nashangazwa kwa kuwa naona kama uamuzi huo umekuwa ni wa haraka sana na unaonekana kama una ushabiki au maslahi binafsi.

Tenga ni kati ya walio katika kamati za Fifa. Inawezekana mapenzi yake au ameamua kumtetea bosi wake na yeye ameamua kushuka hadi kwa Malinzi na kumshawishi kuhusiana na Blatter, naye amekubali.

Au inawezekana Malinzi naye ameamua kufanya hivyo kutokana na misaada ya chinichini, waziwazi au vinginevyo ambayo anaipata kwa Blatter akiwa na shirikisho?

Napata maswali mengi sana kwa kuwa Malinzi na Tenga hawakuweka wazi kipi hasa ambacho Blatter ameisaidia Tanzania na si Afrika.

Sidhani kama Watanzania wanataka kusikia zaidi kuhusu Afrika badala ya Tanzania ambayo ni nchi yao na wanajua Fifa ina uwezo mkubwa sana wa kifedha.

Malinzi na Tenga wanaamini kiasi cha fedha kinacholetwa na Fifa kama msaada kinatosha kweli? Hawaoni kama Fifa inastahili kuisaidia Tanzania zaidi?

Lakini wakati wanakubali kumpigia kura Blatter, wamewahi kumsikiliza Luis Figo ambaye ni mgombea mwenza wa Blatter kwamba yeye ataisaidiaje Tanzania au Afrika?

Sasa vipi wamewahi kukubali kumtetea au kumpigia kura Blatter wakati hawajajua lolote kuhusu Figo. Kama walijua mbona hawajawaambia Watanzania kwamba Figo hatakuwa na msaada mkubwa?

Kweli Tenga na Malinzi wote wanaweza kuwa na haki ya kuchagua wampigie nani. Lakini kwa Malinzi anapaswa kujua yeye ni mwakilishi wa Watanzania ambao wamemchagua.

Nafasi aliyonayo ni uwakilishi wake kwa Watanzania kwenda Fifa. Hivyo kabla ya kuchukua uamuzi fulani au jambo fulani, basi wana kila sababu ya kuwafafanulia kwa undani Watanzania wajue.

Bado sijawa na uhakika uamuzi waliouchukua ni sahihi au la kwa kuwa sijasikia sababu zao ni msingi au la. Hii inatokana na kutokuwa na maelezo ya kutosha kutokana na umuhimu ninaouzungumzia.

Lazima Malinzi akubali, TFF ni ya umma. Hivyo kuwafafanulia Watanzania kuhusiana na uamuzi unaowahusu ni jambo jema ili kuondoa hisia za huenda kuna wachache wanaofaidika kwa kuwa inajulikana, licha wa ukubwa wa Fifa, wakati mwingine imekuwa ikichafuka sana hasa katika kipindi cha masuala ya uchaguzi.



1 COMMENTS:

  1. Kila mtu anajua kuwa Blatter ni mtu wa rushwa!! Amekuwa raisi wa FIFA kiipindi chote cha Tenga na kuna pesa nyingi za miradi zilikuwa zinakuja zinaliwa na wajanja na mwisho wa siku wanakuja watu toka fifa kuwasafisha. Hata kipindi cha Malinzi anajua pesa nyingi za miradi na mapato wanazitumia sivyo ndivyo na hakuna mtu wa kuhoji zaidi ya Fifa. Zimwi likujualo...., wanjua wanamhitaji Blatter ili waendelee kula good time, na haya ni maelekezo ya Issa Hayatou!! Hawana maelezo ya kukupa zaidi ya kwamba ni maelekezo na wanachotakiwa ni kutimiza. Vicha vya panzi, hakuna siku vitakuja kuvaa kilemba

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic