December 13, 2014


Na Saleh Ally
INAWEZEKANA kabisa katika mechi zote za Yanga dhidi ya Simba ambazo umewahi kushuhudia iwe uwanjani au ukiwa umekaa pembeni ya runinga, hii ya leo ndiyo utatakiwa kuangalia kwa umakini zaidi.
Mechi ya leo ya Bonanza la Nani Mtani Jembe ndiyo itakuwa na maswali mengi ambayo kila dakika 90 zinavyosonga mbele majibu yatakuwa yanapatikana.
Mechi hiyo inaweza ikatengeneza maswali mengi, kwa kuwa inawezekana kabisa ikashindwa kutoa majibu kwa asilimia mia.

Maswali ni yale yanahohusiana na wachezaji wapya wa kila upande, lakini wale waliokuwepo tokea awali.
Kikubwa ni suala la namna gani wanacheza kwa wachezaji wa zamani, lakini kwa wachezaji wapya, viongozi kupitia kamati zao za usajili, wamefanya kazi yao kwa ufasaha au kubahatisha.
Wachezaji watatu wa kuwatupia macho kwa Yanga kwa upande wa wapya ni Danny Mrwanda, Emerson Roque na Kpah Sherman.

Mrwanda:
Ni Mtanzania, anajulikana kwa uwezo wake wa kufunga. Lakini hii ni mara yake ya kwanza kuichezea Yanga, tena anaanza katika mechi dhidi ya Simba ambayo inajulikana ndiyo ilimpa umaarufu mkubwa na ‘anaipenda’.
Je, ataweza kuonyesha uwezo, atawafurahisha mashabiki wa Yanga kwamba wamefanya kazi sahihi kuiwahi Simba na kumchukua?

Emerson:
Baadhi ya mashabiki wamefanikiwa kuona kazi yake kwenye video akiwa katika mechi mbalimbali, anaonekana ni jembe. Je, ataonyesha hayo akiwa kazini leo dhidi ya Simba?
Itakuwa ni mechi yake ya kwanza, hana sababu ya kusingizia presha kubwa kwa kuwa ni professional kutoka Brazil, kinachotakiwa ni kazi.

Sherman:
Alicheza mechi ya Ligi Kuu Cyprus, wiki iliyopita. Alipofika mazoezini Yanga, akakimbia raundi kumi, hakuna ubishi, yuko fiti.
Umbo lake linavutia kwa mshambuliaji, sasa kinachotakiwa ni kazi. Picha za video zinaonyesha asipofunga, anatoa pasi. Je, leo atafanya hivyo?

Wenyeji:
Kwa upande wa Yanga, wenyeji wapo ambao wanatakiwa kuonyesha mabadiliko au mundelezo mzuri. Simon Msuva, amekuwa chachu ya ushindi ya Yanga. Leo ataendeleza, halafu Mrisho Ngassa ambaye anaonekana mvuto wake umeshuka, atapiga kiki na kuurudisha leo?

Kwa upande wa Simba halikadhalika kuna mambo sawa na yale ya Yanga kwani kuna wachezaji watatu watakuwa wanaichezea Simba kwa mara ya kwanza.

Danny Sserunkuma:
Kiuwezo hakua maswali, lakini anaweza kuupasua ukuta mgumu uliojengwa na Kelvin Yondani, Nadir Haroub pamoja na nyongeza na Mbrazil, Emerson.
Si kazi lahisi, kuonyesha umahiri wake ni lazima afunge au kutoa pasi za mabao, mwisho aipe Simba ushindi.

Juuko Murushid:
Ni beki mpya, timu anayochezea Uganda si kubwa. Hata kama yuko kwenye timu ya taifa, ataiweza presha ya mechi ya watani.

Ni beki, kwelia taweza kupambana na mikiki ya ‘jitu’ kama Sherman, ufundi wa Mrwanda na kasi ya Msuva na Ngassa. Si kazi ndogo na kama kweli Simba wamemtema Peirre Kwizera na kumpa yeye nafasi, basi acha tumuone.

Simon Sserunkuma:
Ni bwa’mdogo wa Danny Sserunkuma. Alikuwa anakipiga Express na akawa Simba shidaaaa wakati walipocheza mechi ya kirafiki iliyoisha kwa sare ya suluhu.

Tatizo la Amissi Tambwe msimu huu limeonekana ni mabao, anachotakiwa ni kuonyesha amekuja kumaliza tatizo hilo. Kama amepewa nafasi ya Mrundi huyo, Mganda huyu lazima aonyesha Simba wamepatia.

Wenyeji:
Shabani Kisiga na Ramadhani Singano ‘Messi’ wana deni, hawakumaliza vizuri mechi saba za mwanzo. Lazima waonyesha mabadiliko na kwamba wao msaada maana Simba inacheza mechi yao ikiwa ina mabadiliko ya kikosi chake kwa asilimia 55, maana haitakuwa na Amri Pierre Kwizera, Amissi Tambwe (kama Simba imeachana nao), Kiemba, Haruna Chanongo, Miraji Adam ambao walianza katika mechi ya kwanza ya ligi dhidi ya Coastal Union.

Ukuta vs fowadi:
Ukiachana na wachezaji hali halisi inaonyesha Yanga ina safu ngumu ya ulinzi, inajumuisha wazoefu na watu wa kazi. Angalia ikiwa hivi, mbili, Mbuyu Twite, tatu-Oscar Joshua, nne-Yondani, tano-Cannavaro na sita-

Emerson:
Kweli ni ukuta wa chuma, lakini Simba pia wana fowadi kamwe hutakiwi kuidharau. Angalia hawa Waganda watatu, Sserunkuma wawili na Emmanuel Okwi. Pia katika mechi kama hiyo huwezi kudharau uzoefu wa Shabani Kisiga na ukali wa Ramadhani Singano ‘Messi’.
Ukitaka kufaidi, hata kama uwanjani, punguza kelele na maneno mengi. Angalia kazi, nani ataifanya, kiungo yupi au kiungo cha timu gani kitapiga chakula kinono.
Ukizungumza sana, dakika 90 za mechi zitamalizika, halafu utatoka uwanjani na maswali kibao.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic