May 25, 2015



SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) ndilo lenye jukumu la kuisimamia timu ya taifa, Taifa Stars ambayo ni mali ya Watanzania.

Jukumu hilo linaendana na mambo mengi kwa kuwa TFF wanalazimika kuhakikisha timu hiyo inapata kila kinachohitajika ili mambo yaende vizuri.

Kwa sasa mambo hayaendi vizuri na hata TFF wanalijua hilo, kuwa mambo si shwari hata kidogo na Watanzania hatuna raha na timu yetu.

Kocha Mart Nooij ameyumba kwa kiasi kikubwa. Hajaonyesha njia sahihi ambayo inaweza kuisaidia Taifa Stars katika mambo mengi, ndiyo maana wadau wanapiga kelele ya kutaka aondoke.

Mimi naungana na wale wanaotaka aondoke, licha ya kuwa TFF nao wametoa hoja zao kwamba kama akiondoka katika kipindi hiki, itakuwaje kuhusiana na suala la mechi nyingi zinazokuja kuwa karibu.
TFF wanaona ni sahihi kumbakiza Nooij kwa kuwa mechi inayofuata dhidi ya Misri ni wiki mbili zijazo. 

Baada ya hapo, ndani ya wiki mbili tutacheza na Uganda mara mbili, usisahau pia mechi ya Nigeria. Hadi Septemba 10, kutakuwa na mechi zaidi ya nne. Hiyo ndiyo hofu ya TFF kwamba kama atakuja kocha mpya, itakuwa ni vigumu sana kuwajua wachezaji na kuanza kukipanga kikosi kilivyo! Lakini huenda wangewatumia makocha wazawa kusaidia kumuongoza mgeni.

Wakati TFF bado wanapambana na hili la kumbakiza au kumuondoa Nooij, uchunguzi nilioufanya ndani ya shirikisho hilo, inaonekana kumekuwa na matatizo makubwa ya ulipwaji wa fedha za udhamini kutoka kwa Kampuni ya Bia Tanzania (TBL).

TBL kupitia bia yake ya Kilimanjaro ndiyo wadhamini wakuu wa Taifa Stars na tunapaswa kuwapongeza kwa kuijali timu yetu ya taifa. 

Hiyo ndiyo timu namba moja ambayo inawaunganisha Watanzania wote wanaojitambua na kuipenda nchi na michezo kwa dhati.
Kampuni inayojitokeza kuidhamini timu ya taifa, inapaswa kuthaminiwa. Lakini nimegundua kuna tatizo kubwa unapofikia wakati TBL kutakiwa kuilipa TFF fedha kwa ajili ya maandalizi fulani ya timu ya taifa, jambo ambalo limekuwa likisababisha matatizo makubwa.

Mara kadhaa, TFF wamekuwa wakilazimika kukopa kutokana na TBL kuchelewesha malipo yao. Yaani hawafuati mkataba unavyoeleza, jambo ambalo si sahihi na linaweza likawa linachangia pia kuua morali ya wachezaji.

Taifa Stars iliwahi kuwa katika mgogoro mkubwa na wamiliki wa hoteli moja nchini Zimbabwe, kwa kuwa walikwenda kwa kubangaiza kwa sababu TBL walichelewesha kuwapa malipo yao.

Safari hii Taifa Stars imeboronga kwenye Michuano ya Cosafa kwa kufungwa mechi zote na hakika Nooij ni namba moja katika hili kwa kuwa timu ilishindwa kuonyesha kiwango, ikaondoka Afrika Kusini bila ya kufunga hata bao moja.

Wakati tunapambana na Nooij, nataka na TBL nao wajipime kwamba pamoja na kuwa wadhamini wanaosaidia, mwisho wanaweza kuwa sehemu ya anguko la timu hiyo, kwa kuwa wanaonekana kwa mara ya pili au tatu sasa wanashindwa kulipa fedha kwa wakati mwafaka.

Mara mbili nimeelezwa mwishoni mwa Aprili ndiyo ulikuwa wakati mwafaka wa TBL kulipa fedha zake za udhamini. Haikufanya hivyo na Taifa Stars ikaondoka kwenda Afrika Kusini kwa kujichanga ‘kiaina’.

Hakukuwa na nafasi ya kuwapa wachezaji angalau motisha ya kutosha kwa kuwa hata posho TFF walilazimika kujichanga. Jiulize kama TBL wao ni wadhamini, vipi wanaona ugumu kutoa fedha hizo hadi waingie katika mzozo na TFF?

Lengo lao hakika ni kujitangaza, lakini kama watawahisha fedha ambazo hawana sababu ya kuzichelewesha hawaoni wanaweza kusaidia ufanisi wa Taifa Stars? Au hawajui kuendelea kuicheleweshea malipo ni kuendelea kuizorotesha? Vipi wao wanaona sahihi kudhamini kitu kinachozorota huku wao wakiwa wanachangia?

Itakuwa vizuri sana TBL wakabadilika katika hilo ili kujiepusha kuunganishwa kwenye kundi la wale wanaoizorotesha Taifa Stars kama ambavyo tumeona kwa kocha huyo Mzungu ambaye anaonekana hajui kilichomleta Tanzania.

Lengo la TBL ni kujitangaza kwa uzuri, sasa kama wataendelea hivi, mwisho watakuwa eneo la tatizo na mwisho watashindwa kujitangaza wanavyotaka.





0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic