December 16, 2013

ANDY COLE AKIZUNGUMZA NA SALEH ALLY KATIKA MAHOJIANO MAALUM. YUKO HAPA NCHINI KWA AJILI YA KAMPENI YA MIMI NI BINGWA INAYOENDESHWA NA KAMPUNI YA AIRTEL TANZANIA



Na Saleh Ally
IMEKUWA si rahisi kwa wapenda soka wengi kukumbuka kwamba maisha ya soka ya mshambuliaji Andrew Alexander Cole, maarufu kama Andy Cole, yalianzia Arsenal.


Labda inatokana na kwamba mafanikio makubwa aliyapata akiwa na Manchester United, Cole hajawahi kusahau hata kidogo kuhusiana na Arsenal kwa maana ya maisha yanavyotakiwa kuwa, unapoanzia unapajua, lakini hujui mwisho wake.

Baada ya mambo kutokwenda vizuri na Arsenal, Cole alipelekwa Fulham iliyokuwa daraja la kwanza kwa mkopo na baada ya mechi 13 akiwa amefunga mabao matatu tu, akauzwa katika klabu ya daraja la kwanza ya Bristol aliyoifungia mabao 20 katika mechi 41, hii ni katika msimu wa 1992-93.
AKIKABIDHIWA KIFAA CHA MIMI BINGWA

Uwezo wake uliwavutia Newcastle, maana yake akarejea tena Ligi Daraja la Kwanza England, ikiwa ni baada ya msoto wa zaidi ya miaka mitatu. Akaisaidia kubeba ubingwa na kupanda ligi kuu.

Utaona baadaye akipita Newcastle, Manchester City, Blackburn Rovers, Fulham na Manchester United, Cole anaingia kwenye rekodi baada ya kuweka rekodi ya kuwa mfungaji bora wa pili mwenye mabao mengi zaidi katika Ligi Kuu England, kinara ni Allan Shearer.

Cole yuko hapa nchini katika kuiongezea nguvu promosheni ya Mimi ni Bingwa inayoendeshwa na Kampuni ya Simu ya Airtel na hii ni mara yake ya pili kuja nchini. Mara ya kwanza ilikuwa ni 2011 na alikuja kwa ajili ya Airtel Rising Stars.
Katika mahojiano maalum kati ya Cole na Championi Jumatatu, mshambuliaji huyo nyota enzi hizo, anasema hakuna kitu kinachopatikana kwa urahisi huku akisisitiza, programu ya Airtel Rising Stars ina nafasi ya kuleta mabadiliko katika soka Tanzania lakini bado kuna mambo ya kufanya.
Championi: Unafikiri kuna kitu cha kuiongezea Airtel Rising Star?
Cole: Hiyo ni programu na ina kila nafasi ya kufanya vizuri, lakini watu ndiyo wanatakiwa kuongoza kila kitu kupitia makundi yao.
Championi: Unaweza kufafanua zaidi?
Cole: Mfano wanaokuzwa ni vijana, wanaofanya kazi ya kuwaendeleza ni makocha na wahusika wengine. Wote wanatakiwa kujituma, kuwa na nia ya kuzifikia ndoto zao kwa kuwa Airtel itawapa vifaa vyote kama mipira, jezi na vitu vingine, lakini wao watatakiwa kufanya kitu.

Championi: Wewe unaweza kuwa mfano, uliuzwa hadi timu ya daraja la pili ukitokea ligi kuu ukiwa na Arsenal, ilikuwaje uliweza kuamka na kufikia hapa ulipo?
Cole: Haikuwa kazi rahisi hata kidogo, sikulala kwa kuwa lengo langu lilikuwa ni kufikia ndoto yangu ya kuwa mshambuliaji bora.
Championi: Unafikiri Tanzania ina nafasi siku moja ya kupata mchezaji atakayecheza Ligi Kuu England?
Cole: Inawezekana kabisa, lakini kama nilivyosema kuwa na ndoto, halafu juhudi na maarifa kutaka kuzifikia.
Championi: Labda kama Tanzania tunahitaji muda wa miaka mingapi kufanikiwa katika hilo?
Cole: Nani anajua? Inawezekana ni siku chache zijazo, inategemea na wahusika wanavyoitumia nafasi hiyo bora wanayopewa na Airtel, kwanza waamini si kitu kidogo na wakifanyie kazi.
Championi: Kuja Tanzania kwa Andy Cole si kila kitu, labda nini kingine cha kufanya?
Cole: Kikubwa ni vijana, angalieni sana hilo. Bila kuwakuza na kuwaendeleza hakuna mafanikio, ndiyo maana nasema Airtel wamefanya kitu bora, muwaunge mkono.
Championi: Tukirudi England, umekuwa na mafanikio makubwa, mmoja wa wafungaji bora katika historia, umecheza timu kubwa kama Arsenal, Man United, Man City. Vipi Liverpool, hukuvutiwa nayo?
Cole: (Tabasamu), inawezekana lakini ukweli ni kwamba nimecheza Manchester United kwa mafanikio makubwa. Sidhani kama nilihitaji tena kwenda Liverpool, ila sina chuki nayo.
Championi: Vipi pamoja na kuwa bora, uliamua kumaliza soka lako England, hukupenda changamoto nje ya nchi yako na hasa Hispania au Italia kama ilivyokuwa kwa Beckham, Owen na wengine?
Cole: Kwangu kucheza Premiership ni kitu cha kujivunia, napata kila kitu na ukisema ubora pale ni zaidi. Bado utaona tunacheza na wachezaji wa kila nchi, Ligi ya Mabingwa unakutakana pia na timu za Hispania, Italia.
Championi: Umekuwa bora katika ufungaji mabao, lakini huna umbo kubwa sana, hilo liko vipi?
Cole: Hisia hizo zimekuwa potofu, wengi wanaamini hivyo kwamba watu wenye miili mikubwa ndiyo wanaweza kufunga. Kikubwa kipaji, mazoezi na kujituma, ndiyo maana nimefanikiwa.
Championi: Vipi kufanya kazi na Alex Ferguson, kuna ugumu?
Cole: Ferguson si mtu lelemama, hapendi watu wazembe na siku zote ukiwa unajituma na unafanya kazi vizuri, basi unakuwa rafiki yake mkubwa.
Championi: Kabla ya kuja hapa mwaka 2011, uliwahi kusikia lolote kuhusu mpira wa Tanzania?
Cole: Kweli hapana, nchi hii si maarufu kisoka kama Ghana, Afrika Kusini, Cameroon. Mnahitaji kukua ingawa wakati juhudi zinafanyika, lazima mkubali muda unahitajika, kidogokidogo tu.
Championi: Timu yako ya zamani Manchester United inayumba sasa, unafikiri itakaa vizuri?
Cole: Hiki ni kipindi cha mpito tu, Manchester United itasimama na kufanya vizuri. Kwa mabadiliko ya kocha ilikuwa ni lazima iwe hivyo.
Championi: Vipi wanaweza kuwa mabingwa au angalau kupata nafasi nne za juu?
Cole: Lolote linawezekana, ingawa naweza kusema wakikosa ubingwa, sidhani kama watakosa hata nafasi ya nne. Tusubiri.

MAKOMBE ALIYOWAHI KUTWAA:
Arsenal
Ngao ya Jamii ya FA (1991)
Newcastle United
Ubingwa Ligi Daraja la Kwanza (1992-93)
Manchester United
Ligi Kuu England (mara 5)
Kombe la FA (mara 2)
Ngao ya Jamii (mara 2)
Ligi ya Mabingwa Ulaya (mara moja).

FIN.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic