March 12, 2014

YANGA WAKIJIFUA KWENYE UWANJA WA MAZOEZI WA AL AHLY

Na Saleh Ally, Cairo
KLABU za Zamalek na Al Ahly ndiyo unazoweza kuzilinganisha na Yanga na Simba nchini, kama utakuwa unazungumzia suala la ukongwe na maendeleo.

Unaweza kufanya hivyo kwa maana ya historia na kuangalia timu zipi ni kongwe na historia ndefu katika nchi husika, lakini kama ni suala la maendeleo, basi hizo mbili za Misri ndiyo mwili na zile za nyumbani ni vivuli.
UWANJA WA AL AHLY, TAYARI WAMEANZA KUJENGA MWINGINE AMBAO WATAUTUMIA KWA AJILI YA MECHI.

Simba na Yanga ndiyo klabu zinazopaswa kuwa na maendeleo zaidi kuliko nyingine yoyote Tanzania, lakini si hivyo kwa sasa kwa kuwa zimekuwa na mipango duni, isiyo endelevu kwa kipindi kirefu sana.
Yanga iko hapa Cairo baada ya kucheza mechi yake ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya al Ahly, imejifunza mengi kupitia klabu hiyo kongwe ingawa hakuna litakalofanyiwa kazi kwa kuwa kila mara timu hizo, iwe Simba au Yanga, zimekuwa zikisafiri na kukutana na mengi ya kujifunza, wakirejea nyumbani, kila kitu wanakiacha walipokiona, maana yake hawajifunzi zaidi ya kushangaa.
ENEO LA MADUKA KATIKA ENEO LINALOMILIKIWA NA KLABU YA ZAMALEK, NYUMA UNAONEKANA UWANJA WAKE WA MAZOEZI.

Jana asubuhi, Yanga walifanya mazoezi yao wa mwisho kwenye Uwanja wa Al Ahly, hapo ndiyo makao makuu ya klabu hiyo, katikati mwa jiji hili.
Wachezaji walionyesha kufurahishwa na kushangazwa, namna ambavyo wenzao wana mazingira mazuri kupitiliza ya kazi. Ndani ya uwanja kuna vyumba vya kupumzikia ambavyo kuna vitanda 20 kwa mchezaji iwapo atataka kupumzika.
Kuna chumba maalum kwa ajili ya mafunzo au wachezaji kujipumzisha na runinga kubwa imeweka huku makochi yakiwa yamepangwa kwa mpangilio mzuri sana.
Achana na suala kuwa na gym bora, bado wana uwanja wa kisasa kabisa wa kufanyia mazoezi ambao Yanga na Simba, tokea miaka ya 1930 zilipoazishwa, imekuwa ni hadithi tu, huku Watanzania wakiendelea kuonyeshwa ramani za viwanja.
Ndani ya klabu hiyo, kuna mgahawa mkubwa wenye uwezo wa kubeba zaidi ya watu 300 kwa wakati mmoja na biashara yakiwemo maduka mbalimbali yakiendelea.
Kabla ya hapo, Championi Jumatano lilifanya ziara kwenye Uwanja wa Zamalek ambao hauna tofauti kubwa na ule wa Al Ahly, pia wana mgahawa mkubwa ambao unaingiza watu zaidi 200 wakiwa wamekaa safi kabisa.
Lakini Zamalek inamiliki eneo kubwa na limepangishwa maduka, mmoja wa viongozi ameliambia gazeti hili, asilimia 28 ya mapato yao yanatokana na hayo maduka kwa kuwa wafanyabiashara zaidi ya 36 wamekodisha na wanalipa pango.
Yanga ina eneo Mtaa wa Mafia, Kariakoo, hakuna cha maana kinachoendelea. Simba wana maduka makao makuu ya klabu yao, fedha zinaingia matumboni mwa wajanja, ni majanga tu.
Ahly ni kati ya klabu zinazomiliki kituo kikubwa cha runinga barani Afrika. Yanga na Simba hawawezi? Lakini wamewahi hata kufikiri na kufanya mipango ya kuanza taratibu?
Ahly na Zamalek sasa hawana kipato cha mashabiki tena, wanategemea wadhamini na miradi hiyo ndiyo inachukua nafasi ya mapato yao ya milangoni ili kuendelea kulipa mishahara mikubwa ya wachezaji wao.
Jiulize Yanga na Simba, zingeishi vipi kama kungekuwa na adhabu ya mashabiki kutoingia viwanjani? Wakati ni huu, lazima kuwe na mabadiliko na mwendo wa fikra endelevu badala ya kuamini mafanikio ya klabu ni timu kushinda pekee.

Jitanueni kiakili na mnapojifunza, lifanyieni kazi. Simba na Yanga, kuendelea kubaki mlipo ni sawa na mtu mzima au mzee anayelazimisha kupaka rangi nyeusi kwenye ndevu zake nyeupe ili aendelee kuonekana kijana, kumbe umri umeenda.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic