April 18, 2015


Kikosi cha Etoile du Sahel ya Tunisia, kililazimika kuganda Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) kwa dakika 100 kukamilisha taratibu za uhamiaji na walipotoka uwanjani hapo walionekana wakiwa na wapishi, vyakula na maji ya kunywa.


Klabu hiyo imefanya yote hayo ili kukwepa hujuma kutoka kwa Yanga ambayo leo Jumamosi watacheza nayo kwenye Uwanja wa Taifa, Dar katika mechi ya Kombe la Shirikisho.

Kikosi cha Etoile kilitua uwanjani hapo saa 9:00 usiku wa kuamkia jana kwa ndege ya kukodi, lakini kilitumia muda mwingi katika kukamilisha taratibu za uhamiaji na kutoka saa 10:40 alfajiri kueleka Hoteli ya Ledger ambayo zamani ilifahamika kama Bahari Beach iliyopo Kunduchi, Dar.

Waarabu hao walitua na msafara wa watu 56, wakiongozwa na Rais wa Shirikisho la Soka Tunisia (FTF), Krifa Jalel na rais wa klabu hiyo, Charefeddine Ridha. Wengine ni wachezaji 19, viongozi na watu wa benchi la ufundi 13, waandishi wa habari 12 na mashabiki 10. Msafara huo uliondoka uwanjani hapo na mabasi mawili na magari madogo manne.

Muda mfupi baada ya kutua, kiongozi mmoja wa Etoile alimfuata mwakilishi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Raphael Matola ili awasaidie wapewe kipaumbele kwa watu wa uhamiaji ili kukamilisha taratibu lakini alikataa akiwataka kufuata utaratibu uliopo.

Ulipofika wakati wa kutoka, msafara wao ulionekana kuwa na mizigo mikubwa ya vyakula mbalimbali na maji ya kunywa ambapo ofisa mmoja aliyejitambulisha kuwa ni mpishi alisema wamefanya hivyo ili kukwepa hujuma.
“Tumekuja na kila kitu, hapa tuna maji na chakula ambacho tutakula hadi siku tunaondoka, tumepanga kufanya vizuri,” alisema ofisa huyo.

Maofisa wa Etoile waliwakataza wachezaji wao kufanya mahojiano na vyombo vya habari na hata straika wao wa kutumainiwa, Mualgeria, Baghdad Bounedjah alikataa kuzungumza akisema hafahamu Lugha ya Kiingereza.

Alipotakiwa kuzungumzia mchezo huo kwa Lugha ya Kiingereza, Baghdad alijibu kwa lugha hiyo: “Siielewi vizuri Lugha ya Kiingereza, nafahamu Kifaransa kidogo, labda uongee na wenzangu.”

Hata hivyo, Baghdad alionekana akizungumza Kiingereza safi na wenzake ndani ya basi dogo la Hoteli ya Ledger lililowafuata uwanjani hapo. Alipoulizwa atafunga mabao mangapi kwenye mechi ya leo dhidi ya Yanga, Baghdad alionyesha vidole vitatu akiwa na maana atafunga mabao matatu.

Alipofuatwa Kocha wa Etoile, Roger Lemeur, alisema: “Mimi Kiingereza changu siyo kizuri, isitoshe nimechoka na safari hii ndefu.”

Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa Yanga, Jerry Murro alithibitisha kuwa timu hiyo kuja na wapishi, vyakula na maji ya kunywa.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic