July 2, 2016



Baada ya Simba kumpa mkataba wa miaka miwili Kocha Joseph Omog raia wa Cameroon, nchi anayotoka gwiji wa zamani wa soka Afrika, Roger Milla, yeye amejigamba anataka kushinda ikiwa ni pamoja na kuwamaliza watani wao wa jadi, Yanga.

Omog kwamba msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara, Simba ilifungwa mechi zote mbili za ligi tena kila mechi ilifungwa mabao 2-0.

Omog aliposikia hivyo, akakuna kichwa na kusema: “Simba inipe muda lakini nakuambia Yanga inafungika.”

Simba jana Ijumaa ilimpa kazi Omog ya kukinoa kikosi chake ambacho msimu uliopita kilishika nafasi ya tatu kikiwa na pointi 62 katika mechi 30.

Hadi inampa kazi Omog, msimu uliopita Simba ilifundishwa na Muingereza, Dylan Kerr na baadaye Mganda, Jackson Mayanja.

Mcameroon huyo aliyewahi kuifundisha Azam FC kwa mafanikio msimu wa 2013/14 na kutwaa ubingwa wa ligi kuu bila kufungwa, ana rekodi ya kuifunga Yanga mabao 3-2 kwenye mzunguko wa kwanza na wa pili akatoka sare ya bao 1-1.

Omog aliyewasili nchini usiku wa kuamkia jana akitokea kwao Cameroon, alisema anajua Simba ina kiu ya taji la ligi kuu baada ya kulikosa kwa misimu minne iliyopita.

Omog alisema, siyo kazi rahisi kwake kuipa mfanikio hayo Simba bila ya kukiandaa kikosi chake vizuri ambacho kitaleta ushindani kwa kila timu watakayokutana nayo uwanjani.

“Mimi sera yangu ya soka ni kushinda kila mechi tutakayocheza iwe ya mashindano au kirafiki bila kujali ninakutana na timu ya aina gani na hayo yote yanawezekana kama nitafanya maandalizi mazuri ya kikosi changu.

“Hakuna kitakachoshindikana kwangu, nalifahamu vizuri soka la Tanzania, hivyo mashabiki wa Simba waondoe hofu nimekuja kuleta furaha ya mataji likiwemo la ligi kuu,” alisema Omog.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic