October 5, 2016



Na Saleh Ally
MECHI ya watani wa jadi haiwezi kupita kimyakimya, baada ya sare ya bao 1-1 kumekuwa na gumzo ya mambo mengi yanayoendelea.

Bao la Yanga lililofungwa na Amissi Tambwe limekuwa gumzo zaidi kwa kuwa kabla ya kufunga aliunawa mpira. Lakini Simba pia wamekuwa wakilalama kuhusiana na bao la Ibrahim Ajibu, kwamba mwamuzi aliashiria ameotea lakini haikuwa hivyo.

SALEHJEMBE ilizungumza na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe kutaka kujua maoni yake kuhusiana na mechi hiyo, lakini mwenendo wa kikosi chake.

SALEHJEMBE: Kikosi kinakwenda vizuri, ukiangalia hata msimu uliopita ilikuwa hivi, mkayumba mwishoni. Vipi mmejiandaa na hili?
Hans Poppe: Kwanza nikuambie safari hii tuna kikosi bora zaidi ukilinganisha na misimu mitatu iliyopita. Suala la kuhakikisha tunaanza vizuri na kumaliza vizuri ni la wote na tunaamini tutalifanya.

SALEHJEMBE: Kwa nini unaamini mtalifanya?
Hans Poppe: Wanachama na mashabiki wanaonyesha umoja wa hali ya juu, wakati mwingine wanachangishana, Sh milioni tano kila mechi wakati mwingine inafika hadi milioni kumi. Si kitu kidogo.

SALEHJEMBE: Mechi dhidi ya Yanga mmeonekana ni walalamishi sana, mfano bao la Tambwe, kweli alishika lakini huenda mwamuzi hakuona.
Hans Poppe: Haiwezekani, upande aliogeukia Tambwe mwamuzi ilikuwa lazima aone. Yule mwamuzi msaidizi alisita, lakini Saanya kwa kuwa alinuia aliachia na Tambwe akafunga.


SALEHJEMBE: Huenda lilikuwa tukio la haraka sana.
Hans Poppe: Hapana, ilikuwa inawezekana kabisa kuona tena mwamuzi alipaswa awe makini maana huyu Tambwe imekuwa kasumba sasa, anataka kushikashika mipira na anafunga. Alifunga dhidi ya Coastal Union kwa mkono, akasababisha vurugu kubwa Mkwakwani, wengine hawakumbuki hili. Tena ajabu mnamsifia tu, acheni hivyo atazidi huyu kufanya haya mambo ya kijinga.

SALEHJEMBE: Kumsifia namna gani?
Hans Poppe: Kwamba alifunga vizuri, sijui ndiyo fowadi na hiyo ni kazi yake.

SALEHJEMBE: Ukiangalia wewe, kweli alishika na alikosea. Lakini umaliziaji wake ulionaje, nafikiri ulikuwa na ufundi mwingi.
Hans Poppe: Hakuna cha ufundi wowote, alijipigia tu tena kawaida kabisa. Mwizi ni mwizi tu, huwezi tena kumsifia kaiba halafu kanunua gari nzuri.

SALEHJEMBE: Tambwe alifunga na kwenda kwa mashabiki wa Simba, huoni hili lilikuwa tatizo jingine?
Hans Poppe: Adebayor aliadhibiwa kushangilia kwa mashabiki wa Arsenal wakati akiwa Man City. Hii ni sheria, Tambwe alichangia kuamsha hasira za mashabiki wa Simba ambao tayari walichoka kuonewa msimu uliopita.

SALEHJEMBE: Umesikia watu wanatoa mfano kuwa ni sawa na mabao ya Henry, Maradona?
Hans Poppe: Kama wanafananisha na mabao hayo, basi na Tambwe aombe radhi pia kwa kuwalaghai watu walioingia uwanjani, pia kuwafanyia Simba kitendo kisicho sahihi. Maradona na Henry waliomba radhi. Angeweza kuwa muungwana hata kidogo.

SALEHJEMBE: Ulisema, mmechoka kuonewa, hukufafanua, ni waamuzi au TFF au vipi?
Hans Poppe: Niseme waamuzi na wanaowasimamia wanaliona hili. Ilikuwa Nkongo, kaja yule dada, tukasema mwanamke labda hajui. Sasa huyu Saanya na wasaidizi wake. Tena wote wanakosea upande wetu tu, hapana.

SALEHJEMBE: Kadi nyekundu ya Mkude, inaonyesha hajakomaa. Wewe unaonaje?
Hans Poppe: Kweli Mkude hakuwa sahihi, yeye ndiye angesimama na kuwatuliza wenzake. Kama tungebaki kumi na moja, sidhani kama Yanga wangesimama.

SALEHJEMBE: Mashabiki wenu wamevunja viti, vipi mnashindwa kuwadhibiti. Sasa mnapata hasara kubwa?
Hans Poppe: Tuwadhibiti vipi, tumezungumza nao kwenye matawi. Tumekuwa tukiweka tangazo pale kwenye Uwanja wa Taifa na tunalipia.

SALEHJEMBE: Sasa hawaachi, mnafanyaje sasa?
Hans Poppe: Kwanza ni hasara kwetu. Pia angalia, hawa wanachama na mashabiki pia ni watu wanaochoka. Kuna haja ya Serikali kuweka kamera za CCTV, ili wawaadhibu wahusika moja kwa moja. Maana hatuwezi kuwa na uhakika wanaofanya hivi wote ni Simba.

SALEHJEMBE: Mnahisi wanaweza kuwa Yanga?
Hans Poppe: Ndiyo, inawezekana. Kwani mara ngapi wanakuja kukaa upande wetu. Hizi timu tunatambuana kwa rangi za jezi, akivaa mamluki?

SALEHJEMBE: Sasa mnatakiwa kulipa mamilioni, mnalipaje?
Hans Poppe: Nimesikia sijui inafikia milioni 300, sina uhakika ndiyo sahihi. Lakini sidhani kama ni sahihi, tumewahi kulipa viti na si bei hiyo, tena kitu kibaya zaidi walirudisha vilevile halafu wakavifunga na waya.

SALEHJEMBE: Lakini lazima mlipe, au hamfurahii kulipa?
Hans Poppe: Hatuwezi kufurahia maana wanaofanya vurugu wanaweza kuendelea kufanya. Lakini sisi tuko tayari kuweka wakandarasi warekebishe na kuvurudishia viti. Sidhani kama sawasawa tutaadhibiwa kwa hasira.

SALEHJEMBE: Kwa hasira kivipi?

Hans Poppe: Walioharibu walikuwa na jazba, serikali haipaswi kuwa na jazba katika kuamua hili. Isiwe adhabu ya kutukomoa. Viongozi hatujawahi kuongoza au kupanga vurugu.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic