November 28, 2014




SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limeanza mchakato wa kutafuta jezi mpya ya timu ya taifa, Taifa Stars.


TFF imeanza mchakato huo mara tu baada ya kuanza kushindwa ule wa kutaka kubadilisha jina la timu ya taifa na wadau wakawa wakali kweli.

Katika mchakato wa kutafuta jezi hizo mpya za timu ya taifa, TFF ilianza kutangaza wabunifu wajitokeze, wachore kitaalamu ili kuwasilisha michoro ya jezi hizo.

Hilo likafanyika na kwa mujibu wa TFF, Watanzania 86 walijitokeza katika ubunifu huo kwa kupendekeza aina ya jezi walizoona ni sahihi.

Jezi 11 za nyumbani, bukta nane za nyumbani, jezi nane za ugenini na bukta tano za ugenini. Maana yake kweli katika kipindi kifupi, watu wamejitokeza.

Hilo ni jambo la kujivunia hasa kama kweli wabunifu hao waliofanya ubunifu ni Watanzania kweli. Kimwenendo, inaonekana wazi TFF hawana mtaalamu wa kuwashauri vizuri kuhusiana na suala hilo.

Kwani wameamua kufanya michakato ya aina mbili. Kwanza wameiweka michoro ya jezi hizo kwenye mtandao wao. Mchakato wa pili ni watu waanze kupiga kura kwa kubofya kwenye picha za michoro na mwisho kura zitaamua zipi ziwe jezi za nyumbani na ugenini za Taifa Stars.

Mimi naona hicho ni kichekesho, ndiyo maana nasisitiza, TFF hawana utaalamu wa masuala hayo na hilo halina ubishi. Hivyo walipaswa kuwapa nafasi watu wanaoweza kuifanya kazi hiyo, nitaukosoa kwa hoja mchakato huo.

Kwanza:
Kuweka kwenye mtandao watu wapige kura kuna uwezekano mkubwa wa mbunifu mmoja ambaye jezi zake zinaweza zisiwe na mvuto zaidi, lakini akawa mjanja katika ushiriki wa kubofya mara nyingi kwa kutumia watu mbalimbali, mwisho akashinda wakati hakustahili.

 Pili:
Kama kweli lengo la TFF ni kuhakikisha Watanzania wote wanashiriki, inajua Watanzania wangapi wanaoingia kwenye mtandao huo wa TFF? Jiulize watu wa Makete, Iringa au Kyaka, Kagera au Dihimba, Mtwara na kwingineko, wana nafasi ya kuingia kwenye mtandao?

Wote hao ni Watanzania, unapoweka hadharani, maana yake unazungumzia usawa. Sasa utapatikana vipi kama kura zitapigwa na watu wa mijini tu, tena wale wanaotumia mitandao tu? Na nani kawaambia TFF mitandao inatosha kufikisha kura?

Tatu:
Tayari TFF imezianika jezi hizo hadharani, inatambua jezi kwenye klabu au timu ya taifa ni biashara. Angalau ungekuwa mchakato wa siri hadi siku jezi inatangazwa, wabunifu wangeweza kupeleka kazi zao kimyakimya, nitakupa sababu.

Kitaalamu katika ulimwengu wa sasa, feki ndiyo gumzo. Kabla hata TFF haijachapisha jezi hizo, zinaweza kuingia mitaani na kuuzwa, tayari ni hasara kubwa.

Hata siku moja hauwezi kusikia Adidas wanatangaza aina fulani ya jezi zao kabla ya kuzitengeneza. Zikiwa tayari na zimeingia mtaani, ndiyo wanatangaza, huo ni mfumo wa kibiashara kote duniani.

Bado utajiuliza, TFF kama inataka kuanika hadharani ‘dizaini’ ya jezi zake, zitatengenezwa na kampuni ipi ambayo itakubali kuchukua kitu kilichosambaa kila sehemu hata kabla ya kukabidhiwa?

Dunia nzima, kwa sasa kila mmoja anaficha ubunifu wa kitu chake. Iwe kuimba, kuchora au vinginevyo hadi unapofikia wakati wa kukitoa kitu husika. Vipi TFF haioni hilo?

Kingine, TFF lazima wakubali kazi yao ni mpira, hivyo wana kila sababu ya kufanya mgawanyo wa kazi. Wawaachie wataalamu kwenye sekta nyingine wafanye kazi ili kufanya mambo yasonge. Kung’ang’ania kila kitu ni kutanguliza siasa kwenye soka.

Pia kama mchakato utaendelea kwa njia hii, inaweza kuiingiza TFF kwenye shimo la kashfa kwamba ilipanga mapema. Maana hata wapiga kura, watakuwa wachache na hawana haki ya kuwawakilisha Watanzania wote wapenda mpira.






1 COMMENTS:

  1. Hapa kuna kaescrowwwwwww fulani either kwa tff or sj!

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic