April 7, 2016



Nyota wa zamani wa Arsenal na Nigeria, Super Eagles Nwankwo Kanu ameshiriki katika uzinduzi wa duka jipya la kampuni ya StarTimes Tanzania lililopo katika jengo la Mkuki Mall Barabara ya jijini Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo mchezaji Nwankwo Kanu ambaye pia ni balozi wa makampuni ya StarTimes barani Afrika ambapo inafanya shughuli zake katika nchi zaidi ya 10 amesema kuwa anajisikia mwenye furaha kuwepo nchini na atashiriki shughuli mbalimbali za kampuni pamoja na za kijamii.

“Ni mara ya kwanza mimi kuwepo nchini Tanzania, nashukuru nimefika salama na kupokelewa kwa ukarimu mkubwa, kwa kweli sikutarajia. Uwepo wangu hapa ninaiwakalisha kampuni ya StarTimes barani Afrika kama balozi wao na kama balozi ninao wajibu wa kufika kila nchi ambayo kampuni hii ipo. 


"Kwa namna nilivyopokelewa ninaamini kuwa kweli StarTimes ni kampuni kubwa, inapendwa na kujulikana miongoni mwa watanzania wote.” Alielezea Bw. Kanu

“StarTimes wamejitahidi kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kuwa wateja wake wote wanafurahia huduma za matangazo ya dijitali kwa ubora wa hali ya juu na gharama nafuu. Na hii ni kutokana na falsafa iliyojiwekea kampuni ya kutaka kuhakikisha kuwa kila nyumba ya muafrika inafikiwa na matangazo hayo. 

"Changamoto ni nyingi katika uendeshaji na utoaji huduma za kidijitali lakini kampuni imejizatiti kuwekeza kwa kiasi kikubwa katika uboreshaji wa vipindi na chaneli zake. Kwa mfano kwa sasa kama mnavyoweza kushuhudia kuwa ligi kubwa barani Ulaya za Bundesliga na Serie A za nchini Ujerumani na Italia zinaonyeshwa moja kwa moja kupitia StarTimes Pekee.” Aliongezea Kanu


“Michezo na burudani ni maudhui muhimu sana ambayo lazima yawekewe mkazo kwani ndivyo vitu vinavyopendwa na kuwavutia wateja wengi hivyo haina budi kuweka mkazo. Ninaamini kuwa uwepo wangu nchini Tanzania utasaidia kwa kukaa chini na uongozi wa kampuni nchini na kuweza kuona wanawaongezea na kuwapatia nini wateja wao. 

"Ninatumaini ninacho cha kuongezea kwa nilichojifunza kutoka nchi kama za Uganda na Kenya ambazo nimetokea huko pia,” alisema na kumalizia Kanu kuwa, “Nashukuru kuwepo Tanzania na ninaamini nitajifunza na kushirikiana kwa mengi kwa kipindi nitakachokuwepo mpaka kuondoka kwangu.”


Naye kwa upande wake akizungumza wakati wa uzinduzi wa duka hilo jipya ambalo litakuwa ni la saba kwa mkoa wa Dar es Salaam pekee, Mkurugenzi wa Uendeshaji (Operesheni) wa StarTimes Tanzania, Carter amebainisha kuwa duka hilo jipya litawarahishia wateja wote wanao kama maeneo ya jirani kama vile Tandika, Mbagala, Temeke, Kurasini, Yombo, Kiwalani, Vingunguti na kwengineko kujipatia huduma na bidhaa kwa urahisi zaidi.


“Leo tunayo furaha kubwa kufungua duka hili jipya ambalo katika kumbukumbu litakuwa limezinduliwa na balozi wetu barani Afrika, Nwanko Kanu. 

Duka hili litakuwa msaada mkubwa kwa wateja walio maeneo ya jirani na kwingineko na ningependa kuwatoa wasiwasi kuwa litakuwa linatoa huduma zenye ubora sawa na maduka yetu yote hivyo wasiwe na wasiwasi. 

Ninawaomba wateja wetu watembelee hapa kujipatia huduma kama vile kununua visimbuzi, antena na kebo, vocha za malipo ya mwezi pamoja na huduma kwa wateja.”

Kanu alikuwa kati ya nyota walioanza kutamba na Nigeria katika michuano ya Olimpiki wakizifunga Nigeria na Brazil katika nusu fainali na fainali.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic