April 7, 2014





MCHEZO wa soka hapa nchini umetawaliwa na vituko vingi zaidi kwa viongozi kuliko hata vile vinavyotokea uwanjani.

Wataalamu wa soka wanasema hivi, soka linapokuwa burudani zaidi uwanjani, ndiyo muonekano sahihi kwamba limekua. Lakini kama migogoro baina ya viongozi na wanachama ikitawala, basi ujue kuna walakini.
Coastal Union ni moja ya klabu kongwe nchini, asili yake ni mkoa wa Tanga na imefanya vizuri sana katika miaka ya 1980 na hata 1990 kabla ya kuanza kuyumba.
Mkoa wa Tanga una watu wa mpira, ni kati ya mikoa ambayo watu wake wana mapenzi ya juu na mchezo huo wa soka hata kama timu zao hazipo ligi kuu.
Safari hii wana timu mbili, Coastal Union na Mgambo Shooting na timu zinazosafiri kwenda kucheza kwenye Uwanja wa Mkwakwani zinajua namna timu hizo ambavyo zimekuwa na ushindani wa hali ya juu.
Tokea Coastal Union imerejea Ligi Kuu Bara, kwa kiasi kikubwa imeongeza changamoto kwenye ushindani wa ligi hiyo ingawa msimu huu imeonekana kuyumba kwa kiasi kikubwa. Inawezekana ni suala la kusubiri kujipanga.
Lakini kuna jambo moja ambalo limekuwa ni la kushangaza zaidi baada ya wanachama kadhaa wa Coastal Union kusumbuka kwa zaidi ya miezi mitatu wakisaka uanachama katika klabu hiyo bila ya mafanikio.
Wanachama hao, wameamua kuandika barua kuipeleka hadi kwa Shirikisho la Soka Tanzania wakidai kwamba wamekuwa wakiomba kupewa uanachama wa Coastal Union lakini juhudi zao zinagonga mwamba na wamemtuhumu Katibu Mkuu wa Coastal Union, Kassim El Siagi, kuwa anawakwamisha.
Wanachama hao wakiongozwa na kiongozi wao, Abdulatif Famau, wamelalamika kwamba kumekuwa na hali ya kuzungushwa kupata uanachama, tena imefikia hatua katibu huyo wa Coastal akiwaambia lazima wajaze fomu na majina yao yajadiliwe kwenye mkutano wa wanachama ili kuwapa nafasi, kichekesho!
Kwa mujibu wa Famau, amesema wamewahi hadi kufika nyumbani kwa katibu huyo na kumuachia maagizo mkewe kwamba wanataka uanachama na wamekuwa wakifanya hivyo bila ya mafanikio na waliamua kwenda nyumbani kwa katibu huyo kwa kuwa imekuwa ni vigumu kumpata akiwa ofisini.
Kinachoshangaza, timu kama Manchester United, Real Madrid, Barcelona, Arsenal, Chelsea na nyingine zinaendelea kusaka wanachama duniani kote. Vipi Coastal Union inaweza kuweka kauzibe kupokea wanachama wapya?
Uchunguzi niliofanya nikagundua kuwa, wanakataa wanachama wapya kwa kuwa uongozi wa Coastal Union una taarifa kwamba kuna watu wanataka kuwa wanachama eti ili waufanyie vurugu uongozi. Hiki ni kichekesho kingine.
Coastal Union inaendeshwa kwa mujibu wa katiba, kama kuna watu watakuwa wanaingia wafanye vurugu ni rahisi kuwathibiti kwa kufuata kanuni, lakini si kuwazuia eti watafanya vurugu, nani ana uhakika na hilo?
Binafsi naona ni tabia ya viongozi waoga na wale wa kizamani ndiyo watakuwa wanahofia changamoto kutoka kwa watu wengine na hasa vijana ndiyo maana Al Siagi na wenzake wanajaribu kupiga chenga kuwapa uanachama vijana ambao wanaamini watahoji mambo kadhaa.
Kuna kila sababu ya kubadilika, kujifunza na kujiamini kwa viongozi hao wa Coastal Union na wakiwa bora basi ni lazima wazikubali changamoto kwa kuwa kila wanachama wanavyoongezeka, maana yake Coastal Union ina nafasi ya kupiga hatua zaidi.
Inapendeza Coastal Union ikiwa na wanachama nchi nzima na baada ya hapo iendelee kujitanua hadi nje ya nchi. Lakini kama leo uongozi utaanza kuhofia kuchukua wanachama wapya tena wanaotokea mkoani Tanga, hiki ni kichekesho cha juu zaidi na lazima kuwe na kipimo sahihi na msisitizo, lazima katiba ifuatwe na ndiyo itakuwa muongozo na si kuipindisha kwa ajili ya kulinda nafasi zenu hata kama Coastal inaporomoka eti kisa ni kukwepa changamoto!
FIN.


1 COMMENTS:

  1. wewe kaseja tunajua simba damu, tena yanga wala hatukutaki

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic