October 4, 2014


Na Saleh Ally
UKIINGIA kwenye Jumba la Makumbusho la Real Madrid ambalo liko kwenye Uwanja wa Santiago Bernabeu jijini Madrid, moja ya vitu vinavyovutia ni glavu za kipa Iker Casillas.
Hii inaonyesha wanamjali, si unfair kwa Kingereza au injusta kwa Kihispania. Na ndiyo jambo bora kwa maana ya kuonyesha thamani.
Kumjali ni sehemu ya kuonyesha mambo makubwa ambayo ameyafanya Casillas akiwa na klabu hiyo kwa miaka 15.
Miaka hiyo 15 ni ile ambayo ameichezea timu kubwa na kufanikiwa kuibebesha makombe 17 yanayotambulika au kuheshimika.
Mfano Ligi ya mabingwa mara tatu, La Liga makombe matano, Copa de Rey, mawili na mengineyo.
Kipa huyo anaaminika amewashawishi makipa nyota katika nchi mbalimbali duniani wapatao 1,000 kuamua kuwa makipa.
Kwamba hata kama walikata tamaa, lakini waliamua kuwa makipa kwa kuwa waliona yeye anafanya vizuri na wao wangeweza kufanya hivyo au walitamani kuwa kama yeye.
Tena kinachovutia zaidi kwa Casillas kuwa ni kipa ambaye ni nahodha, nahodha mwenye mikono ya bahati.
Asilimia 70 ya makombe yaliyotua Real Madrid tokea mwaka 1999, yamepitia mikononi mwake kwa kuwa alikuwa nahodha.
Katika mechi ya juzi wakati Real Madrid ilipoivaa Lodogoret ya Bulgaria katika mechi ya Ligi  ya Mabingwa Ulaya na kushinda kwa tabu kwa mabao 2-1, Casillas alikuwa nyota wa mchezo kutokana na kuokoa hatari nyingi.

Kinachoumiza kwake, au inaweza hata ikawaogopesha wanasoka wachanga wanaochipukia ni vitendo vya baadhi ya mashabiki wa Real Madrid kumzomea kwenye mechi kadhaa.
Walimzomea kwa kuwa alifanya  makosa kadhaa, wakiamini yalisababisha timu hiyo kupoteza ushindi katika mechi moja au kukaribia kupoteza.
Mashabiki wanaweza kweli kumzomea Casillas! Kweli mpira haujali au hauna haki, Waingereza wanasema unfair na Wahispania wanatamka injusta.
Kweli injusta, si haki kumzomea shujaa wa miaka 15 kwa makosa mawili. Kwa nini binadamu wanasahau sana?
Shukurani ya binadamu ni kwa wakati husika tu? Au huu ndiyo mfumo wa binadamu wanaopenda mpira? Jiulize kuzomewa kunamsaidia au kumshusha zaidi?
Kikubwa ni kutenda haki, kuamini watu wanakosea na wanaokosea wapewe muda kidogo wa kujirekebisha.
Linalotokea kwa Casillas linaweza kuwatokea wachezaji hapa nyumbani lakini kuna mambo mawili ya kujifunza kila upande.
Kwanza kwa wachezaji, Casillas amekuwa akizomewa, lakini hajaacha kujituma na kuendelea kufanya vizuri kwa kuwa anataka kuwaziba midomo wanaozomea, hili ni funzo kwa wachezaji wa hapa nyumbani.
Pili ni kwa mashabiki, kumzomea Casillas ambaye anakuwa anpambana kwa ajili yao, ni kijishambulia wao wenyewe kwa kuwa wakimchanganya, inayoathirika ni Madrid na ukweli ni kwamba, hastahili dhaharu na manyanyaso hasa kutoka wa wale anaoamini anawapenda, pia wanampenda na kumuunga mkono, kwani asipokuwa makini, watammaliza kabisa.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic