April 2, 2016


Azam FC imebakisha siku nane tu kucheza na Esperance ya Tunisia mechi ya Kombe la Shirikisho Afrika, kocha wa timu hiyo, Stewart Hall amekuwa mkweli kwa kusema wana kibarua kizito katika mechi hiyo. 

Hall, ambaye timu yake ilifuzu 16 Bora kwa jumla ya mabao 7-3 dhidi ya Bidvest ya Afrika Kusini, aliliambia Championi Jumamosi kuwa: “Ninazo video kumi za mechi za hivi karibuni za Esperance na kwa kushirikiana na wenzangu tunachambua kila kitu, kuanzia ubora, udhaifu, kona na upigaji wa faulo.

“Kila kitu tunacho kwenye mashine yetu, upigaji wa faulo, kuona safu ipi ni bora, wapi kuna udhaifu kwao ili iwe faida kwetu, lakini niseme tuna kazi kubwa sana. 

“Hawa jamaa (Esperance) katika safu ya kiungo, wale wa pembeni wote ni hatari sana na mbele pia wako vizuri,” alisema Hall na kuongeza: “Katika hali hiyo usitegemee mechi rahisi.”

Hata hivyo, Hall raia wa Uingereza alisema anajua wapinzani wao watakuja na lengo la kutoa sare ili wakamalize kazi katika mechi ya marudiano nchini Tunisia. 

“Pamoja na ugumu uliopo, tutajitahidi kupata matokeo mazuri ili tusipate kazi kubwa katika marudiano kwani najua Esperance watakuja na lengo la kutoka sare,” alisema Hall.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic