February 3, 2014



GUMZO kubwa katika kipindi hiki ni kuhusiana na suala la tiketi za elektroniki.

Mashabiki wa soka wanaona ni jambo geni, tumeona katika mikoa ambayo mechi za Ligi Kuu Bara zimechezwa na mfumo wa malipo ya elektroniki umetumika.


Mashabiki wengi wamelalamika kwamba mfumo huo hawauelewi na unawapa wakati mgumu sana kuutumia.

Kuna malalamiko kadhaa kama namna ya upatikanaji kwa tiketi hizo, wengi wanalazimika kwenda kununua sehemu ambazo wanaona ni mbali.

Imezoeleka kuwa, tiketi za mechi zinapatikana uwanjani, mtu anapokwenda ananunua palepale na kuingia zake uwanjani kushuhudia mechi.

Lakini kuna waliolalamika kuwa, wauzaji wanaonyesha dharau kwa wanunuzi, mfano mzuri yule ambaye alikuwa akifanya kazi ya kuuza tiketi kwenye moja ya matawi ya Benki ya CRDB wakati Yanga ilipokaribishwa na Coastal Union mjini Tanga.

Muuza tiketi aliyekuwa na miwani, anaonekana kutumia muda mwingi kuzungumza na simu wakati mashabiki wa soka wakiwa kwa wingi wakisubiri kununua tiketi hizo.

Sitaki kuingia kwenye kundi la wanaoamini kwamba mikataba ya uuzwaji tiketi za elektroniki ni ufisadi au kashfa kwa uongozi wa TFF ya Leodegar Tenga.

Lakini naliangalia suala hilo kwa njia hii, kwamba TFF hii ya Jamal Malinzi, inafanya nini kuhakikisha mfumo huo wa tiketi za elektroniki unakwenda kama inavyotakiwa? Kwa kuwa hata tukiukataa leo, bado utatumika miaka ijayo kwani dunia ndiko inapokwenda.

Sasa TFF ya sasa inauacha kwa kuwa haikubaliani nao au kwa kuwa TFF ya Tenga ndiyo iliingia mkataba huo? Maana kuna mambo mengi ya msingi hayafanyiki.

Zaidi ya kuuzungumzia kizembe, yaani hakuna nguvu inayotumika kuonyesha kuna mabadiliko, hata namna ya ununuzi wa tiketi hizo, TFF inategemea kutoa tu taarifa kwenye vyombo vya habari.

Kama TFF haifanyi lolote, mfano matangazo kwenye runinga, redio au magazeti ili kutoa elimu kuhusiana na mfumo huo mpya, nani atafanya kazi hiyo?

Kinachofanyika ni Bodi ya Ligi au TFF kufanya biashara lakini hawataki kufanya matangazo. Wakati mwingine najiuliza, hata hao CRDB pamoja na uzoefu wao katika biashara, vipi hawatangazi na kufafanua ili kumaliza maswali mengi ya wapenda soka?

Kinachoonekana ni kwamba, wahusika wanataka kufanya biashara, lakini wanahofia gharama ya kuitangaza, kitu ambacho si sahihi hata kidogo.

Tunajua, nchi hii kama ni biashara kwa kuvizia mikutano au taarifa kwa vyombo vya habari si sahihi. Vipi kuhusu kile kitengo cha masoko cha TFF?


Lakini Bodi ya Ligi Kuu, kama ilivyo TFF kwa kuwa wanaingiza fedha, basi lazima wakubali kwamba wana kitu cha kufanya hasa kufafanua, kuutangaza mfumo huo mpya pamoja na faida zake na si kwenda kwa kubahatisha tu.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic