MNAOBEZA
uwezo wa mshambuliaji wa Yanga, Obrey Chirwa sikieni hii! Beki wa kimataifa wa
Zimbabwe anayeichezea Azam FC, Bruce Kangwa, ameweka wazi kuwa mshambuliaji
huyo ni hatari kutokana na kuwa na uwezo wa hali ya juu, tofauti na watu wanavyomchukulia.
Chirwa
aliyesajiliwa Yanga kwa dola laki moja (zaidi ya Sh milioni 200 za Kitanzania)
akitokea FC Platinum ya Zimbabwe, amekuwa kwenye wakati mgumu kutokana na
kuonyesha kiwango cha kawaida kwenye michezo mbalimbali ya timu hiyo na mpaka
sasa hajaifungia bao lolote licha ya kupewa nafasi mara kwa mara.
Akizungumza
na Championi Jumamosi, Kangwa anayecheza nafasi ya beki ya kushoto, amesema
anamjua Chirwa kuwa ni mshambuliaji mwenye uwezo mkubwa na kama akipewa muda
zaidi, anaweza kuibeba timu hiyo kwenye michezo ijayo.
“Namjua
Chirwa kwa sababu tumecheza wote kule Zimbabwe na ni mshambuliaji hatari, pia
ni msumbufu kwa mabeki tofauti na watu wanavyomchukulia.
“Siamini
kama ameshindwa kuonyesha kiwango kwa sababu hana uwezo, nadhani labda bado anaendelea
kuzoea mazingira ya hapa na kama akipewa muda zaidi, basi watakuja kumkoma
kwenye michezo ijayo,” alisema Kangwa ambaye ametokea timu ya Highlander ya
Zimbabwe.
Mavugo azua hofu Simba, kocha apagawa
Sweetbert
Lukonge
KIVUMBI
cha Ligi Kuu Bara msimu wa 2016/17 kinaanza kutimua vumbi leo katika viwanja
vitano tofauti kwa timu 10 kushuka uwanjani kuianza safari ya zaidi ya miezi
nane ya kuwania ubingwa wa ligi hiyo ambao msimu uliopita ulinyakuliwa na
Yanga.
Mechi
hizo tano za ufunguzi wa ligi hiyo zitakazopigwa leo hii ni ile ya Simba dhidi
ya Ndanda FC kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Stand United na Mbao
FC (Kambarage, Shinyanga), Mtibwa Sugar na Ruvu Shooting (Manungu, Morogoro),
Azam FC na African Lyon (Azam Complex, Chamazi) pamoja na Majimaji dhidi ya
Prisons (Majimaji, Songea).
Simba
ambayo imesajili wachezaji 11 msimu huu, watano wakiwa ni wa kimataifa na sita
wazawa, macho na masikio ya mashabiki wake yatakuwa juu ya Mrundi, Laudit
Mavugo ambaye amejiunga nayo hivi karibuni akitokea Vital’O.
Kwa
upande wa Azam FC, mashabiki wake pia watakuwa wakiifuatilia mechi yake hiyo
dhidi ya African Lyon iliyopanda daraja msimu uliopita wakitaka kuona ni jinsi
gani imejipanga kuhakikisha inatwaa ubingwa wa ligi hiyo kwa mara ya pili tangu
kuanzishwa kwake.
Hata
hivyo, Kocha Mkuu wa Simba, Mcameroon, Joseph Omog, ameliambia gazeti hili
kuwa, kikosi chake kipo tayari kwa ajili ya mchezo huo pamoja na mingine yote
inayokuja.
“Tupo
tayari kwa ajili ya mechi hiyo na kila mchezaji yupo tayari kwa vita ili
kuhakikisha msimu huu tunakuwa mabingwa. Wachezaji wa kimataifa ninaweza
kuwakosa kutokana na kutokuwa na vibali vya uhamisho wa kimataifa (ITC) pamoja
na vile vya kufanya kazi hapa nchini.
“Wachezaji
ambao ITC zao hazijafika ni Besala Bokungu, Blagnon Fredric na Method Mwanjale
lakini Mavugo na Mousa Ndusha wao ITC zao tayari tumeshazipata.
“Hata
hivyo nina hofu kuwa ninaweza kuwakosa katika mechi hiyo kutokana na kutokuwa
na vibali vya kufanya kazi hapa nchini kwani taarifa nilizopewa ni kwamba TFF
(Shirikisho la Soka Tanzania) imeagizwa na idara ya uhamiaji hapa nchini
kuhakikisha kila mchezaji wa kimataifa anakuwa na kibali hicho ndipo aweze
kuitumikia timu yake, vinginevyo hawatacheza,” alisema Omog.
Alipotafutwa
Msemaji wa Simba, Haji Manara kuzungumzia suala hilo, alisema kila kitu
kimeshakamilika juu ya wachezaji hao wa kimataifa isipokuwa Bokungu ambaye naye
alikuwa katika hatua za mwisho kupata kila nyaraka inayohusika ili apate nafasi
ya kucheza.
Rais wa
Simba, Evans Aveva hakupatikana kwa kuwa simu yake ilikuwa ikiita tu bila
kupokelewa huku Katibu Mkuu, Patrick Kahemele akiwa hapatikana.
Mwenyekiti
wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe, alipoulizwa juu ya suala
hilo alisema: “Nipo Nairobi, natokea Burundi kufuatilia ITC ya Mavugo ambayo
tayari imeshafika, kwa hiyo mambo mengine yanayohusiana na uhamiaji sina
taarifa nayo, waulize viongozi walioko huko.”
Mapema
jana, Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas, alisema kuwa watu wa uhamiaji walifika
katika ofisi za shirikisho hilo Ilala jijini Dar, juzi na kuwaagiza kuwa
wachezaji wote wa kimataifa watakaoingia uwanjani wanatakiwa kuwa na vibali vya
kufanyia kazi nchini, ikiwa vinginevyo basi mzigo utaiangukia TFF.
Alfred
aliongeza kuwa klabu zote zinatakiwa kuwalipia wachezaji hao ada za leseni
ambayo ni Sh 500,000 kwa kila mchezaji.
CHANZO: CHAMPIONI
0 COMMENTS:
Post a Comment