May 6, 2015


Majambazi Yameiba gari la kipa wa Yanga, Ally Mustapha ‘Barthez’, aina ya Toyota Carina SI lenye namba za usajili T 224 CXR.

Akizungumza na Championi Jumatano, Barthez alisema kuwa gari hilo liliibiwa usiku wa kuamkia Ijumaa iliyopita wakati yeye akiwa safarini akielekea Tunisia kwa ajili ya mchezo wa marudiano wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Etoile du Sahel uliomalizika kwa Yanga kufungwa bao 1-0.

Barthez alisema kuwa, gari hilo liliibiwa kwenye maegesho ya magari eneo la Majumba Sita, Ukonga jijini Dar es Salaam.

 Akisimulia mkasa huo kwa masikitiko makubwa, Barthez alisema aliliacha gari hilo mikononi mwa mdogo wake hadi linakumbana na mkasa huo.

“Ninaishi Kitunda nilipojenga nyumba ninayoishi na familia yangu, mara nyingi ninaposafiri ninamuachia mdogo wangu Aziz Mustapha anayeishi Majumba Sita kwa ajili ya kulilinda.

“Kwa sababu kule kwangu ninapoishi vibaka wapo wengi na mara nyingi wamekuwa wakiruka ukuta na kuiba baadhi ya vitu vilivyopo kwenye gari. Wakati narejea nchini nikiwa kwenye Uwanja wa Ndege, ndiyo nikampigia simu mdogo wangu na kunipa taarifa za kuibiwa gari hilo. “Hivyo nikatumia usafiri mwingine kwenda Majumba Sita walipo wazazi wangu ndiyo wakanipa taarifa hizo kuwa gari liliibiwa usiku wa kuamkia Ijumaa iliyopita.

“Nilipohoji vipi mlinzi alikuwa wapi, mdogo wangu akanijibu kuwa alipokwenda asubuhi alikuta gari na mlinzi wote hawapo na ndiyo akaenda kuripoti kituo cha polisi, wakati anafika hapo akakutana na watu wengine watatu waliofika kuripoti kuibiwa gari kwenye maegesho hayo ya gari.

“Polisi wanaendelea na upelelezi kwa ajili ya kuchunguza wizi huo wa magari manne yaliyoibiwa,” alisema Barthez.
 Mshambuliaji wa Yanga, Simon Msuva anayemiliki gari aina ya Altezza, naye alitoa masikitiko yake. “Kwa kweli nimesikitika sana, nimempa pole Barthez kutokana na tukio hilo baya. Mimi mwenyewe kila nikisafiri nimekuwa namuachia mzee gari anakuwa nalo maana pale nyumbani kuna watu wengi na ulinzi upo.

“Nachofanya ni kujaza mafuta ya kutosha na mzee anaendelea na misele yake. Siku nikirudi nalichukua,” alisema Msuva.

Kwa upande wa Nahodha wa Yanga, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, alisema: “Kweli inauma sana, kwa kweli wamefanya kitu kibaya sana.
“Mimi nimekuwa makini sana, mara nyingi nikisafiri naliacha nyumbani Kigamboni ambako kuna ndugu zangu na familia yangu.”


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic