April 18, 2019


WAKATI uongozi wa Simba ukiwa kwenye harakati za kumuongezea mkataba kiungo wake mchezeshaji, Haruna Niyonzima, habari zinasema kuwa ishu hiyo mwenyewe ameiweka kando kutokana na harakati za kuwania ubingwa zikiwa zimepamba moto.

Niyonzima ambaye mkataba wake unamalizika mwishoni mwa msimu huu, hivi sasa viongozi wa Simba wanahaha kumuongezea mapema baada ya kukoshwa na kiwango chake alichokionyesha kwenye michuano ya Kombe la Ligi ya Mabingwa Afrika.

Chanzo kutoka ndani ya Simba kinadai kuwa, licha ya hivyo, lakini kumekuwa na mvutano wa viongozi ambapo wengine wanataka Niyonzima aondoke na wengine wakitaka aendelee kuwepo kikosini hapo.

“Kama unavyojua mkataba wa Niyonzima unamalizika, kuna viongozi wanataka aongezewe na wengine wanapinga wakitaka aondoke, sasa kumekuwa na mvutano mkubwa sana jambo ambalo linawaumiza watu vichwa.

“Lakini mwenyewe amesema hawezi kusaini sasa mpaka ahakikishe lengo lake la kuipa ubingwa Simba linatimia kwa sababu kuna mechi ngumu mbele hivyo anataka kuweka mawazo yake huko na sio kwengine,” kilisema chanzo hicho.

Championi lilipomtafuta Niyonzima kuzungumzia ishu hiyo ya mkataba, alisema: “Kwa sasa siwezi kuzungumzia kuhusu mkataba wangu, ligi ikiisha ndiyo nitaweka wazi. Niacheni kwanza niipe ubingwa timu yangu.”

CHANZO: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic