July 1, 2017



Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) muda wowote kuanzia sasa litatuma maofisa wake kuja nchini kufuatilia tuhuma za utakatishaji fedha alizonazo Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi.

Malinzi na wenzake ambao ni Katibu Mkuu wa TFF, Mwesigwa Selestine na Mkurugenzi wa Fedha wa shirikisho hilo, Nsiande Mwanga walipandishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa makosa 28 yakiwemo ya utakatishaji fedha.

Baada ya kusomewa mashitaka yao mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbord Mashauri katika kesi yao namba 213, watuhumiwa hao walinyimwa dhamana na kupelekwa mahabusu hadi kesi yao itakaposikilizwa tena keshokutwa Jumatatu.

Makamu wa Rais wa TFF, Wallace Karia alisema Fifa tayari ina taarifa za viongozi hao wa TFF kukamatwa na kupandishwa kizimbani kisha kwenda mahabusu.

“Fifa itatuma maofisa wake muda wowote kuanzia sasa na wakifika nchini tutakutana nao katika kikao Jumanne ijayo ili waweze kujua undani wa tuhuma zote walizonazo wenzetu, nadhani kila kitu kitakuwa sawa baada ya hapo.

“Sisi kama TFF hatuwezi kuzungumza lolote kuhusu kukamatwa kwa watu hawa kwani tayari shauri lipo mahakamani,” alisema Karia ambaye pia anagombea nafasi ya urais wa TFF katika uchaguzi utakaofanyika Agosti 12, mwaka huu mjini Dodoma.

Ni wazi kwamba kuna ugumu wa Malinzi kuwahi usaili kwani leo ndiyo mwisho na yeye atafikishwa mahakamani keshokutwa Jumatatu.


Hata hivyo, jana mchana zilivumishwa habari za rais huyo kuwasilisha barua kwa kamati ya uchaguzi ya kuomba udhuru wa kutofanya usaili katika siku zilizopangwa ili afanyiwe Jumatatu ijayo.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Wakili Revocatus Kuuli alikanusha uvumi huo jana jioni.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic