May 5, 2013



Na Saleh Ally
UNAMUONA Francis Cheka akiwa ulingoni akipambana, anarusha makonde kadhaa kwa ajili ya kusaka ushindi. Pamoja na kupingwa ngumi kadhaa, wakati mwingine hata kuangushwa lakini anainuka na kuendelea.

Mwisho huibuka na ushindi, awali ushindi wake ulikuwa ukishangiliwa na watu wengi sana, hasa wale walioonekana ‘kuchoshwa’ na ushindi mfululizo wa familia ya akina Matumla ambao walikuwa wakiongoza kutokana na kuwa na vipaji vingi vya mchezo huo katika familia yao.

Huenda wengi waliamini Cheka anaweza kuwa ‘nguvu ya soda’ hasa baada ya kuwashinda wababe wakati huo kama Rashind Matumla na baadaye Maneno Oswald au Mtambo wa Gongo. Lakini akaendelea hivyo kwa kutoa kipigo kikali kwa Hassan Matumla ambaye lilikuwa tegemeo la mwisho la kummaliza bondia huyo wa Morogoro.

Wakati Cheka akizipiga na Japhaet Kaseba, wengi waliamini ulikuwa ni mwisho wake. Lakini wapi, alichokifanya ilikuwa ni zaidi ya ‘sterlling’ anayetaka kulipa kisasi zaidi ya ‘jambazi’.

Alimpiga alivyotaka na kushinda hadi mmoja wa mashabiki anayejulikana alipopanda jukwaani na kuvuruga pambano. Lile la marudiano, halikufanyika.


Kama ambavyo wengi walichoshwa na ushindi wa akina Matumla, huenda sasa wamechoshwa na ule wa Cheka. Tena inaonekana ‘raia’ wa Dar es Salaam ndiyo hawataki kumuona tena Cheka akishinda.

Awali ilikuwa ni watu wa Keko ambao walikuwa na upinzani mkubwa na wale wa Kinondoni ambao wao walimuunga mkono Cheka. Lakini baada ya kumchapa Kaseba, akawa adui wa Kinondoni.

Sehemu nyingine maarufu kwa mchezo wa ngumi ni Manzese jijini Dar es Salaam. Usiku wa kuamkia jana, Cheka amevunja kambi hiyo, amempiga Thomas Mashali kwa knockout (KO) katika raundi ya 10 na kumaliza kabisa ndoto za mabondia wa kumshinda.

Wakati akipigana na Mashali, ilionekana wazi Cheka sasa ni adui wa Dar es Salaam, hana ugomvi lakini ujuzi wake unasababisha asiwe na mpinzani unamfanya aonekane adui.

Lakini ukweli Cheka ni shujaa wa taifa, ndiye bondia wa kulipwa anayeliwakilisha vilivyo taifa letu, waulize mabondia wote kutoka sehemu mbalimbali barani Afrika waliopigana naye, wana taarifa zake.

Amekuwa akifeli kwa mabondia wa Ulaya, inawezekana maandalizi ya michezo ya kimataifa ikawa tatizo kwake, lakini kocha wake, Abdallah Saleh ‘Komando’ ambaye ni mwanajeshi mstaafu anajitahidi vilivyo kumsaidia kijana wake kuendelea kuwa imara.

Bado Cheka anahitaji sapoti, si kutoka Morogoro pekee anakotokea, badala yake ni nchi nzima kwa kuwa ndiye mwakilishi anayeing’arisha Tanzania katika mchezo huo baada ya kuzeeka na kupoteza umaarufu kwa Rashid Matumla ambaye pia anastahili kupewa heshima kubwa.

Kwa mabondia wanaochapwa na Cheka kila kukicha, si sahihi kuvizia ‘uzee’ wake wapate nafasi ya kulipa kisasa, lakini lazima wajifunze kwa kuwa Cheka si malaika na si sahihi kuamini ushirikina unamsaidia kuwa bora.

Nani hufanya mazoezi kama yeye, maandalizi yake ni zaidi ya pambano. Mabondia wengine hawafanyi hivyo na wanalijua hilo, lakini wanataka kushinda kwa ndoto.

Kushinda bila ya maandalizi ya kutosha hasa kujituma kwa kocha na bondia mwenyewe si rahisi. lazima kuwe na uungwana wa kukubali anachokifanya Cheka na wanaotaka mafanikio wanaweza kujifunza kwake.

Kumchukia kwa kuwa anatokea Morogoro na wewe ni wa Dar es Salaam ni sawa na kuisaliti Tanzania. Washauri mabondia unaowashabikia wajifunze kutoka kwake, alichofanya yeye si ndoto za mchana, amejituma kufikia alipo pamoja na kwamba aliishi maisha ya shida ya kuishi kwa kuokota na kuuza chupa mitaani.

Cheka ameleta mapinduzi ambayo wengi mmekuwa wavivu kufungua kurasa za kitabu chake kusoma kilichomo. Mnaona ‘kava’ lenye picha linatosha kuwaeleza kila kilichopo, kosa kubwa. Cheka ni shujaa wa taifa letu.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic