April 28, 2014





SITAKI kabisa kuingia kwenye mkumbo wa kuwalaumu vijana walio kwenye kikosi cha Taifa Stars maboresho wala kocha wao Salum Mayanga.

Kamwe sitawaunga mkono watu waliokuwa wanawazomea pale Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam juzi wakati walipocheza na kufungwa mabao 3-0 na wageni wao Burundi huku Amissi Tambwe na Didier Kavumbagu wakifunga bao moja kila mmoja.
Kweli inauma kwa kuwa timu ya taifa ni yangu mimi, wewe na Watanzania wote. Sasa vipi ifanyiwe mzaha kama ambao Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) wanaona ni kitu rahisi na inawezekana tu kufanyika?
Sina nia ya kupinga wanachokifanya kuhusiana na kuwatafuta vijana mikoani, kuwaweka kambini na mwisho kufanya mchujo wa kuwapata wale ambao wameunganishwa kwenye kikosi cha timu ya taifa na jana kwa mara ya kwanza wakapewa nafasi ya kucheza kwenye kikosi cha kwanza cha Taifa Stars!
Ukiwaona wale vijana wanacheza, utakubaliana nami kwamba kweli wana vipaji, ni sehemu ya vipaji vya wachezaji wengi wa Kitanzania ambavyo hupotelea mitaani, hivyo ni jambo zuri kuvitafuta na kuanza kuvionyesha.
Lakini nasema huo ni mzaha na hasa mambo yanavyopelekwa, haiwezekani na haitawezekana rundo la wachezaji kutoka katika timu za daraja la tatu au zile za mchangani wapewe mafunzo halafu moja kwa moja wanakwenda kuichezea timu ya taifa inayocheza dhidi ya taifa jingine, huu ni mzaha!
Wachezaji ambao hawajacheza hata mechi moja ya ligi, wachezaji ambao hawajui mikikimikiki ya michuano ya kimataifa, wanapewa nafasi ya kuanza kuichezea timu ya taifa.  Ninaamini kuna utani na TFF ya sasa, TFF chini ya Jamal Malinzi, kiasi fulani hawajui maana ya timu ya taifa.
Vijana waliowateua kweli ni wazuri, lakini bado kuna sehemu wanatakiwa wapite ili kufikia hatua ya kuichezea timu ya taifa. Kama kweli sisi tunaishi dunia hii ambayo kuna mataifa mahiri ya soka kama Brazil, Uholanzi, Hispania, Ivory Coast, Ghana na mengineyo, vipi tunakuja na mfumo wetu pekee ambao hakuna anayeweza kuufanya?
Timu ya taifa ni ‘cream’ ya taifa. Wachezaji bora kabisa kwenye nchi, hilo ndilo ninalojua. Sasa TFF wanaweza kusema vijana hao ndiyo bora zaidi kwa nchi hii! Kawaida wachezaji walio na sifa hiyo hupatikana kutokana na ligi ya nyumbani na zile za nchi nyingine.
Tambwe na Kavumbagu wamepata nafasi ya kucheza kwenye timu yao ya taifa kwa kuwa wanacheza ligi ya Tanzania Bara na wanafanya vizuri katika timu zao. Hao waliochezea Taifa Stars wanafanya vizuri wapi? Sasa kigezo cha kupata nafasi hiyo ni kipi? Au utaratibu upi umetumika?
Uzoefu wao hadi kufikia hapo ni upi, vipi wapewe nafasi ya kuichezea Taifa Stars? Si sahihi na timu hiyo si ya kufanyia majaribio ya wachezaji tena katika mechi ambayo inaingia kwenye rekodi kuwa Stars ilicheza mechi ngapi, ikashinda ngapi, ikapoteza na sare ngapi. TFF mnalijua hili? Au ndiyo ilimradi bora twende na kwa kuwa mna washauri wenu wa kuunda timu ambao wanaamua mambo ilimradi tu!
Ndiyo maana nasema Kocha Salum Mayanga na wale vijana hawana kosa lolote, hili ni tatizo la TFF ambayo kama imefanya kitu lakini inaonekana ina haraka sana na inataka vijana wale waonekane tu ili ijulikane imefanya kazi. Huenda ni kutaka kuwaridhisha wadhamini wao, kitu ambacho si sahihi.
Angalia kuna mchezaji mmoja aliingizwa katika kipindi cha pili, ni mshambuliaji. Wakati timu inapambana kusawazisha, angalau kupata bao moja ikiwa imefungwa tatu, yeye alikuwa akiupoza mpira na baadaye kupiga visigino, mashabiki wakaanza kumzomea. Maana alionyesha anavyojali furaha yake kuliko umuhimu wa taifa.
Lazima TFF wakae na kulifanyia kazi hilo, kama wataendelea hivi hata huyo kocha mpya Mholanzi atakuwa hana maana kwa kuwa atapotea njia.
Lakini ukiachana na wachezaji, jamani hebu angalieni jezi ambazo Taifa Stars walivaa kwenye mchezo ule, hazikuwa na uhalisia wowote kuwa inayocheza ni timu ya taifa.

Kwanza zilikuwa na kiwango duni, lakini pia hazikuwa na rangi zetu ambazo tumezizoea kwenye timu ya taifa pamoja na kwamba ilikuwa siku maalum ya Miaka 50 ya Muungano.
Taifa Stars si sehemu ya majaribio, nafikiri mmeelewa. Nitarudi siku nyingine.
Fin.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic