LONDON, England
UNAPOAMUA kuzungumza
ukweli mara zote ni lazima utakuuma wewe unayezungumza au ukamuumiza yule au
wale ambao unawasema, hasa kama ikiwa kwa mabaya au kwa kukosoa.
Thierry Henry ana jina
kubwa ndani ya Klabu ya Arsenal na kila shabiki wa timu hiyo analijua hilo,
inaaminika kuwa ndiye mchezaji bora kuwahi kutokea ndani ya klabu hiyo, kwa
ufupi heshima yake ni kubwa klabuni hapo.
Pindi alipotangaza
kustaafu kucheza soka na kuamua kuwa mchambuzi, wengi waliamini kuwa ipo siku
lazima atakwaruzana na timu yake hiyo ya zamani na ndivyo inavyoanza kutokea.
Awali alipoanza kazi ya
uchambuzi ndani ya kituo cha Sky, hakuwa mkosoaji mzuri, lakini muda mfupi
baadaye akaanza kukosoa mambo mengi yakiwemo hata yanayoihusu Arsenal.
Gumzo ni juu ya kauli
yake kuwa Arsenal haiwezi kutwaa ubingwa kwa kumtegemea mshambuliaji Olivier
Giroud, alisema anaamini ni jambo zuri kwa kocha wa timu hiyo, Arsene Wenger,
kusajili straika wa kiwango cha juu kama kweli anahitaji ubingwa wa Premier.
Tangu Henry alipoondoka
klabuni hapo, Arsenal haijawahi kutwaa ubingwa wa Premier kwa muda wa miaka 11,
kumekuwa na sababu nyingi lakini hiyo ya kukosa straika mwenye kiwango cha juu
inatajwa kuwa moja ya sababu kubwa.
Kuhusu hilo Wenger
alijibu kuwa anajua mchezaji wake huyo wa zamani analipwa fedha nyingi na
anapata presha kubwa kutoka kwa mabosi wake wa sasa ili aweze kukosoa na
kutengeneza vichwa vya habari, ndiyo maana anatoa kasoro hizo.
Alichosema Wenger ni
kweli, presha ni kubwa na hata fedha ni nyingi anayolipwa, lakini ndani ya
nafsi yake anajua alichosema Henry kina ukweli.
Kwa asili ya Premier, ni
jambo gumu kuona timu ikitwaa ubingwa ikiwa haina mshambuliaji wa kiwango cha
juu daraja A. Mfano ni ilivyokuwa kwa Chelsea msimu uliopita, ilikuwa na
washambuliaji wa kawaida, lakini safari hii ikamsajili Diego Costa kwa dau
kubwa na ndiye aliyechangia ubingwa kwa kiwango cha juu.
Arsenal imekuwa ikipata
tatizo la kutokuwa na straika daraja A kwa miaka mingi, angalau miaka ya hivi
karibuni Wenger alikuwa akisajili wachezaji wa gharama kubwa tofauti na
ilivyokuwa sera yake ya kutegemea chipukizi wa bei rahisi ili awakuze, ndiyo
maana akapata taji la FA Cup na Ngao ya Jamii.
Giroud naye amemjibu
Mfaransa mwenzake huyo na kuonyesha kupuuzia kile alichokisema, lakini akikaa
chumbani kwake juu ya kitanda na kutulia, anaweza kuwa anaujua ukweli lakini tu
hataki kuonyesha kuwa anaujua.
Kauli ya Henry, ambaye
alifunga mabao 226 katika maisha yake ya Arsenal, ilikuwa hivi: “Nafikiri Giroud
anacheza vizuri lakini unadhani unaweza kutwaa ubingwa kwa kumtegemea yeye?
Sidhani kama inawezekana hiyo.”
Giroud, 28, anaelekea
kumaliza msimu akiwa amefunga mabao 14 katika mechi 26 alizocheza baada ya kuwa
nje kutokana na kuandamwa na majeraha kwa muda wa wiki kadhaa, hivyo kukosa
mechi nyingi ndani ya msimu huu.
Arsenal inamaliza msimu
huu ikiwa katika nafasi ya tatu nyuma ya Chelsea yenye Costa na Manchester City
yenye Sergio Aguero, huku ikiwa mbele ya Manchester United yenye Robin van
Persie na Radamel Falcao ambao hawakuwa kwenye kiwango kizuri.
Hali hiyo ya Falcao na
van Persie inathibitisha kuwa ili ubebe ubingwa au ufanye vizuri, pamoja na
kuwa na kikosi imara lakini straika wa kiwango daraja la kwanza na ambaye yupo
kwenye kiwango kizuri ni muhimu zaidi.
Jina: Olivier Giroud
Kuzaliwa: Septemba 30, 1986
Alipozaliwa: Chambéry, Ufaransa
Urefu: 6 ft 4 in
Nafasi: Mshambuliaji
Jezi: Namba 12
0 COMMENTS:
Post a Comment