November 24, 2014


WIKI iliyopita niliandika kuelezea suala la wachezaji wanaokwenda kupumzika baada ya Ligi Kuu Tanzania Bara kusimama kwa muda.


Ligi itaanza mwishoni mwa Desemba, lakini wachezaji watakuwa wamerejea katika maandalizi mapema kidogo hasa wale wa Yanga na Simba kwa kuwa wana mechi ya kirafiki ya Nani Mtani Jembe.

Wengine kama Azam FC na Yanga pia, watakuwa wanajiandaa na michuano ya Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho. Hivyo maandalizi yao yatakuwa tofauti kidogo na timu nyingine zitakazosubiri ligi kuanza.

Maana yake idadi kubwa ya wachezaji kutoka katika timu 11 za ligi watakuwa kwenye mapumziko marefu ukilinganisha na wale wa timu tatu za Yanga, Simba na Azam FC.

Nilieleza namna ambavyo wachezaji wanaweza kupumzika lakini wakajitunza, wakatambua kwamba watakaporejea kwenye ligi ushindani utakuwa ni mkubwa zaidi ukilinganisha na mechi saba walizokuwa wameishacheza.

Leo nakumbushia zaidi, kwa wale waliopata nafasi ya kuiona video ya kiungo Andrey Coutinho akijifua kwao nchini Brazil, sasa watakubaliana nami kuwa kuna jambo ambalo wachezaji wa hapa nyumbani wanatakiwa kufanya.
Katika video hiyo iliyovuja sehemu mbalimbali, Coutinho anayekipiga Yanga, yuko ‘bize’ akipambana kwa mazoezi makali chini ya kocha ambaye jina lake halikutambulika mara moja.

Coutinho anafanya mazoezi makali ya aina tofauti akiwa katika usimamizi huo wa uhakika kutoka kwa kocha huyo. Kuonyesha kweli kiungo huyo amepania, anafuata kila kitu kwa umakini mkubwa huku akiwa na juhudi ya juu.
Coutinho amejifanyia tathmini baada ya kuuvaa mziki wa Ligi Kuu Bara, amegundua kasoro zake, aliporejea kwao Brazil, alichokifanya ni kuanza kuyafanyia kazi matatizo yake.

Moja ya matatizo hayo ni nguvu, kwani alionyesha uwezo mzuri lakini akashindwa kupambana vilivyo. Mazoezi anayoyafanya akiwa gym chini ya kocha huyo maalum ni sehemu ya kujitambua. Anayafanyia kazi makosa aliyoyaona baada ya kucheza mechi za mwanzo za ligi kuu.

Kutokana na uwezo alionao, Coutinho anaamini kama atazifanyia kazi kasoro zake, basi ana uhakika wa kuwa na kiwango cha juu zaidi, awe tishio, aisaidie Yanga na ikiwezekana alipwe juu zaidi au auzwe kokote kule, ghali zaidi.
Wachezaji wangapi wa Yanga wanafanya kama Coutinho? Wachezaji wangapi wazalendo kutoka Simba, Azam FC, Mtibwa Sugar, Polisi Moro, Stand United, Mbeya City na kwingine wanafanya kama anavyofanya Mbrazil huyo?

Kweli ni muda wa mapumziko, lakini yeye ameamua kuutumia vizuri kufanya marekebisho kwa ajili ya kutafuta ubora. Inawezekana wengi wa wachezaji wazalendo wamerejea vijijini au mikoani walikozaliwa au kukulia kwenda kuwatembelea wazazi na hawafanyi lolote kujiweka fiti.

Achana na kufanya mazoezi kujiweka fiti, lakini inawezekana kabisa hakuna anayefanya jitihada ya alichokosa wakati wa mechi saba za ligi zilizopita, badala yake wanaamini wamerogwa na huenda wako ‘bize’ na waganga wa kienyeji.

Tumeficha sana kuhusiana na masuala ya ushirikina, huu sasa ndiyo wakati mzuri wa kuweka mambo hadharani kwamba hii imezidi. Uchawi wa mpira ni mazoezi, mipango na juhudi. Si kwenda kwa waganga.

Huwezi ukasema Brazil hakuna waganga wa kienyeji, lakini Coutinho ameamua kuingia gym kwa kuwa anajua umuhimu wake. Achaneni na mambo ya hisia, badala yake vitendo na jitihada ziwe dira ya kuwapeleka kwenye mafanikio.

Coutinho hajafikisha hata nusu msimu, ameanza kurekebisha aliyoona amekosea. Wa kwetu hapa mnafanya nini? Hata kama itawaudhi, tafadhali mnaweza kuangalia mazuri na kuyafanyia kazi.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic