September 4, 2015


Na Saleh Ally, aliyekuwa Istanbul
WAKATI wa Kombe la Dunia mwaka 1994, timu ya taifa ya Romania ndiyo ilikuwa gumzo zaidi licha ya kwamba Brazil ikiongozwa na Romario na Bebeto ndiyo ilifanikiwa kubeba ubingwa.


Pamoja na Bebeto na Romario ilikuwa vigumu kutowazungumzia wachezaji wawili, beki wa Marekani, Alex Lalas, jamaa aliyekuwa na mzuzu mrefu. Halafu Gheorghe Hagi aliyekuwa nahodha wa timu ya taifa ya Romania.

Hagi alifunga mabao matatu katika michuano hiyo, moja likiwa ni dhidi ya Argentina na jingine dhidi ya Colombia ambalo lilikuwa moja ya mabao bora ya michuano hiyo.

Alifunga umbali wa mita 40 baada ya kugeuka na kuachia mkwaju iliomshinda kipa Oscar Cordoba. Mwisho wa michuano hiyo licha ya kuishia robo fainali, Romania ikachaguliwa kuwa timu bora ya michuano.



Kwao Romania, Hagi anajulikana kama Regele, yaani mfalme. Jina ambalo anastahili, kwani licha ya kuingoza timu ya taifa kwa mechi 124 na kufanikiwa kufunga mabao 35, aliipa nchi hiyo heshima kubwa akichezea timu kubwa duniani kama Barcelona na Real Madrid.

Hagi alimalizia soka lake Galatasaray ya Uturuki, alianza kuichezea kuanzia 1996 hadi 2001 alipostaafu soka.
Baadaye akapata nafasi ya kuifundisha msimu mmoja na akaiwezesha kubeba ubingwa huku ikiwachapa wapinzani wake wakubwa Fenerbahce kwa mabao 5-1 hiyo ilikuwa mwaka 2004 hadi 2005.

Baadaye alitimuliwa, halafu akarejea na kuifundisha timu hiyo tena kuanzia mwaka 2010 hadi 2011, akatimuliwa tena kutokana na kutofanya vizuri.



Sasa Hagi ni shujaa wa Galatasaray na heshima yake imeendelea kubaki juu kwa kuwa akiwa mchezaji aliisaidia kubeba makombe ya ligi na michuano mingine.

Siku tano zilizopita nilikuwa katika makao makuu ya klabu ya Galatasaray jijini Istanbul ambako nilifanya ziara fupi ya kujifunza mambo.
Mengi nimeshangaa, mengi nimejifunza lakini kwanza nianze na lile la kuona jezi namba 10, tena katika mfumo wa jezi za sasa za Galatasaray ikiuzwa kwa bei juu kabisa.

Fedha ya Uturuki inajulikana kwa jina la Lira, hivyo jezi moja yenye jina namba ya Hagi ni Lira 241. Ukibadilisha dola 100, unapata Lira 261 hadi 280.

Utaona jezi hiyo ina thamani kubwa, takribani dola 10 ya Marekani. Bei hiyo ni sawa na zile za nyota wengine wa sasa wa Galatasaray kama Wesley Snejdeir na Karel Podolski! kwangu kilikuwa kitu kigeni, nikajifunza kwa kuuliza.



Aliyeniongoza katika ziara hiyo ya mafunzo, kanieleza inatokana na heshima kubwa ya Hagi akiwa kocha na mchezaji. Wanaitambua na kuithamini hadi leo.

Tena akanieleza, jezi hiyo imekuwa ikiingiza fedha nyingi kimauza na Hagi naye amekuwa akifaidika!.
Haraka nikakumbuka wachezaji wa zamani wa Yanga na Simba kama Makumbi Juma au enzi zile za kina Abdallah Kibadeni.

Nikaona labda ni mbali sana, vipi sasa akina Edibily Lunyamila au hivi karibuni watu kama Juma Kaseja na Selemani Matola. Hawa si walizipa Yanga na Simba makombe? Hawa si walizipa timu zao heshima?

Mbona Yanga na Simba hawataki kufanya biashara wala hawataki kuwa wabunifu. Au viongozi wana hofu leo wakiuza jezi za kina Lunyamila na Kaseja watafunikwa umaarufu wao?

Yanga na Simba si wabunifu wa biashara kwa kuwa hawafikirii mbali? Hawana watu enye uwezo mkubwa wa kufikiria au zaidi wanawaza leo tu, hakuna anayejua klabu hizo zitafika kesho?

Maswali ni mengi, wanaoweza kuyajibu ni Yanga na Simba wenyewe ingawa najua longolongo na sababu lundo zisizo na msingi zitatawala lakini habari ndiyo hiyo. Hadi leo Galatasaray wanauza jezi ya Hagi. Yule shujaa wa Romania mwaka 1994 na shujaa wao hadi mwka 2001. Jifunzeni na mkubali na muacha kupokea mambo yakapita sikio moja na kutokea jingine halafu mkaendelea kubaki vilevile!


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic