December 19, 2014



Na Saleh Ally
WAKATI anamfunga kipa Juma Kaseja wa Yanga katika mechi ya kwanza ya Nani Mtani Jembe, kiungo wa Simba, Awadhi Juma alikuwa anacheza namba 10.


Kocha Zdravko Logarusic alimuamini Juma kucheza namba 10, lakini aliwahi kumpa nafasi ya kucheza namba sita au nane.

Raia huyo wa Croatia alijulikana kwa ukorofi, lakini hakutaka mchezo kazini. Wakati fulani aliwahi kusikika akisema, kama atafukuza wachezaji wote kikosini, basi angebaki na Awadhi.


Wakati anamfunga kipa Deogratius Munishi ‘Dida’ wa Yanga katika mechi ya pili ya Nani Mtani Jembe, Jumamosi iliyopita, Awadhi alikuwa anacheza kiungo mchezeshaji, yaani namba nane.

Baada ya ujio wa Patrick Phiri kutokea Zambia, wapo waliodhani nafasi ya Awadhi isingekuwepo tena lakini kiungo huyo anayetokea Tanzania Visiwani amezidi kuonyesha ni mchezaji wa aina yake.

Wakati akiwa Mtibwa Sugar, zaidi walimtegemea kucheza kama kiungo mkabaji, pia wakati mwingine kama namba saba au kiungo mchezeshaji.


Ameendelea kuonyesha kuwa ndiye kiraka bora zaidi katika kipindi hiki kwa maana ya kuvuka wigo wa namba ipi acheze kwani akiwa Simba amewahi kucheza kama beki wa kulia, namba saba.

Hadi sasa, rekodi zinaonyesha Juma ndiye mchezaji pekee aliyecheza vizuri zaidi katika mechi mbili za Nani Mtani Jembe.

Ndiye mchezaji pekee wa Simba na hata Yanga aliyefunga mabao katika mechi zote mbili za kirafiki za bonanza la Nani Mtani Jembe.

Katika timu kumekuwa na wachezaji ambao nyota zao si kali sana hata kama wanafanya mambo makubwa, mfano mzuri kwa Yanga ni mshambuliaji Justin Mtekere (marehemu). Alikuwa akifunga karibu kila mechi, lakini hakuwa maarufu sana kama wasiofunga.

Awadhi si maarufu kama wachezaji wengine wa Simba ambao huenda wana uwezo wa kucheza nafasi moja tu uwanjani.

Kiungo huyo ana uwezo wa kucheza zaidi ya namba tano uwanjani, iwe ni kwa ajili ya ulinzi au kushambulia.

Hilo halina ubishi kwa kuwa katika kipindi ambacho ameanza kuichezea Simba, tayari makocha kutoka nchi tatu tofauti wameonyesha imani ya juu kwake.

Alianza kuaminiwa na kocha mkongwe nchini, Abdallah Kibadeni ‘King Mputa’, akaaminiwa na Logarusic wa Croatia na sasa Phiri kutoka Zambia.

Ndiyo maana Simba imekuwa na jeuri ya kumuacha Pierre Kwizera kwa kuwa kama Jonas Mkude hatakuwa fiti wakati fulani, wana jeuri Awadhi yupo.

Namba tatu muhimu kwenye ulinzi na ushambulizi, sita, nane na kumi, zote amecheza kwa ufanisi mkubwa na hii inaonyesha ni mmoja wa wachezaji wa kiwango kizuri au cha juu lakini hawana ‘sura’ ya kupendwa na mashabiki.

Nenda mazoezini Simba uone tofauti ya Awadhi na wachezaji wengi wengine. Juhudi anayoonyesha inathibitisha kuwa, amelenga kupata mafanikio, ingawa anajua haonekani.

Wachezaji kama Awadhi, bila ya kuzunguka ni wale wanaotakiwa kupata nafasi katika kikosi cha Taifa Stars, Mart Nooij amtupie jicho.

Wachezaji kama Awadhi ni kati ya wale wanaopaswa kupewa heshima na kuthaminiwa na klabu yake kwa kuwa ni mchapakazi, asiye na maneno, si msumbufu na huenda ana ubora kuzidi hata wachezaji wengi wa kigeni.

Lengo si kumvimbisha kichwa lakini kuonyesha anachokifanya kinaonekana, anaweza kuongeza zaidi ya hapo, akafika mbali na kuwashangaza wengi licha ya kwamba kwa sasa, wengi hawamuoni.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic