November 10, 2014


BAADA ya kucheza mechi sita, ikatoka sare sita, ikafunga mabao sita na kufunga sita, Simba imebadili gia katika mechi ya saba.

Simba imeshinda mechi yake ya kwanza ya Ligi Kuu Bara kwa kuwatwanga Ruvu Shooting kwa kuichapa bao 1-0.
Bao pekee la Simba jana limefungwa na Emmanuel Okwi ambalo ni la tatu kwake msimu huu. Mabao mawili aliyofunga mwanzo, yote yalirejeshwa. Jana, likang’ang’ania.
Ushindi wa Simba unaweza kuwa hatua mpya ya kuwabadilisha wapenda soka ambao walianza kuamini eti ushirikina au ‘laana’ inaweza kufanya kazi timu ikashindwa kufunga mabao.
Taarifa zilizokuwa zinasambazwa na kupewa nguvu eti kwa kuwa uongozi wa Simba ulikuwa umewasimamisha wanachama waliokwenda mahakamani, basi ndiyo maana ilicheza mechi sita na zote ikatoka sare.
Tena ikaelezwa kwamba Ukawa wamesema Simba itacheza hadi mechi saba zote itatoka sare na mambo yanaweza kubadilika pale uongozi utakapokubali kukaa mezani na Ukawa na kumalizana nao.
Haya ni kati ya mambo ya ajabu kabisa ambayo hayapaswi hata kutamkwa kwenye mchezo wa soka na watu wanaoamini vitu kama hivyo wanapaswa kusaidiwa.
Mchezo wa soka unapendwa na wengi kutokana na kuwa na burudani za kila aina. Sare za Simba zilikuwa ni sehemu ya burudani lakini kiufundi, kikosi cha Msimbazi hakikuwa kimekaa sawa.
Pamoja na ushindi wa kwanza, ukiangalia bado kuna marekebisho yanatakiwa kufanyika na si suala la Ukawa wala laana.
Mashabiki na wadau wa soka hasa kwa wale waliokuwa wanaamini, wanapaswa kubadilika kuanzia sasa na kuamini soka ni maandalizi ya kutosha, benchi bora la ufundi na ushirikiano kwa pamoja.
Sidhani pia kama ni sahihi kuwatisha viongozi wanaoona kuna matatizo kuwa wasiyafanyie kazi. Wale wanachama walikwenda mahakamani, wanajua katika soka hilo ni tatizo, kuwachukulia hatua watukutu ni sahihi na inapendeza wao wakiomba msamaha na si uongozi eti uwafuate.
Taarifa imeelezwa kuna wazee wa Simba hawana furaha, ndiyo maana pia Simba ilikuwa haishindi. Haya ni maneno ya kwenye chai pia, hayapaswi kupewa nafasi hata kidogo kwa watu wanaokwenda kwenye dunia ya sayansi na teknolojia.
Kama kuna tatizo, basi wazee walishughulikie kiutu uzima na si kuizuia Simba kushinda, kama ingekuwa kweli. Ukawa haikuwa na uwezo wa kuizuia Simba kushinda.
Uongozi wa Evans Aveva hauwezi ukawa umepatia kila jambo hadi sasa. Lakini unaweza kupongezwa kwa mazuri uliyofanya, mojawapo ni hili la kugoma kukutana na Ukawa na kuelekeza nguvu nyingi katika kutatua matatizo ya timu, hilo ndiyo ya msingi na sasa ukweli umethibitika.
Kuna swali lilikuwa linaulizwa na baadhi ya mashabiki wa soka, kwamba “Ukawa wanacheza namba ngapi uwanjani?”
Jibu sahihi limepatikana na wale waliotaka kutumia sare za Simba kama sehemu ya kujinufaisha, sasa biashara imekwisha, turuki kwenye ukweli na kuuangalia mpira kitaalamu badala ya kufanya mambo kwa kubabaisha.
Jambo moja ambalo ninalipiga ni Ukawa kufanyiwa vurugu. Sidhani kama ni jambo zuri kwa kuwa wale wanaendelea kubaki kama Wanasimba. Kama watakuwa na hisia tofauti, haiwezi kuwageuza na kuondoka kwenye klabu hiyo.
Hivyo kama ni wakati wa kurudisha umoja, sasa inawezekana na litakuwa jambo jema kama Ukawa ndiyo watautafuta uongozi halafu wazungumze na kushirikiana na kuijenga Simba moja ambayo kama kuna jambo limetokea basi linaweza kurekebishwa pamoja.
  



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic