April 8, 2015


Mshambuliaji nyota wa Yanga, Amissi Tambwe, amerejesha fadhila kwa kumshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe, kwa kudai alisaidia kuokoa kipaji chake baada ya kuidhinisha auzwe kwenda Yanga.


Tambwe aliuzwa na Simba kwenda kuitumikia Yanga msimu uliopita, lakini usajili huo ulipigiwa kelele sana na mashabiki wa soka wa timu hiyo huku kila mmoja akiamini kuwa Simba hawakuwa sahihi kumuuza.


Hata hivyo, viongozi wa Simba walikuwa wakitupiana mpira mara kwa mara huku kila mmoja akisema kuwa hakuhusika kuuzwa kwa mchezaji huyo, lakini juzi Hans Poppe kupitia makala iliyoandikwa na Gazeti maarufu la Michezo na Burudani la Championi, alisema kuwa yeye ndiye alipitisha usajili huo ili kuokoa kipaji chake.

Hata hivyo, ingawa Tambwe ambaye ni mfungaji bora wa Ligi Kuu Bara msimu uliopita alionekana kujiuliza maswali mengi kuhusiana na kauli ya Hans Poppe akilinganisha na maisha halisi aliyokuwa akiishi klabuni hapo, mwisho akaiunga mkono akitamka kuwa anashukuru kwa hicho alichokifanya kwake maana sasa amerejea kwenye kiwango chake cha awali na mambo yanamnyookea uwanjani.

“Nilikuwa silifahamu hilo na siwezi kumbishia, ila kama alivyosema ninamshukuru, kweli nashukuru kwa alichokifanya kwangu kwa ajili ya kuniokoa. Sasa hivi nipo Yanga nafanya vizuri na nimeanza kurejea kwenye kiwango changu, nashukuru kwa kweli kama alivyokuwa amesema, maana sijui ingekuwaje hapo baadaye.


“Unajua kocha anaweza kukumaliza hivihivi kama ikitokea ameamua kufanya hivyo na wakati ule nisingeweza kumbishia Phiri au kusema lolote kwa kuwa ananiweka benchi kwa sababu yeye ndiyo mwamuzi wa mwisho, ila ndiyo hivyo Mungu naye anaona, kama mtu anafunga mlango mdogo basi yeye anaweza kukufungulia mlango mkubwa na ukanufaika zaidi,” alisema Tambwe ambaye mpaka sasa ana mabao matano kwenye ligi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic