April 20, 2015


KILA mmoja wetu anaweza kuwa na mawazo yake tofauti na unavyofikiria wewe au mimi. Hii ndiyo sahihi kwangu. Leo nataka kukuuliza jambo ambalo limekuwa likinishangaza sana na ninakosa majibu.


Nakuuliza swali kuhusiana na Dk Damas Daniel Ndumbaro. Kitaaluma huyu ni mwanasheria, tena ni daktari wa sheria, unaweza kumuita gwiji.

Dk Ndumbaro ni mwalimuwa sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam pia Chuo Kikuu Huria (Out). Daktari huyo wa sheria pia amewahi kufundisha katika Chuo Kikuu cha Kiislam cha Morogoro.

Dk Ndumbaro amewahi kuwa wakala wa kuuza wachezaji anayetambuliwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), ni kati ya wadau ambao wameshiriki mambo kadhaa ambayo yanahusiana na mchezo huo.

Nakumbuka mwaka juzi nilikutana naye makao makuu ya Fifa jijini Zurich, Uswiss wakati nikiwa nimepata mwalimu wa kutembelea na kujifunza mambo kadhaa kuhusiana na shirikisho hilo.

Ghafla nilimuona Dk Ndumbaro akitoka katika moja ya ghorofa za jengo hilo akiwa ameongozana na marefa kutoka nchini Sweden, tukaanza kufanya mazungumzo. Kwangu niliona faraja kumuona Mtanzania mwenzangu akiwa katika eneo hilo.

Binafsi nimekuwa na mtazamo tofauti kuhusiana na Dk Ndumbaro, ninaamini ni kati ya Watanzania wanaotakiwa na Watanzania kwa ajili ya kuendeleza mchezo wa soka kwa kuwa ili tubadilike, tunahitaji watu imara, wenye upeo wa kuleta maendeleo na si kutaka kufaidishwa na mpira au kuchota tu fedha.

Bila ya kupindisha maneno, ninaamini Dk Ndumbaro ana uwezo mkubwa wa kuchangia na wadau wengine kuusaidia mpira wetu kupiga hatua kama tutaachana na ushabiki au akili za uoga.

Naanza na ninaendelea kushangazwa na kesi kati ya Dk Ndumbaro na TFF namna ambavyo imekuwa ikiendelea. Hivi karibuni alifungiwa miaka saba, eti kisa alizitetea klabu zisikatwe fedha zao!

Kwangu niliona ajabu sana, nilipiga kelele sana kwa kuwa haikuwa haki. Klabu zilionyesha unafiki kwa kukaa kimya na kumuacha, akahukumiwa kwa kuonewa kila mmoja aliona.

Akakata rufaa, tuliona alilazimika kutoa Sh milioni moja ili rufaa yake isikilizwe. Kwangu niliona angekuwa hajafungiwa, fedha hiyo ingeweza kusaidia mchezo wa soka katika kuendelea hata kama ni robo hatua. Au ingeshindikana angenunua mboga akala na wanaye nyumbani. Lakini aliitoa kwa kuwa ana mapenzi mchezo wa soka.

Kupokea rufaa ilikuwa lahisi, lakini TFF kuthibitisha kama imepokea rufaa ikawa kizumbumkuti, ikajaribu kupiga chenga hapa na pale, ili mradi tu.
Siku chache zilizopita kimefanyika kituko kingine. Kamati ya rufaa ya TFF ilijaribu kusikiliza kesi ya Dk Ndumbaro bila ya kumuita, kilikuwa ni kitu cha ajabu sana kuingia masikioni na kueleweka kwenye ubongo wa yoyote hata kama angekuwa juha. Mwisho, ikashindikana.

Usisahau, hata wakati anahukumiwa na kufungiwa miaka saba, alikuwa nje ya nchi akiwa amealikwa kufundisha katika chuo kikuu kimoja cha Marekani. 

Alidhulumiwa, hakupewa haki ya kujitetea. Sasa alitaka kudhulumiwa hata haki yake ya kujitetea katika rufaa.
Leo nasikia TFF imemuongezea kesi, kwamba aliandaa mechi wakati akiwa kiongozi wa Simba. Jambo liko wazi, kipindi hicho alikuwa wakala na hakuwa kiongozi wa Simba maana alijiuzulu uenyekiti wa kamati ya uchaguzi ya Simba kabla ya kuchaguliwa tena.

TFF ya Leodeger Tenga ilikuwa inajua ndiyo maana ikamruhusu kuandaa, ikamkopa fedha zake. Ikalipa kiasi nab ado anaidai. TFF ya Malinzi hiyo ni kesi, mimi najua TFF ni moja. Sasa hii inaona sawa, hii si sawa! Ajabu kabisa!

Kwa nini TFF ya Malinzi inamuogopa Dk Ndumbaro, au ndiyo ile hadithi kwamba anataka kuchukua nafasi ya Malinzi?

Sasa itafanya hivi hadi lini? Mimi nilifikiri watu imara ndiyo wajumuishwe na kushirikishwa katika soka kusaidia maendeleo? Sasa aliye na uwezo anaogopwa, mwisho wa hili ni nini? walio imara au bora hawastahili kwenye soka, tunataka waoga na wasio na uwezo ili uwaendeshe na maisha ya soka yaendelee kuwa ya kubahatisha. 

Mimi nimechoshwa na hadithi ya Dk Ndumbaro kuhofiwa utafikiri Simba mla watu wakati inajulikana ubora wa kazi yake na anaweza kuwa msaada katika maendeleo ya soka nchini. TFF mlitafakari hili.



1 COMMENTS:

  1. Huyo ni daktari wa kitabuni sio vitendo ndio maana hata wambura alihofia huo udk wake!

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic