April 7, 2014




Pointi tatu za mezani ambazo timu ya soka ya Standa United ya mkoani Shinyanga ilipewa hivi karibuni na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutokana na kushinda rufaa yake dhidi ya JKT Kanembwa ya Kigoma, zimezua balaa mkoani humo baada ya kuifanya Mwadui FC inayofundisha na Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ kukosa na nafasi ya kupanda ligi kuu.


Licha ya kushinda mchezo wake wa mwisho dhidi ya Polisi Dodoma, Mwadui haijapanda daraja kwa kuwa pointi tatu za mezani za Stand zinaifanya timu hiyo kufikisha pointi 32, mbele ya Mwadui kwa tofauti ya pointi moja.

Julio amegeuka mbogo na kutamka wazi kuwa atahakikisha anapambana mpaka tone la mwisho la damu yake ili Mwadui iweze kupata haki yake. Julio amedai wameonewa na baadhi ya viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na Chama cha Soka Mkoa wa Shinyanga.
Akizungumza na Championi Jumatatu, Julio alisema taratibu ambazo TFF ilizitumia kuipatia pointi tatu Stand United katika rufaa yake waliyokuwa wamekata dhidi ya JKT Kanembwa si sahihi na zilijaa ubabaishaji.
“Sikubaliani kabisa na maamuzi hayo ambayo yamelenga kutunyima haki yetu, haiwezekani TFF wakatoa maamuzi hayo bila ya kusikiliza pende zote mbili, lakini pia majibu ya rufaa hiyo wakayatangaza saa chache kabla ya mechi zetu za mwisho kuanza.
“Hakika TFF hivi sasa kumejaa ubabaishaji ambao unanifanya nimkumbuke Sunday Kayuni, kwani kuna siku Katibu Mkuu wa Chama cha Soka Mkoa wa Shinyanga, alinipigia simu akiwa na Jamal Malinzi (Rais wa TFF).

“Akaniambia kuwa nisijisumbue kwani timu yangu haiwezi kupanda daraja kwa sababu yeye amekuja Dar es Salaam kuchukua ponti tatu za Stand United ambazo waliwakatia rufaa JKT Kanembwa zitakazotunyima ushindi,” alisema Julio.

Alisema kutoka na hali hiyo, kwa sasa TFF kumejaa ubabaishaji tofauti na zamani ambapo alidai kuwa watu wengi walikuwa wakimwona aliyekuwa Mkugenzi wa Ufundi wa shirikisho hilo, Sunday Kayuni kuwa hafai kwa sababu tu ya kuwa mkali na kukataa mambo ya kibabaishaji lakini kwa sasa hali ni mbaya.
Katika hatua nyingine, Julio aliongeza kuwa mpaka sasa yeye anajua kuwa timu yake ya Mwadui ndiyo iliyopanda daraja na siyo Stand United, hivyo atafanya usajili kwa ajili ya michuano ya ligi kuu msimu ujao kama kawaida na TFF wakae wakilijua hilo.
Kabla ya mechi za juzi Jumamosi, Mwadui ilikuwa na pointi 28 na Stand United 26 lakini baada ya timu hizo kushinda, Mwadui ilifikisha ponti 31 na Stand United 29, lakini ushindi wa mezani unaifanya Stand iwe na 32.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic