January 28, 2015


Uongozi wa Kagera Sugar umeamua kuhamia mkoani Shinyanga na kuachana na Uwanja wa CCM Kirumba kwa kile kilichotajwa kurogwa na wenyeji wa uwanja huo, Toto African, kwa sababu zilizotajwa kuwa waliapa kuhakikisha Kagera haitoki na pointi uwanjani hapo.


Chanzo cha bifu lao ni kwamba Toto wanalipiza kisasi cha Kagera kuwabania misimu miwili iliyopita ambapo iliwafunga katika mchezo wa mwisho, kichapo kilichowashusha daraja Toto African licha ya Kagera tayari ilikuwa imejihakikishia pointi za kubaki ligi kuu.

Kagera Sugar ilihamishia maskani yake kwenye Uwanja wa Kirumba, kutokana na uwanja wao wa nyumbani, Kaitaba, kuwa katika matengenezo lakini vichapo vitatu mfululizo kutoka kwa Azam, Mbeya City na cha juzi dhidi ya Ndanda vimewatia shaka.

Chanzo cha habari kutoka ndani ya Kagera, kimesema kuwa wamekubaliana kuhamia mkoani Shinyanga ambapo mechi zao zote watachezea mkoani humo.

 “Waswahili wanasema lisemwalo lipo, sawa, hakuna mwenye uhakika na kinachosemwa, lakini kadiri mechi zinavyokwenda, tunazidi kuingiwa na hofu. Tulianza kusikia watu wa Toto wakisema hivyo katika mechi ya kwanza na Mbeya, maneno hayo yakaendelea kwenye mechi zilizofuatia, lakini sasa tumeanza kuamini. Kila mmoja anaujua uwezo wa Kagera, kabla ya kuja Mwanza ilikuwa imepoteza mechi moja tu kati ya nane.

“Hivi kweli sisi ndiyo wa kufungwa mechi tatu mfululizo? Haijawahi kutokea timu hii ifungwe namna hii, tumeanza kuamini imani za kishirikina kama siyo mbinu chafu za wenyeji wetu wanazotuambia hadharani,” alisema mtoa habari.

Alipotafutwa Mratibu wa Kagera, Mohammed Hussein, alikiri kusikia maneno hayo na kuongeza kuwa tayari wamehamishia makazi yao mkoani Shinyanga.
“Ni kweli nimeyasikia maneno hayo si mara moja na tumeamua kuhamia mkoani Shinyanga ambapo mechi zote tutakuwa tukichezea  huko,” alisema Hussein.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic