November 28, 2014



KILA unapokatiza kwenye mitaa habari ni juu ya sakata la fedha za Escrow, kila mtu anazungumza lake, lakini hiki kilichosemwa na straika wa Yanga, Jerryson Tegete, mmmh!


Tegete amesema kuwa wahusika wote walioiba mabilioni ya fedha za mradi wa umeme, wanatakiwa kunyongwa kwa sababu imekuwa mazoea yao kuiba fedha za wananchi.

Sakata hilo limekolea hasa baada ya juzi Kamati ya Hesabu za Serikali na Mashirika ya Umma (Pac) chini ya mwenyekiti wake, Zitto Kabwe, kumtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, mawaziri na viongozi wengine kuwajibika kutokana na kashfa hiyo.

“Hali inayoendelea sasa katika nchi yetu inasikitisha kwa sababu bado Watanzania wengi wanaishi katika maisha magumu kutokana na kodi kuwa kubwa, uchumi wenyewe unazidi kudidimia kila kukicha lakini cha kushangaza, viongozi ambao tunawategemea ndiyo wamegeuka kuwa wezi wa mabilioni ya fedha.

“Fedha hizo zingeweza kusaidia wananchi kupata huduma muhimu kama elimu, maji na umeme.

“Nadhani hatua nzuri ambayo inapaswa kuchukuliwa kwa sababu imekuwa kawaida kwa viongozi kufanya mambo kama hayo ni kunyongwa kwani itasaidia kuwafanya wengine waogope kufanya kama hivyo kwani mambo hayo yanaturudisha nyuma katika maendeleo ya nchi,” alisema Tegete.    

Alipoulizwa Rais wa Simba, Evans Aveva juu ya suala hilo alifunguka: “Hayo mambo ni makubwa mno kwani hadi waziri mkuu yumo, mpira na siasa ni vitu viwili tofauti, hivyo siwezi kusema chochote. Nina imani sheria itafuata mkondo.”


Upande wa Katibu Mkuu wa Klabu ya Yanga, Beno Njovu, alishikwa na kigugumizi na kusema: “Mimi naangalia familia yangu jamani, watoto bado wadogo sana na wananihitaji. Sitaki kuzungumzia hizo habari. Escrow ina mambo mengi sana.”

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic