October 1, 2016


Kipa wa zamani wa Yanga na Simba, Ivo Mapunda, ameionya Yanga kwa kuiambia kwamba, ikibweteka na kuzubaa ikidhani itaifunga Simba kirahisi leo basi itakula kwao.

Mapunda aliyeichezea Yanga miaka ya nyuma kabla ya kuibukia Simba msimu uliopita, amesema Wanajangwani wakibweteka na matokeo ya ushindi ya mechi za msimu uliopita, watafungwa.

Msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara, Yanga iliifunga Simba katika mechi zote mbili kwa mabao 2-0, leo timu hizo zinakutana kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

“Unajua mechi hizi usizione nje tu, ukiwa ndani zinakuwa na presha kubwa, tena sana, lakini kwa jinsi hali halisi ilivyo, siwezi kusema timu gani itaibuka mshindi, japo sidhani kama itakuwa sare.

“Najua Yanga wataingia uwanjani wakijiamini kutokana na matokeo ya mechi zile mbili za msimu uliopita, niwaambie tu wawe makini kwani wakiwa na akili hiyo watafungwa kwa kuwa wenzao wanataka kulipiza kisasi.

“Lakini kitu kingine naweza kusema wachezaji wa Yanga wametumika sana kwenye michuano ya kimataifa na sasa wamechoka tofauti na Simba,” alisema Ivo ambaye sasa ni mchambuzi wa soka katika runinga.

SOURCE: CHAMPIONI


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic