October 31, 2014




Na Saleh Ally
KIUNGO mkongwe nchini Amri Kiemba yuko kwenye mgogoro na uongozi wa klabu yake kwa madai kadhaa ambayo yanaunganishwa na utovu wa nidhamu.


Kiemba anatuhuma nyingi za chinichini, lakini kati ya hizo, lililozungumzwa ni kuhusiana na kuonyesha kiwango cha chini katika mechi anazoichezea Simba.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Pope yeye alisema hadharani kabisa kuonyesha hafurahishwi na jambo hilo.

Pia akasisitiza kwamba, alipoingia Kiemba katika mechi dhidi ya Prisons, wenyeji wakasawazisha kwa kuwa yeye alifanya uzembe. Hata hivyo, Hans Poppe, alisisitiza alihadithiwa ilivyotokea.

Siku moja baadaye uongozi wa Simba kupitia Kamati ya Utendaji ulitangaza kuwasimamisha Shabani Kisiga, Haroun Chanongo na Amri Kiemba.

Leo ndiyo itakuwa siku ya hukumu watakapokaa na uongozi na kila mmoja kuzungumza alichonacho kabla ya kuangalia kipi sawa na kipi si sahihi.

Kabla hata hawajakaa, Kiemba tayari amehojiwa na vyombo vya habari na kuweka wazi kwamba kama riziki yake na Simba itakuwa imefikia mwisho, basi hana lolote la kupinga. Kwa maneno hayo, ni sahihi kusema Kiemba yuko tayari kwa lolote.

Taarifa kutoka ndani ya Simba zilieleza kwamba tayari Kiemba alihojiwa na baadhi ya viongozi wa Simba, kwamba kwa nini amekuwa akicheza chini ya kiwango akiwa na Simba, halafu anafanya vizuri akiwa na Taifa Stars.

Yeye akawajibu kwamba, akiwa Taifa Stars hana presha na anacheza kwa kufuata maelekezo ya mwalimu na si kufuata anachotaka mwalimu na wengine.

Inawezekana ni fumbo, wanachotaka wengine ni kina nani, viongozi wa Simba au kina nani? Rafiki zake Kiemba au vinginevyo lakini inaonyesha viongozi watakuwa wamemuelewa ana maanisha nini!

Neno lake kama riziki imeisha pia lina tafsiri kubwa sana, kwamba Kiemba anaona anaweza kuondoka. Hilo si tatizo, lakini kuna kila sababu ya viongozi kabla ya kukaa na Kiemba, basi watafakari.

Kwamba kabla ya kuitwa Taifa Stars, alikuwa akifanya vizuri Simba, ndiyo maana akateuliwa katika kikosi hicho cha taifa. Asingeweza kuteuliwa kama angekuwa anaboronga.

Chanzo cha Kiemba kushuka ni kipi, uwezo umepungua, ana matatizo nje ya mpira, kuna kitu hakimridhishi ndani ya Simba?

Pia wanaweza kutafakari mambo mawili, kwanza ni namba anayochezeshwa Simba na ile ya
Taifa Stars ziko sawa?

Pili Simba wajiulize, mfumo wa Makocha Patrick Phiri na ule wa Mart Nooij wa Taifa Stars unafanana au unaweza kuwa sawa kwa Kiemba?

Ninamjua Kiemba kuwa ni mmoja wa watu wasiohofia kusema ukweli bila ya kujali yuko wapi na wakati gani.

Ninavyoona, kama Kiemba angekuwa hafai kwenye mfumo wa Phiri, basi asingekuwa anamtumia kwenye kikosi chake iwe kwa kuanza au kumuingiza kipindi cha pili.

Tukubaliane, kutokana na uzoefu wake mkubwa katika soka, Phiri anajua zaidi kuliko Hans Pope au viongozi wengine wa Simba kuhusiana na Kiemba anafaa au la.

Kuna jambo jingine la kulifanyia kazi pia, kuwa kama Kiemba alicheza soka safi wakati wa Milovan Cirkovic na Zdravko Logarusic, vipi sasa wakati wa Phiri au naye kuna kitu anachompa kinamshinda?

Ndiyo maana Simba wanapaswa kuwa na umakini mkubwa, wafanye uchunguzi wa kutosha kabla ya kuanza kikao cha leo.

Wakati wanashughulikia suala lake pia wenzake, yaani Kisiga na Chanongo wanapaswa kuangalia suala la ukweli na haki. Kwamba kama mchezaji atasema ukweli na wakaona kuna jambo la kulishughulikia, basi wasichukulie jazba au kwenda kwenye kikao wakiwa na maamuzi yao tayari.


1 COMMENTS:

  1. Viongozi Simba wasitafute kujikosha, tatizo ni usajili wa mbwembwe usiozingatia mahitaji ya timu! Okwi sawa, lakini kwanini wasingeangalia mtu wa kumkata kwa nafasi inayolingana au karibu na ya Okwi matokeo yake wanabomoa beki ambayo ni tatizo toka msimu uliopita na ilianza kutulia! Bora wangemuacha Kwizera au Kiongera kuliko Musoti! Watawatuhumu wachezaji wakati beki haijatulia! Huo ni ufinyu wao wa kufikiri kiufundi na kufikiri kishabiki!

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic