September 16, 2016

Na Selemani Matola
James Aggrey Siang’a alikuwa ni kocha mwenye misimamo, alikuwa na hasira na hakutaka kuyumbishwa au kuona yeye au mchezaji wake akionewa.

Ilikuwa Morogoro kwenye Uwanja wa Jamhuri tunacheza dhidi ya Polisi Morogoro, sasa kwa kuwa kipindi hicho tulikuwa na upinzani mkali na timu hiyo, siku ya mechi kulikuwa na askari polisi wengi sana uwanjani.


Tukajua zile ni mbinu za kutumaliza kisaikolojia lakini sisi tulitulia na kuonyesha uwezo mzuri tu, mwisho wa mchezo tukashinda mabao 2-0, huku kukiwa na vurugu za hapa na pale.


 Wakati mchezo umeisha kukatokea mabishano kati ya beki wetu, Boniface Pawasa na Ali Moshi wa Polisi Moro, mimi nikaenda kuamua ule mzozo, wakati nawaamua kuna mchezaji wa Polisi akanipiga ngumi ya mgongo.





Kumbe wakati ananipiga, mchezaji wetu Madaraka Selemani alimuona na yeye akamtandika ngumi yule aliyenipiga mimi.

Kuona hivyo, basi wale askari waliokuwa nje ya ‘pitch’ wakaingia uwanjani wakaanza kumkimbiza Madaraka ili wampige, akakimbia lakini alifika sehemu akawa anarudi kinyumenyume, kumbe kuna askari alikuwa amevaa kiraia na ameshika rungu anamvizia Madaraka ambaye alikuwa akisogea upande wake ili amtandike na lile rungu.

Wakati yote hayo yakitokea Siang’a aliyaona, wakati yule askari akijiandaa kunyanyua rungu ampige Madaraka, Siang’a alitoka mbio moja kwa moja akamrukia yule askari aliyevaa kiraia, alimpiga kichwa cha hatari kama vile anaunganisha krosi.

Hasira zote za wale askari zikageukia kwa Siang’a, wakaanza kumpiga, walimpiga sana, baada ya pale alikimbizwa hospitali na kulazimika kushonwa nyuzi nyingi tu, kwa kuwa alikuwa ni mtu wa mazoezi na yupo imara, ndicho kilichomsaidia vinginevyo alikuwa apoteze maisha palepale kwa kile kipigo alichokipata.

Pamoja na kipigo kile, unajua nini kilitokea kwa yule askari aliyepigwa kichwa? (Matola anacheka) Daaa! Alizimika palepale uwanjani, ikabidi akimbizwe hospitali na kugundulika kuwa alikuwa amezimia na amepata maumivu makali ya kichwa.

Kesho yake Mkuu wa Jeshi la Polisi Morogoro akakutana na viongozi wa Simba na wale askari wakazungumza na kuyamaliza kwa kuwa yalikuwa ni masuala ya mpira tu!

Enyimba noma, walimfanyia kitu kibaya
Kuna siku tulienda Nigeria kucheza dhidi ya Enyimba, tulifika siku nne kabla ya mchezo huo. Siang’a alikuwa na kawaida ya kuzungumza na wachezaji mida ya saa sita mchana siku ya mechi, alikuwa akielezea mipango na kutaja kikosi.

Siku ya mchezo huo mpaka kufikia saa nane alikuwa bado kalala tu chumbani kwake, ilipofika saa tisa ikabidi twende na viongozi kujua kulikoni, tulipofika tukamkuta hajiwezi yupo hoi kitandani, akilalamika kuumwa ghafla na mkono mmoja ukawa haufanyi kazi.

Ikabidi nipewe mimi ile listi na maelekezo kadhaa nikaenda kuwaambia wachezaji. Muda wa mchezo alienda uwanjani lakini alikuwa yupoyupo tu hakufanya chochote, tukapigwa mabao 3-0. Ikaonekana kama Wanigeria wamemfanyia kitu.

Alikuwa kiboko ya Yanga
Nakumbuka Yanga walikuwa hawamsumbui kabisa, kwenye mechi nyingi tuliwafunga au kupata sare wakati kabla ya hapo Yanga walikuwa wakiionea sana Simba.



MWISHO

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic