October 31, 2016


Na Saleh Ally

HIVI karibuni, timu kadhaa zinazoshiriki Ligi ya Mpira wa Kikapu nchini Marekani (NBA), zilianza kuonyesha nia ya kumuwania Mtanzania Hasheem Thabeet Manka.

Timu hizo zilionyesha nia kutokana na maendeleo mazuri ya Hasheem katika timu yake ya Grand Rapid ambako ameendelea kuonyesha ubora wakati ikipambana katika D-League ya NBA.

Wachezaji wengi ambao wanakuwa hawajafanya vizuri, hushiriki katika ligi hiyo. Hasheem, aligoma kusaini kuzitumikia timu kubwa za mpira wa kikapu barani Ulaya katika nchi za Hispania, Ugiriki na kwingineko, akaamua kubaki D-League.

Angekubali kwenda Ulaya, pamoja na donge nono angekuwa gumzo barani humo. Lakini imani yake, ilikuwa ni anaweza kurudi NBA na sasa timu zimeanza kuonyesha nia kwake, jambo ambalo linathibitisha kweli inawezekana kwake.


Hasheem amekodi kocha maalum ambaye ni maarufu na ana uwezo mkubwa na hutumiwa na wachezaji wengine nyota wa NBA. Malipo ya kocha huyo yanaonyesha ni hadi dola 20,000 (zaidi ya Sh milioni 42.4) kwa mwezi kwa wanaomkodisha. Lengo la Hasheem ni kujiweka sawa, awe fiti na mwisho arejee NBA.

Hasheem ni binadamu, Mtanzania wa kwanza kucheza NBA akitokea kwenye nafasi ya draft katika kundi ambalo wako wanaoendelea kufanya vizuri kama DeMar DeRozan na Stephen Curry.

Inawezekana kama binadamu aliteleza, lakini utaona kwa kiasi gani wengi wameishia kumsema, hakuna aliyeonyesha sapoti.

Angalia, hukuwahi kusikia kiongozi hata wa serikali au yule wa mpira wa kikapu akimpa moyo kwamba siku moja atarejea na kipi cha kufanya.


Hasheem anarudi kwenye historia tena, kama ambavyo alifikia hapo, ameanza mwanzo kwa kufanya mazoezi makali, juhudi ya juu na kama kuna sehemu alikosea amepaona na anapafanyia kazi.

Wakati anachipukia, hakukuwa na kiongozi wa serikali wala vyama vya mpira wa kikapu aliyemsaidia, maana wote waliamini hana uwezo. Akapambana sana, mwisho akawa gumzo la taifa, nyota ya taifa, mwanamichezo ghali zaidi kuwahi kutokea Tanzania. Akageuka furaha na faraja ya wote.

Alipoonekana kuyumba, akawa gumzo na sehemu ya watu kuweka maneno ya kila aina. Sasa ameamua kukaa kimya, peke yake tena anapambana tena na inawezekana siku nyingine akarejea tena.

Ana nafasi ya kurejea kwa kuwa rekodi zake za mwisho kwenye D League akiwa na Grand Rapid zinaonyesha ana nafasi.


Lazima tukubali, Hasheem hakubahatisha na anaweza kuwa mtu wa mfano kama utatulia na kujiuliza umbali wa NBA na yeye alifikaje maana kufika hapo, kuanza kupambana na watu kama Kobe Bryant wakati wakicheza na wengine, si kazi ndogo.

Rekodi zake za mwisho na Grand Rapids Drive, zinaonyesha alicheza mechi 23 akiwa na wastani wa pointi 1.2 , rebaundi 1.7, blocks 4, hii ni katika kila dakika 8.3 za mchezo.

Katika msimu uliopita wa D League, wastani wake ulikuwa bora zaidi hadi kufikia pointi 8.6, reboundi akapata 6.2, blocks ikawa pointi 2.4, hii ni ndani ya kila dakika 22.2.


Lakini katika wachezaji wote wa D League, alishika namba tatu kwa kuwa na blocks 117, namba nne kwa kuwa na ubora wa ulinzi akipata pointi 101.3, na namba tano kwenye blocks baada ya kupata asilimia 8.7.

Hasheem mwenye umri wa miaka 29, ni Mtanzania wa aina yake, alijiinua peke yake, kaanguka anaweza kujiinua tena. Jambo ambalo bado tunaweza kujifunza ni kwamba unaweza kupambana ukiwa na watu wachache na ukashinda.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic