September 3, 2015



Na Saleh Ally
HIKI ndiyo kile kipindi cha siasa, wanasiasa wanajaribu kuzungumza lolote wakiwa na nia ya kupata ‘kiki’.
Hata unieleze vipi, hauwezi kunitosheleza kuamini kwamba kweli wanasiasa wanazungumza mambo kutoka mioyoni mwao wakiwa na lengo la kuwakomboa Watanzania.


Wapo wenye nia hiyo tena ni wachache sana, lakini wengi ni wale ambao wanataka kufanikiwa wanachokitaka na wengi ni nafasi za uongozi.
Siipendi siasa, imejaza watu wengi waongo na wabinafsi, watu wanaotudanganya wananchi kila kukicha na mapenzi yao kwetu ya mayai mabichi, wakati yoyote yanavunjika na kukuchafua.
Kati ya wanasiasa ambao ninawakubali ni Zitto Zuberi Kabwe, sitaki kusema ni mkweli kuliko wote lakini angalau anaweza kuuridhisha moyo wangu namna ambavyo amekuwa akipambana.
Mwanasiasa kijana aliyeipa sifa kubwa Chadema, wakamuona hafai. Safari hii ameingia ACT, yaani kaanzisha chama chake na taratibu kinakwenda, hongera kwake.
Lakini siku chache zilizopita, Zitto ‘alirudi’ nyumbani, kule ambako wanasiasa wanakotokea. Sehemu ambayo wanajiangalia au kudanganya. Sehemu ambayo wanataka kuonyesha ni wazuri sana kwa wananchi bila kujali wengine wataumia vipi.

Akiwa anahutubia huko Mbagala, aliagiza eti TFF iache mashabiki waingie bure katika mechi ya kuwania kucheza Afcon wakati Taifa Stars itakapokuwa inapambana na Nigeria pale kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Waliokuwa kwenye mkutano ule, wakamshangilia kwa nguvu kwa kuwa vyovyote vile, mashabiki watafurahia kuingia bure. Hilo halina ubishi maana mchezo wa soka ni burudani ya wengi.
Mashabiki sawa wanashangilia, huenda wako walimuona muungwana sana. Lakini hakika ukitafakari utaona ndiyo ujanja wa kisiasa kutaka kuitumia tu michezo ili kujifaidisha na huo ndiyo ule ubinafsi ninaousema.
Zitto angekuwa amepata nafasi ya kuwa Katibu Mkuu wa Fat miaka 10 iliyopita asingefanya hivyo. Nilisimama sehemu ya waliompigia debe Zitto alipowania ukatibu mkuu wa Fat, miaka hiyo zaidi ya 10 iliyopita.

Zitto alishindwa na Michael Richard Wambura. Tena kwenye uchaguzi huo hakuwa na nafasi hata kidogo kwa kuwa waliokuwa wakichuana ni Wambura na aliyekuwa katibu wakati huo Ismail Aden Rage ambaye aliangukia pua.
Nilikuwa kwenye timu ya Zitto kwa kuwa niliridhishwa na maneno mazuri aliyoyatoa. Aliyoyapanga na kunuia kuyatekeleza, tatizo hakuwa hata na fedha ya kampeni, ushabiki ulitawala na mazoezi yalimzidi nguvu, akashindwa na mimi nikadondoka.
Sijakutana siku nyingi sana na Zitto, lakini baada ya kauli yake hiyo nilikuwa najaribu kutafakari kama kweli angeshinda siku hiyo, leo akaendelea kubaki kwenye mpira. Je, angekuwa tayari kuachia watu wote waingie Taifa Jumamosi, bure! Naamini isingekuwa hivyo na huenda angekasirishwa sana na kauli ya mwanasiasa kama aliyoitoa yeye, kuwa watu waingie bure.
Vipi Zitto hakusema ACT angalau inalipia hata watu wapatao 2,000 tu na kushauri waliobaki walipiwe na vyama vingine au makampuni fulani.
Bado angeweza kuyashawishi makampuni, wafanyabiashara maarufu au vinginevyo kuwanunulia tiketi Watanzania wengi wapenda soka ukiwa ni mchango wake wa kuongeza nguvu kwa kikosi cha Stars, lakini siyo hicho alichokisema.
Zitto anajua kuwa soka ni gharama, vijana wameandaliwa kwa mamilioni ya fedha ikiwemo kuwasafirisha Uturuki kuweka kambi. Mrisho Ngassa, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wanatumiwa tiketi kwenda na kurudi katika timu zao.
Wanahudhumiwa wanapokuwa jijini Dar es Salaam na Stars inakaa kambini tokea Uturuki hadi hapa nyumbani. Je, ni kweli yote haya Zitto hayajui? Alifikiri kuisaidia TFF angalau kidogo kabla ya kutoa kauli hiyo inayolenga kumuonyesha yeye na ACT wanajali wananchi lakini si TFF?
Je, mwananchi anakubali kwenda uwanjani bure huku akijua akifanya hivyo atawaumiza hata vijana wanaopambana na Nigeria siku hiyo?

Kwangu naona Zitto hakuwa mzalendo, amekuwa mbinafsi, ametaka kuivika TFF ubaya, ametaka aonekane ana huruma sana kuliko wengine wote, jambo ambalo si sawa hata kidogo.
Wengi sana wangehofia kumweleza Zitto ukweli, huenda wataingia na kuuvaaa ubaya ambao kama TFF watatoa kauli katika hilo, watauvaa. Wala sina hofu, namsisitiza Zitto kukumbuka yeye ni mwanamichezo basi anapaswa kuwa mkweli na anayewaonea huruma wanaoisaidia michezo kuliko kuangalia anapata nini kwenye siasa kwa kusema tu ilimradi.
Kweli wako ambao hawawezi kutafakari na wataliona jambo hilo ni sahihi, lakini wako wenye uwezo wa kung’amua kwamba Zitto alifanya siasa lahisi kuwaumiza wanaoihudumia timu ya taifa, jambo ambalo si sawa hata kidogo na itakuwa vizuri hii ikiwa ni mara ya mwisho kutumbukia huko kwa lengo la kujiongezea anachotaka!


1 COMMENTS:

  1. Wanasiasa ni shida na ni wabinafsi!! Na ndio maana wanatumia muda mwingi kuchafuana na kutuchanganya wananchi. Zitto ni mfano mzuri wa akina Slaa, Lipumba nk. It is time wananchi tuwe na upeo wa kuchambua kujua wanatuongopea!! Sema na nyie waandishi hamtusaidii kuchambua badala yake mnakuwa speaker tu!!

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic