April 20, 2015


Na Saleh Ally
YANGA wamefanikiwa kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya wageni wao Etoile du Sahel katika mechi ya kwanza ya Kombe la Shirikisho hatua ya 16 bora.
Timu zote mbili zinapambana kuvuka hatua hiyo ya raundi ya pili ili kuingia hatua ya mtoano ambayo anayevuka anaingia katika hatua ya makundi.


Yanga imefanikiwa kufika hapo baada ya kuing’oa FC Platinum ya Zimbabwe kwa jumla ya mabao 6-3 huku Etoile ikiwa imeitoa Benfica ya Angola kwa mabao 2-1.

Sare ya bao 1-1 katika mechi ya kwanza inaiweka Yanga hatarini, kwamba inakuwa na mchezo mgumu katika kuwania kupata nafasi hiyo. Kuna mambo mengi ya kujiuliza kabla ya kupiga hesabu nyingine.

Lakini kabla ya kuanza kupiga hesabu nyingine kwamba Yanga itafanya nini kule Sousse, Tunisia wiki mbili zijazo. Kwanza ni lazima kukubali kwamba timu hiyo ya Tunisia ina kiwango bora zaidi ya Yanga na kuitoa lazima kazi ya ziada ifanyike.

Yanga ilikuwa inacheza nyumbani, lakini ilizidiwa na mipango yake ilikataa. Ilionekana kama vile Yanga ndiyo ilikuwa ugenini na Waarabu hao walikuwa wakicheza nyumbani.

Huenda mchezo huo ndiyo ulikuwa mbaya zaidi kwa Yanga katika mechi zake zote za kimataifa msimu huu kwa kuwa haikucheza vizuri na ukijumlisha na ubora zaidi wa Etoile, Yanga ikaonekana haina kitu.

Mashabiki waliokuwa katika majukwaa ya Uwanja wa Taifa jijini Dar waliingia uwanjani wakiwa wanajiamini na matumaini yao makubwa. Lakini walitoka uwanjani hao wakiwa tofauti kwa muonekano wa nyuso zao na nusu yao wakiwa wamekata tamaa kabisa kwamba, Yanga sasa basi.

Etoile ni timu ya daraja la juu, Yanga si daraja la Etoile lakini ni timu inayopambana kuhakikisha inamuangusha Goliath, jambo ambalo linawezekana tofauti na wengi walivyofikiria.


Upepo:
Si mara ya kwanza timu za Tanzania kuwahi kuing’oa katika mashindano timu kutoka katika nchi za Waarabu kama Algeria, Misri na kwingineko. Ugumu umeongezeka kwa Yanga kwa kuwa imebadili upepo kutoka Kusini kwenda Kaskazini.

Katika bara la Afrika tunajua timu zenye mafanikio makubwa katika michuano ya Caf ni zile kutoka Afrika Kaskazini, Magharibi na kidogo Afrika ya Kati lakini si Mashariki wala Kusini.

Mechi mbili za mwanzo katika Kombe la Shirikisho, Yanga ilikutana na timu kutoka Kusini mwa Afrika ambazo ni BDF ya Botswana na FC Platinum ya Zimbabwe. Etoile imekuwa timu ya kwanza kutoka Kaskazini na tofauti imeonekana, kwamba Yanga inakutana na watu wanaojua mpira.

Inawezekana:
Kuamini Yanga imeishatolewa kutokana na kiwango walichokionyesha ni jambo bay asana kwa binadamu anayeishi karne hii. Mtu wa namna hiyo, muoga wa hivyo hastahili kuishi.

Nini maana ya kupambana? Ndiyo maana suala la kwanza lilikuwa ni kukubali kwamba jamaa wanajua mpira kuliko Yanga kutokana na uzoefu wa michuano hiyo. Umakini wa mpangilio wa klabu yao, utajiri wao na mpangilio bora kabisa wa uendeshaji wa klabu.

Utajiuliza hivi, kweli walionyesha ni bora kuliko Yanga. Lakini walifunga mabao mangapi katika mechi hiyo? Jibu ni bao moja tu ambalo kama ni jibu la matokeo, halitawatofautisha na Yanga kiubora!

Unaweza kusema walikuwa wanataka sare, sawa. Nafasi nyingi walizopata na kupoteza vipi kwa ubora wao walishindwa kuzitumia? Hiyo ndiyo sehemu ya maajabu ya soka, mwisho matokeo ni 1-1.

Yanga inashindwa kupata 2-2 ikiwa uganini Tunisia? Haiwezi kupambana ikashindwa? Yote yanawezekana kwa kuwa Kocha Hans van der Pluijm sasa atakuwa akiwafundisha wachezaji wake kwa taswira sahihi na si picha za video kama walivyofanya awali.

Wanajua ubora wa Etoile ni kiasi gani? Yanga wanajua ni wapi walikosea na huenda ikawa lahisi zaidi kujua nini cha kufanya.

Huenda kuwa na wachezaji wengi majeruhi iliwaathiri katika mechi ya juzi. Kwa kuwa Hassan Dilunga aliwafanya Yanga kucheza pungufu ya mtu mmoja kwa kipindi chote cha kwanza. Alishindwa kukaba wala kuchezesha timu.

Pluijm akawa muoga kufanya mabadiliko kwa kuwa tayari ilionekana Nadir Haroub ‘Cannavaro’ ambaye ni stopper wake alikuwa anachechemea na mwisho akalazimika kumtoa.

Wachezaji karibu wote wa Yanga walionekana kuwa waoga licha ya kuwa wako nyumbani. Walikimbia hata kuuchukua mpira na ilionekana ni kama mechi fulani walioyokuwa wakikwepa lawama.

Etoile kuona YAnga ni waoga licha ya kuwa wako nyumbani. Wao ndiyo wakaanza kucheza mpira na kuwatawala wanavyotaka. Huenda presha hiyo pia angalau kwa asilimia 20 itahamia kwa Etoile wakiwa nyumbani na Yanga wakiitumia vizuri baada ya kujipanga vizuri, inawezekana.

Kikubwa kwa Yanga ni mambo matatu, kwanza kukubali jamaa wanajua, pili wajipange na kuangalia wlaipokosea, hii ni kwa makocha na wachezaji wote na tatu, waamini hakuna kinachoshindikana na mifano iko mingi.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic