June 13, 2016



Mabingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Young Africans SC na timu nyingine zilizoshiriki katika msimu ulioisha wa 2015/2016 zitakabidhiwa zawadi zao mapema mwezi ujao na Kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania ambayo ni mdhamini mkuu wa ligi hiyo.

Meneja Uhusiano wa Vodacom Tanzania, Matina Nkurlu amesema kuwa ucheleweshaji wa kutoa zawadi hizo baada ya kumalizika, umetokana na baadhi ya timu zinazoshiriki kwenye mechi za mashindano ya kimataifa kama vile mashindano ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika na kuingia kwa mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.

“Tunaomba radhi kwa  timu husika, wachezaji na wadau wa soka kwa zoezi hili kuchelewa ila tunawahakikishia kuwa  zawadi ziko tayari na zitakabidhiwa  mwezi ujao,” alisema Nkurlu.

Pia alishukuru wadau wote waliofanikisha ligi hiyo hadi kufikia mwisho ambapo Young Africans ya jijini Dar es Salaam iliibuka tena bingwa kwa mwaka huu.

“Licha ya changamoto zinazoendeleza kujitokeza katika ligi yapo mafanikio makubwa na ligi hii inazidi kuwa na msisimko mkubwa nchini tunawashukuru wadau  wote na tuna imani kuwa itazidi kuwa bora katika siku za usoni,” alisisitiza Nkurlu.


Alisema kuwa Vodacom Tanzania itaendelea kutoa udhamini wa ligi hii hata katika msimu ujao kwa mujibu wa mkataba wake na TFF na aliwataka wadhamini wengine kujitokeza ili kuboresha zaidi ligi hii ikiwemo kuwawezesha wachezaji kunufaika zaidi katika ushiriki wake.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic