September 19, 2016

Bao la dakika za majeruhi lililofungwa na straika wa Yanga, Donald Ngoma juzi Jumamosi, limemkuna Kocha wa Mwadui, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ na kushindwa kuficha hisia zake baada ya kutamka: “Ngoma amefunga bao kali sana.”

Ngoma alifunga bao hilo katika dakika nne za nyongeza baada ya zile tisini kukamilika kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Mwadui uliopigwa Uwanja wa Kambarage, Shinyanga na kumalizika kwa Yanga kushinda 2-0. Bao lingine lilifungwa na Amissi Tambwe dakika ya tano.


Kabla ya mchezo huo, Julio alikuwa akiwabeza washambuliaji wa Yanga, hasa Ngoma na Tambwe ambapo alitamba vijana wake watawadhibiti na kushindwa kufurukuta, lakini haikuwa hivyo.


Akilizungumzia bao hilo ambalo liliihakikishia Yanga ushindi na kukwea hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi kuu kwa kufikisha pointi kumi, Julio alisema:


“Mazingira ya bao lenyewe yalikuwa hivi; Msuva aliingia na mpira kwenye eneo letu la hatari, akaona hawezi kupiga krosi, akamuachia Niyonzima ambaye alipiga krosi iliyounganishwa na Ngoma kwa kichwa safi, niseme tu Ngoma amefunga bao zuri mimi mwenyewe nimelikubali.


“Lakini bao la kwanza ni uzembe tu wa mabeki wangu kushindwa kuokoa hatari na kumpa mwanya Tambwe kufunga bao la uongozi kabla ya hilo la pili.”


Ikumbukwe kuwa, msimu uliopita timu hizo zilipokutana kwenye uwanja huo, zilitoka sare ya mabao 2-2 ambapo Ngoma aliifungia Yanga mabao yote huku ya Mwadui yakifungwa na Paul Nonga na Bakari Kigodeko.

SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic